Kulingana na Luka 10:1-42

  • Yesu awatuma wale 70 (1-12)

  • Ole kwa miji isiyotubu (13-16)

  • Wale 70 warudi (17-20)

  • Yesu amsifu Baba yake kwa kuwafunulia mambo wanyenyekevu (21-24)

  • Mfano wa Msamaria mwema (25-37)

  • Yesu awatembelea Martha na Maria (38-42)

10  Baada ya mambo hayo Bwana akachagua wengine 70, akawatuma wawili wawili+ wamtangulie katika kila jiji na kila mahali ambako yeye mwenyewe angeenda.  Kisha akawaambia: “Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.+  Nendeni! Tazama! Ninawatuma kama wanakondoo katikati ya mbwamwitu.+  Msibebe mkoba wa pesa wala mfuko wa chakula wala viatu,+ na msimsalimu* mtu yeyote njiani.  Mkiingia katika nyumba yoyote, kwanza semeni: ‘Nyumba hii na iwe na amani.’+  Na kama humo kuna rafiki wa amani, amani yenu itakaa naye. Lakini ikiwa hakuna, itawarudia.  Basi kaeni katika nyumba hiyo,+ na mle na kunywa watakachowaandalia,+ kwa maana mfanyakazi anastahili mshahara wake.+ Msihame kutoka nyumba mpaka nyumba.  “Pia, mkiingia katika jiji nanyi mkaribishwe, kuleni watakachowapa,  na mponye wagonjwa walio huko na kuwaambia: ‘Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.’+ 10  Lakini mkiingia katika jiji nao wasiwakaribishe, nendeni kwenye barabara zake kuu na kusema: 11  ‘Hata mavumbi ya jiji lenu yaliyo kwenye miguu yetu tunayafuta dhidi yenu.+ Hata hivyo jueni kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia.’ 12  Ninawaambia kwamba katika siku hiyo, itakuwa afadhali zaidi kwa Sodoma kuliko kwa jiji hilo.+ 13  “Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! kwa sababu kama matendo yenye nguvu yaliyofanywa kwenu yangefanywa huko Tiro na Sidoni, wangekuwa wametubu zamani, wakiwa wamevaa nguo za magunia na kuketi kwenye majivu.+ 14  Kwa hiyo, wakati wa hukumu itakuwa afadhali zaidi kwa Tiro na Sidoni kuliko kwenu. 15  Nawe Kapernaumu, je, utainuliwa mpaka mbinguni? Utashuka mpaka Kaburini!* 16  “Yeyote anayewasikiliza ninyi ananisikiliza mimi pia.+ Na yeyote anayewapuuza ninyi ananipuuza mimi pia. Isitoshe, yeyote anayenipuuza mimi anampuuza pia Yule aliyenituma.”+ 17  Ndipo wale 70 wakarudi wakiwa na shangwe, wakisema: “Bwana, hata tunawatiisha roho waovu kwa kutumia jina lako.”+ 18  Ndipo akawaambia: “Ninamwona Shetani akiwa tayari ameanguka+ kutoka mbinguni kama radi. 19  Tazama! Nimewapa mamlaka ya kukanyaga nyoka na nge, na juu ya nguvu zote za adui,+ na hakuna kitu chochote kitakachowadhuru. 20  Hata hivyo, msishangilie kwa sababu mnawatiisha roho waovu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”+ 21  Saa ileile akawa na shangwe kubwa kupitia roho takatifu na kusema: “Ninakusifu hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha kwa uangalifu mambo haya wenye hekima na wenye akili+ nawe umeyafunua kwa watoto wadogo. Ndiyo, Ee Baba, kwa sababu umekubali iwe hivyo.+ 22  Baba yangu amenikabidhi vitu vyote, na hakuna mtu anayemjua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemjua Baba isipokuwa Mwana,+ na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.”+ 23  Ndipo akawageukia wanafunzi wake faraghani na kuwaambia: “Yenye furaha ni macho yanayoona mambo mnayoona.+ 24  Kwa maana ninawaambia, manabii na wafalme wengi walitamani kuona mambo mnayoona lakini hawakuyaona,+ na kusikia mambo mnayosikia lakini hawakuyasikia.” 25  Tazama! mtu fulani mwenye ujuzi wa Sheria akasimama ili amjaribu, akamuuliza: “Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 26  Yesu akamuuliza: “Ni mambo gani yameandikwa katika Sheria? Wewe unasomaje?” 27  Akajibu: “‘Lazima umpende Yehova* Mungu wako kwa moyo wako wote kwa nafsi* yako yote kwa nguvu zako zote na kwa akili yako yote’+ na ‘umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.’”+ 28  Akamwambia: “Umejibu vizuri; endelea kufanya hivyo nawe utapata uzima.”+ 29  Lakini, akitaka kujionyesha kuwa mwadilifu,+ mtu huyo akamuuliza Yesu: “Kwa kweli jirani yangu ni nani?” 30  Yesu akamjibu: “Mtu fulani alikuwa akishuka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akavamiwa na wezi, wakamvua nguo, wakampiga, kisha wakamwacha akiwa karibu kufa. 31  Ikatukia kwamba kuhani fulani alikuwa akishuka katika barabara hiyo, lakini alipomwona yule mtu akapita upande mwingine wa barabara. 32  Vivyo hivyo, Mlawi alipofika mahali hapo na kumwona, akapita upande mwingine wa barabara. 33  Lakini Msamaria+ fulani aliyekuwa akisafiri kwenye barabara hiyo alipomwona, akamsikitikia. 34  Basi akamkaribia akayamwagia majeraha yake mafuta na divai, kisha akayafunga. Akampandisha kwenye punda wake akampeleka kwenye nyumba ya wageni na kumtunza. 35  Siku iliyofuata akamlipa msimamizi wa nyumba hiyo dinari* mbili, akamwambia: ‘Mtunze, nami nitakulipa gharama zozote za ziada nitakaporudi.’ 36  Kati ya watu hao watatu, unafikiri ni nani aliyekuwa jirani+ ya mtu aliyevamiwa na wezi?” 37  Akajibu: “Ni yule aliyemtendea kwa rehema.”+ Ndipo Yesu akamwambia: “Nenda ukafanye vivyo hivyo.”+ 38  Walipoendelea na safari, wakaingia katika kijiji fulani. Mwanamke aliyeitwa Martha+ akamkaribisha Yesu nyumbani kwake. 39  Martha alikuwa na dada aliyeitwa Maria, ambaye aliketi miguuni pa Bwana akisikiliza alichokuwa akisema.* 40  Lakini Martha alikengeushwa na kazi nyingi. Basi, akaja na kusema: “Bwana, hujali kwamba dada yangu ameniacha nishughulike peke yangu? Mwambie aje anisaidie.” 41  Bwana akamjibu: “Martha, Martha, unasumbuka na kuhangaikia mambo mengi. 42  Ni vitu vichache tu vinavyohitajiwa au kimoja tu. Maria alichagua fungu zuri,*+ nalo halitaondolewa kwake.”

Maelezo ya Chini

Au “kumsalimu kwa kumkumbatia”
Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Tnn., “neno lake.”
Au “fungu bora.”