Kulingana na Luka 13:1-35

  • Tubuni au muangamizwe (1-5)

  • Mfano wa mtini usiozaa (6-9)

  • Mwanamke mlemavu aponywa siku ya Sabato (10-17)

  • Mfano wa mbegu ya haradali na wa chachu (18-21)

  • Jitihada zinahitajika ili kupitia mlango mwembamba (22-30)

  • Herode, “mbweha huyo” (31-33)

  • Yesu aombolezea Yerusalemu (34, 35)

13  Wakati huo, watu fulani waliokuwa hapo walimwambia Yesu kuhusu Wagalilaya ambao Pilato alikuwa amechanganya damu yao na dhabihu zao.  Akawaambia: “Je, mnafikiri Wagalilaya hao walikuwa watenda dhambi wabaya zaidi kuliko Wagalilaya wengine wote kwa sababu walipatwa na mambo hayo?  Hapana. Ninawaambia msipotubu, nyote mtaangamizwa vivyo hivyo.+  Au wale 18 walioangukiwa na mnara huko Siloamu wakafa, je, mnafikiri walikuwa na hatia kuliko watu wengine wote wanaoishi Yerusalemu?  Hapana, ninawaambia; msipotubu, ninyi pia mtaangamizwa kama wao.”  Kisha akawaambia mfano huu: “Mtu fulani alikuwa na mtini uliopandwa katika shamba lake la mizabibu, akaenda kutafuta matunda kwenye mti huo lakini hakupata.+  Ndipo akamwambia mtunza-mizabibu, ‘Kwa miaka mitatu nimekuwa nikija kutafuta matunda kwenye mtini huu, lakini sijayapata. Ukate! Kwa nini uendelee kuharibu ardhi?’  Akamjibu, ‘Bwana, uache kwa mwaka mwingine mmoja niupalilie na kuutia mbolea.  Ukizaa matunda wakati ujao, vema; la sivyo, utaukata.’”+ 10  Sasa Yesu alikuwa akifundisha katika sinagogi siku ya Sabato. 11  Na tazama! hapo palikuwa na mwanamke aliyekuwa na roho ya udhaifu* kwa miaka 18, mwili wake ulikuwa umepindika na hangeweza kusimama wima. 12  Yesu alipomwona, akamwambia: “Mwanamke, umefunguliwa kutoka kwa udhaifu wako.”+ 13  Yesu akaweka mikono juu ya yule mwanamke na mara moja akanyooka na kuanza kumtukuza Mungu. 14  Lakini ofisa msimamizi wa sinagogi akakasirika kwa sababu Yesu aliponya siku ya Sabato, akauambia umati: “Kuna siku sita za kufanya kazi;+ basi, njooni mponywe katika siku hizo, bali si siku ya Sabato.”+ 15  Hata hivyo, Bwana akajibu: “Wanafiki,+ je, kila mmoja wenu hamfungui ng’ombe au punda wake kutoka kwenye kibanda siku ya Sabato na kumpeleka akanywe maji?+ 16  Je, haifai kwa mwanamke huyu, binti ya Abrahamu, ambaye Shetani alikuwa amemfunga kwa miaka 18 afunguliwe kutoka kwenye kifungo hicho siku ya Sabato?” 17  Aliposema mambo hayo, wapinzani wake wote wakaanza kuaibika, lakini umati wote ukaanza kushangilia ulipoona mambo yenye utukufu aliyofanya.+ 18  Basi akaendelea kusema: “Ufalme wa Mungu unafanana na nini, nitaulinganisha na nini? 19  Ni kama mbegu ya haradali ambayo mtu alichukua na kuipanda katika shamba lake, ikasitawi na kuwa mti, nao ndege wa angani wakajenga viota kwenye matawi yake.”+ 20  Akauliza tena: “Nitaulinganisha Ufalme wa Mungu na nini? 21  Ni kama chachu* ambayo mwanamke alichukua na kuichanganya na vipimo* vitatu vikubwa vya unga mpaka unga wote ukachacha.”*+ 22  Alipokuwa akisafiri kwenda Yerusalemu, Yesu alipita kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji akiwafundisha watu. 23  Sasa mtu fulani akamuuliza: “Bwana, je, wale watakaookolewa ni wachache?” Yesu akawaambia: 24  “Jitahidini sana ili mwingie kupitia mlango mwembamba,+ kwa sababu ninawaambia wengi watajaribu kuingia lakini hawataweza. 25  Mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, mtakuwa nje mkibisha mlangoni, mkisema, ‘Bwana, tufungulie.’+ Lakini atawajibu: ‘Sijui mnatoka wapi.’ 26  Kisha mtamjibu, ‘Tulikula na kunywa pamoja nawe, nawe ulifundisha katika barabara zetu kuu.’+ 27  Lakini atawaambia, ‘Sijui mnatoka wapi. Ondokeni kwangu, ninyi nyote watenda maovu!’ 28  Hapo ndipo mtalia na kusaga meno yenu mtakapoona Abrahamu, Isaka, Yakobo, na manabii wote katika Ufalme wa Mungu, lakini ninyi mkiwa mmetupwa nje.+ 29  Isitoshe, watu watakuja kutoka mashariki na magharibi, na kutoka kaskazini na kusini, nao wataketi mezani katika Ufalme wa Mungu. 30  Tazama! kuna wale wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na kuna wale wa kwanza watakaokuwa wa mwisho.”+ 31  Saa ileile baadhi ya Mafarisayo wakaja na kumwambia: “Ondoka hapa uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua.” 32  Akawaambia: “Nendeni mkamwambie mbweha huyo, ‘Tazama! Ninawafukuza roho waovu na kuwaponya watu leo na kesho, na siku ya tatu nitakuwa nimemaliza.’ 33  Hata hivyo, lazima niendelee leo, kesho, na keshokutwa, kwa sababu haiwezekani* nabii kuuawa nje ya Yerusalemu.+ 34  Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na aliyewapiga mawe wale waliotumwa kwake+—nilijaribu mara ngapi kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga wake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka.+ 35  Tazama! Mmeachiwa nyumba yenu.+ Ninawaambia, hamtaniona tena mpaka mtakaposema, ‘Amebarikiwa yule anayekuja katika jina la Yehova!’”*+

Maelezo ya Chini

Au “roho mwovu aliyemlemaza.”
Tnn., “vipimo vya sea.” Sea moja ilikuwa sawa na kilogramu 3.3 au lita 7.33. Angalia Nyongeza B14.
Au “ukaumuka.”
Au “hamira.”
Au “ni jambo lisilowaziwa.”