Kulingana na Luka 12:1-59

  • Chachu ya Mafarisayo (1-3)

  • Mwogope Mungu, si wanadamu (4-7)

  • Kukiri muungano na Kristo (8-12)

  • Mfano wa tajiri mpumbavu (13-21)

  • Acheni kuhangaika (22-34)

    • Kundi dogo (32)

  • Kukesha (35-40)

  • Msimamizi mwaminifu na msimamizi asiye mwaminifu (41-48)

  • Si amani, bali mgawanyiko (49-53)

  • Uhitaji wa kuchunguza nyakati (54-56)

  • Kutatua mizozo (57-59)

12  Wakati huo, maelfu ya watu walikusanyika hata wakawa wanakanyagana, Yesu akaanza kuzungumza kwanza na wanafunzi wake: “Jihadharini na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki.+  Lakini hakuna jambo lolote lililofunikwa kwa uangalifu ambalo halitafunuliwa, na hakuna siri yoyote ambayo haitafichuliwa.+  Kwa hiyo, mambo mnayosema gizani yatasikiwa nuruni, na mambo mnayonong’ona katika vyumba vya faragha yatahubiriwa juu ya paa za nyumba.  Isitoshe, ninawaambia ninyi, rafiki zangu,+ msiwaogope wale wanaoua mwili na baada ya hilo hawawezi kufanya jambo lolote zaidi.+  Lakini nitawaonyesha yule mnayepaswa kumwogopa: Mwogopeni yule ambaye baada ya kuua ana mamlaka ya kutupa ndani ya Gehena.*+ Ndiyo, ninawaambia, mwogopeni Huyo.+  Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo,* sivyo? Na bado Mungu hamsahau* hata mmoja.+  Lakini hata nywele zote za vichwa vyenu zimehesabiwa.+ Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.+  “Ninawaambia, kila mtu anayenikiri mbele ya watu,+ Mwana wa binadamu pia atamkiri mbele ya malaika wa Mungu.+  Lakini yeyote anayenikana mbele ya watu atakanwa mbele ya malaika wa Mungu.+ 10  Na kila mtu anayesema neno baya kumhusu Mwana wa binadamu atasamehewa, lakini yeyote anayeikufuru roho takatifu hatasamehewa.+ 11  Mtakapopelekwa mbele ya makusanyiko ya watu wote,* maofisa wa serikali, na mamlaka, msihangaike kuhusu jinsi mtakavyojitetea au jambo mtakalosema,+ 12  kwa maana saa hiyohiyo roho takatifu itawafundisha mambo mnayopaswa kusema.”+ 13  Kisha mtu fulani katika umati akamwambia: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi.” 14  Akamwambia: “Ni nani aliyeniweka niwe mwamuzi au mpatanishi kati yenu wawili?” 15  Ndipo akawaambia: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila aina ya pupa,*+ kwa sababu hata mtu anapokuwa na vitu vingi, uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.”+ 16  Ndipo akawaambia mfano huu: “Shamba la tajiri fulani lilizaa vizuri. 17  Basi akaanza kuwaza moyoni, ‘Nitafanya nini kwa sababu sina mahali pa kuhifadhi mazao yangu?’ 18  Kisha akasema, ‘Nitafanya hivi:+ Nitabomoa maghala yangu na kujenga makubwa zaidi, kisha nitahifadhi humo nafaka yangu na vitu vyangu vyote, 19  kisha nitajiambia:* “Una* vitu vingi vizuri ulivyokusanya kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na ujifurahishe.”’ 20  Lakini Mungu akamwambia, ‘Wewe mpumbavu, usiku huu wanautaka uhai wako.* Basi, vitu ulivyohifadhi vitakuwa vya nani?’+ 21  Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejiwekea hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”+ 22  Kisha akawaambia wanafunzi wake: “Ndiyo sababu ninawaambia, acheni kuhangaikia uhai wenu* kuhusu kile mtakachokula au miili yenu kuhusu kile mtakachovaa.+ 23  Kwa maana uhai una* thamani kuliko chakula na mwili kuliko mavazi. 24  Waangalieni kunguru: Hawapandi mbegu wala hawavuni; hawana bohari wala ghala; lakini Mungu huwalisha.+ Je, ninyi si wenye thamani kuliko ndege?+ 25  Ni nani kati yenu ambaye kwa kuhangaika anaweza kurefusha uhai wake kwa mkono* mmoja? 26  Basi, kama hamwezi kufanya jambo dogo kama hilo, kwa nini mhangaikie yale mambo mengine?+ 27  Angalieni jinsi mayungiyungi* yanavyokua: Hayafanyi kazi wala hayasokoti; lakini ninawaambia hata Sulemani katika utukufu wake wote hakupambwa kama maua hayo.+ 28  Basi, ikiwa Mungu huivika hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo leo na kesho hutupwa ndani ya jiko, je, hatawavika vizuri zaidi ninyi wenye imani ndogo? 29  Basi acheni kutafuta kile mtakachokula au mtakachokunywa, na acheni kuhangaika kwa wasiwasi;+ 30  kwa maana mataifa yanatafuta vitu hivi vyote kwa bidii, lakini Baba yenu anajua mnahitaji vitu hivi.+ 31  Badala yake, endeleeni kuutafuta Ufalme wake, nanyi mtaongezewa vitu hivyo.+ 32  “Msiogope, ninyi kundi dogo,+ kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa Ufalme.+ 33  Uzeni mali zenu na kutoa zawadi za rehema.*+ Tengenezeni mikoba ya pesa isiyochakaa, hazina isiyopungua huko mbinguni,+ ambako mwizi hawezi kufika wala nondo* hali. 34  Kwa maana mahali ilipo hazina yenu, ndipo mioyo yenu itakapokuwa. 35  “Vaeni mavazi, muwe tayari*+ na mwashe taa zenu,+ 36  nanyi muwe kama watu wanaomsubiri bwana wao arudi+ kutoka kwenye karamu ya ndoa,+ ili atakapokuja na kupiga hodi wamfungulie mara moja. 37  Wenye furaha ni watumwa ambao bwana wao akija atawakuta wakikesha! Kwa kweli ninawaambia, atavaa vazi la mhudumu* na kuwaambia waketi mezani naye atakuja na kuwahudumia. 38  Akija katika kesha la pili,* au hata kesha la tatu,* na kuwakuta wakiwa tayari, watakuwa wenye furaha! 39  Lakini jueni jambo hili, ikiwa mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi angekuja, hangeruhusu nyumba yake ivunjwe.+ 40  Ninyi pia, endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia.”+ 41  Ndipo Petro akamuuliza: “Bwana, unatuambia sisi tu mfano huo au watu wote pia?” 42  Bwana akasema: “Kwa kweli ni nani msimamizi* mwaminifu, mwenye busara,* ambaye bwana wake atamweka asimamie watumishi* wake na kuendelea kuwapa kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa?+ 43  Mwenye furaha ni mtumwa huyo, ikiwa bwana wake atakapokuja atamkuta akifanya hivyo! 44  Kwa kweli ninawaambia, atamweka rasmi asimamie mali zake zote. 45  Lakini ikiwa mtumwa huyo atasema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia kuja,’ naye aanze kuwapiga watumishi wa kiume na wa kike na kula na kunywa na kulewa,+ 46  bwana wa mtumwa huyo atakuja siku asiyomtazamia na katika saa asiyoijua, naye atamwadhibu kwa ukali na kumweka pamoja na wasio waaminifu. 47  Mtumwa huyo aliyeelewa mapenzi ya bwana wake lakini hakujitayarisha wala kufanya alichoambiwa* atapigwa sana.+ 48  Lakini yule ambaye hakuelewa na hivyo akafanya mambo yanayostahili adhabu atapigwa kidogo. Kwa kweli, kila mtu ambaye alipewa mengi atadaiwa mengi, na yule aliyewekwa kusimamia mengi, atadaiwa mengi kuliko ilivyo kawaida.+ 49  “Nilikuja kuwasha moto duniani, na kama tayari umewaka, ninahitaji nini kingine? 50  Kwa kweli, kuna ubatizo ninaopaswa kubatizwa, na ninataabika sana mpaka umalizike!+ 51  Je, mnafikiri nilikuja kuleta amani duniani? Hapana, si amani bali mgawanyiko.+ 52  Kuanzia sasa kutakuwa na watu watano katika nyumba moja waliogawanyika, watatu dhidi ya wawili na wawili dhidi ya watatu. 53  Watagawanyika, baba dhidi ya mwana, mwana dhidi ya baba, mama dhidi ya binti, binti dhidi ya mama, mama mkwe dhidi ya binti mkwe, na binti mkwe dhidi ya mama mkwe.”+ 54  Kisha akauambia umati: “Mnapoona wingu likitokea magharibi, mara moja mnasema, ‘Kutakuwa na dhoruba,’ na inakuwa hivyo. 55  Nanyi mnapoona upepo wa kusini ukivuma, ninyi husema, ‘Kutakuwa na joto sana,’ na inakuwa hivyo. 56  Wanafiki, mnajua jinsi ya kuchunguza dunia na anga, lakini kwa nini hamjui jinsi ya kuchunguza kinachotendeka wakati huu?+ 57  Kwa nini hamtambui pia mambo yaliyo ya uadilifu? 58  Kwa mfano, unapoenda kwa mtawala pamoja na mtu anayekushtaki, anza kusuluhisha mambo pamoja naye mkiwa njiani, ili asikupeleke mbele ya hakimu, naye hakimu akukabidhi kwa ofisa wa mahakama, naye ofisa wa mahakama akutupe gerezani.+ 59  Ninakuambia, hakika hutatoka humo mpaka utakapolipa sarafu* yako ndogo ya mwisho.”

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Tnn., “kwa sarafu mbili za asarioni. ” Angalia Nyongeza B14.
Au “hampuuzi.”
Au “masinagogi.”
Au “tamaa.”
Au “nitaiambia nafsi yangu.”
Au “Nafsi, una”
Au “nafsi yako.”
Au “nafsi zenu.”
Au “nafsi ina.”
Aina ya maua.
Au “kuwapa maskini zawadi.” Angalia Kamusi.
Aina ya wadudu.
Tnn., “Jifungeni mishipi viunoni.”
Au “atajifunga kiunoni.”
Kuanzia saa 3 usiku mpaka saa 6 usiku.
Kuanzia saa 6 usiku mpaka saa 9 usiku.
Au “msimamizi wa nyumba.”
Au “mwenye hekima.”
Au “watumishi wa nyumbani.”
Au “kufanya mapenzi yake.”
Tnn., “leptoni ya mwisho.” Angalia Nyongeza B14.