Kutoka 9:1-35

  • Pigo la 5: kufa kwa mifugo (1-7)

  • Pigo la 6: wanadamu na wanyama wapatwa na majipu (8-12)

  • Pigo la 7: mvua ya mawe (13-35)

    • Farao ataona nguvu za Mungu (16)

    • Jina la Yehova litatangazwa (16)

9  Kwa hiyo Yehova akamwambia Musa: “Nenda kwa Farao umwambie, ‘Yehova Mungu wa Waebrania anasema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie.+  Lakini ukikataa kuwaruhusu waende zao, na ukiendelea kuwazuia,  tazama! mkono wangu mimi Yehova+ utaipiga mifugo yenu iliyo shambani. Nitawaletea pigo kali sana farasi, punda, ngamia, ng’ombe, na makundi yenu.+  Na hakika mimi Yehova nitaitofautisha mifugo ya Waisraeli na mifugo ya Wamisri, na hakuna mnyama yeyote wa Waisraeli atakayekufa.”’”+  Zaidi ya hayo, Yehova aliweka wakati hususa, akasema: “Kesho, mimi Yehova nitafanya jambo hilo katika nchi hii.”  Na kesho yake Yehova akafanya hivyo, kila aina ya mifugo ya Wamisri ikaanza kufa,+ lakini hakuna mnyama hata mmoja wa Waisraeli aliyekufa.  Farao alipouliza, aliambiwa kwamba hakuna mnyama hata mmoja wa Waisraeli aliyekufa. Hata hivyo, moyo wa Farao ukaendelea kuwa mgumu, naye hakuwaruhusu Waisraeli waende zao.+  Kisha Yehova akawaambia Musa na Haruni: “Jazeni masizi ya tanuru* kwenye mikono yenu miwili, Musa anapaswa kuyarusha hewani mbele ya Farao.  Nayo yatakuwa mavumbi laini juu ya nchi yote ya Misri, kisha yatakuwa majipu yenye usaha kwenye miili ya wanadamu na wanyama katika nchi yote ya Misri.” 10  Basi wakachukua masizi kutoka katika tanuru* na kusimama mbele ya Farao, naye Musa akayarusha hewani, nayo yakawa majipu yenye usaha yaliyotokea kwenye miili ya wanadamu na wanyama. 11  Makuhani wachawi hawakuweza kusimama mbele ya Musa kwa sababu ya majipu hayo, kwa maana makuhani wachawi na Wamisri wote walikuwa wamepatwa na majipu hayo.+ 12  Lakini Yehova akauacha moyo wa Farao uwe mkaidi, na kama Yehova alivyokuwa amemwambia Musa, Farao hakuwasikiliza.+ 13  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Amka asubuhi na mapema uende ukasimame mbele ya Farao, umwambie, ‘Yehova Mungu wa Waebrania amesema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie. 14  Kwa maana sasa ninayaelekeza mapigo yangu yote niupige moyo wako, niwapige watumishi wako, na watu wako, ili ujue kwamba hakuna yeyote aliye kama mimi katika dunia yote.+ 15  Kwa maana kufikia sasa ningekuwa nimeunyoosha mkono wangu kwa nguvu na kukupiga wewe na watu wako kwa pigo kali sana, nawe ungekuwa umefutiliwa* mbali kutoka duniani. 16  Lakini nimekuacha uendelee kuishi kwa sababu hii hasa: ili nikuonyeshe nguvu zangu na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.+ 17  Je, bado unatenda kwa kiburi dhidi ya watu wangu kwa kukataa kuwaruhusu waende zao? 18  Tazama, kesho wakati kama huu, nitaleta mvua kubwa sana ya mawe ambayo haijawahi kuonekana katika nchi ya Misri tangu mwanzo wake mpaka sasa. 19  Kwa hiyo, waambie watu watoe mifugo yote na vitu vyenu vyote vilivyo shambani na kuviingiza ndani ya nyumba. Kila mwanadamu na mnyama ambaye atapatikana shambani na ambaye hatakuwa ameingizwa ndani ya nyumba atakufa mvua hiyo ya mawe itakapomnyeshea.”’” 20  Mtumishi yeyote wa Farao aliyeogopa neno la Yehova aliwaingiza haraka watumishi wake na mifugo yake ndani ya nyumba, 21  lakini yeyote ambaye hakuzingatia moyoni mwake neno la Yehova aliwaacha watumishi wake na mifugo yake shambani. 22  Sasa Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako kuelekea mbinguni, ili mvua ya mawe inyeshe juu ya nchi yote ya Misri,+ iwanyeshee wanadamu na wanyama na mimea yote ya shambani nchini Misri.”+ 23  Kwa hiyo Musa akainyoosha fimbo yake kuelekea mbinguni, na Yehova akaleta ngurumo na mvua ya mawe, na moto* ukashuka duniani, na Yehova akafanya mvua ya mawe iendelee kunyesha juu ya nchi ya Misri. 24  Kulikuwa na mvua ya mawe, na moto ulikuwa ukiwakawaka katikati ya mvua hiyo. Mvua hiyo ilikuwa kubwa sana; mvua kama hiyo haikuwa imewahi kuonekana Misri tangu nchi hiyo iwe taifa.+ 25  Mvua hiyo ya mawe ilipiga kila kitu kilichokuwa shambani katika nchi yote ya Misri, kuanzia mwanadamu mpaka mnyama, iliharibu kabisa mimea yote na kuvunjavunja miti yote ya shambani.+ 26  Ila tu mvua hiyo ya mawe haikunyesha katika nchi ya Gosheni, ambako Waisraeli waliishi.+ 27  Basi Farao akaamuru Musa na Haruni waitwe, akawaambia: “Wakati huu nimetenda dhambi. Yehova ni mwadilifu, lakini mimi na watu wangu tumekosea. 28  Msihini Yehova ili radi na mvua hii ya mawe kutoka kwa Mungu ikome. Kisha nitakuwa tayari kuwaruhusu mwende zenu, hamtakaa tena zaidi.” 29  Kwa hiyo Musa akamwambia: “Mara tu nitakapoondoka jijini, nitainyoosha mikono yangu mbele za Yehova. Ngurumo itakoma na mvua ya mawe haitaendelea kunyesha, ili ujue kwamba dunia ni ya Yehova.+ 30  Lakini tayari ninajua kwamba hata nikifanya hivyo, wewe na watumishi wako hamtamwogopa Yehova Mungu.” 31  Sasa mimea ya kitani na shayiri ilikuwa imeharibiwa kabisa na mvua, kwa sababu mimea ya shayiri ilikuwa na masuke na mimea ya kitani ilikuwa imechanua maua. 32  Lakini ngano na kusemethi* haikuwa imeharibiwa, kwa sababu haikuwa imekomaa.* 33  Basi Musa akaondoka jijini kutoka mbele ya Farao, akainyoosha mikono yake mbele za Yehova, ngurumo na mvua ya mawe zikakoma na mvua ikaacha kunyesha nchini.+ 34  Farao alipoona kwamba mvua ya mawe, na ngurumo zimekoma, akatenda dhambi tena na kuufanya moyo wake uwe mgumu,+ yeye pamoja na watumishi wake. 35  Na moyo wa Farao ukaendelea kuwa mkaidi, na kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia Musa, Farao hakuwaruhusu Waisraeli waende zao.+

Maelezo ya Chini

Au “kalibu.”
Au “kalibu.”
Au “umefagiliwa.”
Labda ni radi kubwa.
Aina fulani ya ngano ya hali ya chini iliyopandwa nchini Misri.
Au “majira yake yalichelewa.”