Kulingana na Luka 16:1-31

  • Mfano wa msimamizi asiye mwadilifu (1-13)

    • ‘Mtu mwaminifu katika dogo ni mwaminifu katika kubwa’ (10)

  • Sheria na Ufalme wa Mungu (14-18)

  • Mfano wa tajiri na Lazaro (19-31)

16  Pia, Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Tajiri fulani alikuwa na msimamizi* ambaye alishtakiwa kwamba anatumia vibaya mali yake.  Basi akamwita na kumwambia, ‘Ni mambo gani haya ninayosikia kukuhusu? Lete rekodi za usimamizi kwa sababu huwezi tena kusimamia nyumba yangu.’  Kisha yule msimamizi akajiambia, ‘Nitafanya nini kwa kuwa bwana wangu ananiondoa kazini? Sina nguvu za kulima na ninaona aibu kuombaomba.  Aha! Najua nitakachofanya, ili nitakapoachishwa kazi, watu wanikaribishe nyumbani mwao.’  Akawaita mmoja mmoja wale waliokuwa na madeni ya bwana wake, akamuuliza wa kwanza, ‘Unadaiwa kiasi gani na bwana wangu?’  Akajibu, ‘Vipimo* 100 vya mafuta ya zeituni.’ Akamwambia, ‘Chukua hati yako ya mapatano, uketi na upesi uandike 50.’  Kisha akamuuliza mwingine, ‘Na wewe, unadaiwa kiasi gani?’ Akasema, ‘Vipimo vikubwa 100* vya ngano.’ Akamwambia, ‘Chukua hati yako ya mapatano uandike 80.’  Bwana wake akamsifu yule msimamizi kwa sababu ingawa hakuwa mwadilifu, alitenda kwa hekima inayotumika;* kwa maana wana wa mfumo huu wa mambo* wana hekima zaidi katika kizazi chao kuliko walivyo wana wa nuru.+  “Pia, ninawaambia: Jifanyieni marafiki kupitia mali zisizo za uadilifu,+ ili zitakapokwisha wawapokee katika makao ya milele.+ 10  Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo si mwaminifu katika lililo kubwa pia. 11  Kwa hiyo, msipokuwa waaminifu kuhusu mali zisizo za uadilifu, ni nani atakayewakabidhi kilicho cha kweli? 12  Na msipokuwa waaminifu kuhusu mali ya mtu mwingine, ni nani atakayewapa mali yenu wenyewe?+ 13  Hakuna mtumishi anayeweza kuwatumikia mabwana wawili, kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kuwa watumwa wa Mungu na wa Utajiri.”+ 14  Sasa Mafarisayo, waliopenda pesa, walikuwa wakisikiliza mambo hayo yote, nao wakaanza kumdhihaki.+ 15  Basi akawaambia: “Mnajitangaza kuwa waadilifu mbele ya wanadamu,+ lakini Mungu anaijua mioyo yenu.+ Kwa maana kitu kinachoheshimiwa sana na wanadamu kinamchukiza Mungu.+ 16  “Sheria na Manabii walikuwa mpaka Yohana. Tangu wakati huo habari njema za Ufalme wa Mungu zinatangazwa, na watu wa namna zote wanajitahidi kuufikia.+ 17  Kwa kweli, ni rahisi zaidi kwa mbingu na dunia kupitilia mbali kuliko sehemu yoyote ya herufi ya Sheria kukosa kutimia.+ 18  “Kila mtu anayempa talaka mke wake na kuoa mwingine anafanya uzinzi, na yeyote anayemwoa mwanamke aliyepewa talaka na mumewe anafanya uzinzi.+ 19  “Kulikuwa na tajiri ambaye alikuwa akivaa mavazi ya zambarau na kitani, na alifurahia maisha ya kifahari siku kwa siku. 20  Lakini mtu fulani aliyekuwa akiombaomba aliyeitwa Lazaro, alikuwa akiletwa kwenye lango lake. Alikuwa na vidonda mwili mzima, 21  naye alikuwa akitamani kula mabaki yaliyoanguka kutoka kwenye meza ya yule tajiri. Ndiyo, pia, mbwa walikuwa wakija na kuramba vidonda vyake. 22  Baada ya muda yule mtu aliyekuwa akiombaomba akafa, malaika wakambeba na kumpeleka kando ya Abrahamu.* “Pia, yule tajiri akafa na kuzikwa. 23  Akiwa Kaburini* akatazama juu, akiteseka sana, akamwona Abrahamu kwa mbali na Lazaro akiwa kando yake.* 24  Kwa hiyo akamwita, ‘Baba Abrahamu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake katika maji aupoze ulimi wangu, kwa maana ninateseka sana katika moto huu mkali.’ 25  Lakini Abrahamu akamwambia, ‘Mwanangu, kumbuka wewe ulikuwa na vitu vingi vizuri maishani, naye Lazaro aliteseka sana. Hata hivyo, sasa anafarijika lakini wewe unateseka. 26  Isitoshe, kuna shimo kubwa kati yetu nanyi, hivi kwamba wale wanaotaka kuvuka kutoka hapa kuja kwenu hawawezi, wala watu hawawezi kuvuka kutoka huko na kuja kwetu.’ 27  Kisha akasema, ‘Basi kama ni hivyo ninakuomba, baba, umtume kwenye nyumba ya baba yangu, 28  ili awatolee ushahidi kamili ndugu zangu watano wasije wakaingia mahali hapa pa mateso.’ 29  Lakini Abrahamu akasema, ‘Wana Musa na Manabii; waache wawasikilize hao.’+ 30  Kisha akasema, ‘Hapana, Baba Abrahamu, hawatasikiliza, lakini mtu fulani kutoka kwa wafu akienda kwao, watatubu.’ 31  Lakini akamwambia, ‘Kama hawamsikilizi Musa+ na Manabii, hawataamini hata mtu fulani akifufuliwa kutoka kwa wafu.’”

Maelezo ya Chini

Au “msimamizi wa nyumba.”
Au “vipimo vya bathi.” Bathi moja ilikuwa sawa na lita 22. Angalia Nyongeza B14.
Au “vipimo 100 vya kori.” Kori moja ilikuwa sawa na kilogramu 170. Angalia Nyongeza B14.
Au “kwa busara; kwa werevu.”
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Tnn., “kwenye kifua cha Abrahamu.”
Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.
Tnn., “kwenye kifua chake.”