Kulingana na Luka 14:1-35

  • Mtu mwenye ugonjwa wa kuvimba aponywa siku ya Sabato (1-6)

  • Uwe mgeni mnyenyekevu (7-11)

  • Waalike watu wasio na uwezo wa kukulipa (12-14)

  • Mfano wa wageni waliotoa visingizio (15-24)

  • Gharama ya kuwa mwanafunzi (25-33)

  • Chumvi inapopoteza nguvu yake (34, 35)

14  Siku moja ya Sabato, Yesu alienda kula chakula katika nyumba ya kiongozi mmoja wa Mafarisayo, nao walikuwa wakimtazama sana.  Tazama! mbele yake kulikuwa na mtu mwenye ugonjwa wa kuvimba mwili.*  Basi Yesu akawauliza wale wenye ujuzi wa Sheria na Mafarisayo: “Je, ni halali au si halali kumponya mtu siku ya Sabato?”+  Lakini wakanyamaza. Basi akamshika mtu huyo, akamponya na kumwambia aende zake.  Kisha akawauliza: “Ni nani kati yenu ambaye mwana wake au ng’ombe wake akianguka ndani ya kisima+ siku ya Sabato, hatamtoa humo mara moja?”+  Wakashindwa kumjibu.  Kisha akawapa mfano watu walioalikwa, alipoona jinsi walivyokuwa wakichagua kuketi mahali pa heshima zaidi.+ Akawaambia:  “Mtu akikualika kwenye karamu ya ndoa, usiketi mahali pa heshima zaidi.+ Huenda pia amemwalika mtu mashuhuri kuliko wewe.  Naye aliyewaalika atakuja kukuambia, ‘Mwachie mtu huyu mahali ulipoketi.’ Kisha utaondoka kwa aibu na kuketi mahali pa chini kabisa. 10  Lakini unapoalikwa, nenda uketi mahali pa chini kabisa, ili mtu aliyekualika akija akuambie, ‘Rafiki yangu, nenda uketi mahali pa heshima zaidi.’ Kisha utakuwa na heshima mbele ya wageni wenzako wote.+ 11  Kwa maana kila mtu anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”+ 12  Kisha akamwambia yule mtu aliyemwalika: “Unapoandaa mlo wa mchana au wa jioni, usiwaite rafiki zako, ndugu zako, watu wako wa ukoo, au jirani zako walio matajiri. Huenda wao pia wakakualika, na hivyo kukulipa ulichowafanyia. 13  Lakini unapoandaa karamu, waalike maskini, viwete, vilema, na vipofu;+ 14  nawe utakuwa mwenye furaha, kwa sababu hawana kitu cha kukulipa. Kwa maana utalipwa katika ufufuo+ wa waadilifu.” 15  Aliposikia mambo hayo, mmoja wa wageni akamwambia: “Mwenye furaha ni yule anayekula* katika Ufalme wa Mungu.” 16  Yesu akamwambia: “Mtu fulani alikuwa akiandaa mlo mkubwa wa jioni,+ naye akawaalika watu wengi. 17  Saa ya mlo wa jioni ilipofika, akamtuma mtumwa wake awaambie walioalikwa, ‘Njooni, kwa sababu kila kitu kiko tayari.’ 18  Lakini wote wakaanza kutoa visingizio.+ Mmoja akasema, ‘Nilinunua shamba, ninahitaji kwenda kuliona; tafadhali, niwie radhi.’ 19  Mwingine akasema, ‘Nimenunua jozi tano za ng’ombe,* ninaenda kuwakagua; tafadhali, niwie radhi.’+ 20  Na bado mwingine akasema, ‘Nimetoka tu kuoa, kwa hiyo siwezi kuja.’ 21  Basi yule mtumwa akarudi na kumwambia bwana wake mambo hayo. Kisha yule bwana wa nyumba akakasirika na kumwambia mtumwa wake, ‘Nenda upesi kwenye barabara kuu na vichochoro vya jiji, uwalete maskini, viwete, vipofu, na vilema.’ 22  Baada ya muda yule mtumwa akasema, ‘Bwana, nimefanya ulivyoniagiza, lakini bado kuna nafasi.’ 23  Basi yule bwana akamwambia mtumwa, ‘Nenda barabarani na kwenye vijia uwahimize watu waje, ili nyumba yangu ijae.+ 24  Kwa maana ninawaambia, hakuna hata mmoja wa watu waliokuwa wamealikwa atakayeonja mlo wangu wa jioni.’”+ 25  Basi Yesu alikuwa akisafiri pamoja na umati mkubwa, kisha akageuka na kuwaambia: 26  “Yeyote akija kwangu naye hamchukii* baba yake na mama yake na mke wake na watoto wake na ndugu na dada zake, ndiyo, hata uhai wake*+ mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.+ 27  Yeyote asipouchukua mti wake wa mateso* na kunifuata hawezi kuwa mwanafunzi wangu.+ 28  Kwa mfano, ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha? 29  La sivyo, ataweka msingi lakini ashindwe kumaliza, na wote wanaomtazama wataanza kumdhihaki, 30  wakisema: ‘Mtu huyu alianza kujenga lakini akashindwa kumaliza.’ 31  Au mfalme akienda kupigana vita na mfalme mwingine, je, haketi kwanza na kufikiri iwapo akiwa na wanajeshi 10,000 anaweza kumshinda yule anayekuja akiwa na wanajeshi 20,000? 32  Ikiwa hawezi, basi yule mfalme mwingine akiwa bado yuko mbali sana, yeye huwatuma mabalozi ili kufanya amani. 33  Vivyo hivyo, kwa hakika yeyote kati yenu asipoaga* mali zake zote hawezi kuwa mwanafunzi wangu.+ 34  “Kwa kweli chumvi ni nzuri. Lakini ikipoteza nguvu yake, itakolezwa na nini?+ 35  Haifai kuchanganywa na udongo wala mbolea. Watu huitupa nje. Yule aliye na masikio ya kusikiliza na asikilize.”+

Maelezo ya Chini

Uvimbe unaosababishwa na umajimaji kuongezeka mwilini.
Tnn., “anayekula mkate.”
Au “ng’ombe kumi.”
Au “hampendi kwa kiwango kidogo zaidi.”
Au “nafsi yake.”
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Au “asipoacha.”