Kulingana na Luka 17:1-37

  • Kukwazika, msamaha, na imani (1-6)

  • Watumwa wasiofaa kitu (7-10)

  • Watu kumi wenye ukoma waponywa (11-19)

  • Kuja kwa Ufalme wa Mungu (20-37)

    • “Ufalme wa Mungu uko katikati yenu.” (21)

    • “Mkumbukeni mke wa Loti” (32)

17  Ndipo akawaambia wanafunzi wake: “Lazima vikwazo vije. Hata hivyo, ole wake mtu atakayevisababisha!  Ingekuwa afadhali kwake kama angefungiwa shingoni jiwe la kusagia kisha atupwe baharini kuliko amkwaze mmoja wa hawa wadogo.+  Jiangalieni ninyi wenyewe. Ndugu yako akitenda dhambi mkemee,+ na akitubu, msamehe.+  Hata akikutendea dhambi mara saba kwa siku, naye anarudi kwako mara saba akisema, ‘ninatubu,’ unapaswa kumsamehe.”+  Mitume wakamwambia Bwana: “Tusaidie tuwe na imani zaidi.”+  Bwana akasema: “Kama mngekuwa na imani inayolingana na mbegu ya haradali, mngeuambia mti huu wa mforsadi, ‘Ng’oka ukapandwe baharini!’ nao ungewatii.+  “Ni nani kati yenu aliye na mtumwa anayelima shamba au kuchunga wanyama, ambaye akirudi kutoka shambani, atamwambia ‘Njoo upesi, keti ule chakula’?  Hapana. Badala yake atamwambia, ‘Nitayarishie chakula cha jioni, na ujifunge vazi la kazi ili unihudumie mpaka nitakapomaliza kula na kunywa, kisha unaweza kula na kunywa.’  Je, utamshukuru mtumwa huyo kwa sababu alifanya mambo uliyomwagiza? 10  Vivyo hivyo, baada ya kufanya mambo mliyoagizwa, semeni: ‘Sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Tumefanya kile tulichopaswa kufanya.’”+ 11  Alipokuwa akienda Yerusalemu, alipita kati ya Samaria na Galilaya. 12  Alipokuwa akiingia katika kijiji fulani alikutana na wanaume kumi wenye ukoma, lakini walisimama mbali naye.+ 13  Kisha wakasema kwa sauti kubwa: “Yesu, Mwalimu, tuhurumie!”* 14  Alipowaona, akawaambia: “Nendeni mkajionyeshe kwa makuhani.”+ Basi walipokuwa wakienda wakatakaswa.+ 15  Mmoja wao alipoona amepona, akarudi akimtukuza Mungu kwa sauti kubwa. 16  Akaanguka kifudifudi miguuni pa Yesu na kumshukuru. Isitoshe, alikuwa Msamaria.+ 17  Yesu akauliza: “Wote kumi walitakaswa, sivyo? Basi, wako wapi wale wengine tisa? 18  Je, hakuna mwingine aliyerudi ili kumtukuza Mungu isipokuwa mtu huyu wa taifa lingine?” 19  Kisha akamwambia: “Simama uende; imani yako imekuponya.”+ 20  Mafarisayo walipomuuliza Ufalme wa Mungu utakuja lini,+ aliwajibu: “Ufalme wa Mungu hautakuja ukionekana waziwazi; 21  wala watu hawatasema, ‘Tazama! uko hapa!’ au, ‘Uko pale!’ Kwa maana tazama! Ufalme wa Mungu uko katikati yenu.”*+ 22  Kisha akawaambia wanafunzi: “Siku zitafika ambapo mtatamani kuona moja kati ya siku za Mwana wa binadamu lakini hamtaiona. 23  Na watu watawaambia, ‘Angalia pale!’ au, ‘Angalia hapa!’ Msiende wala msiwafuate.+ 24  Kwa maana kama radi inavyong’aa kutoka sehemu moja ya mbingu mpaka sehemu nyingine, ndivyo Mwana wa binadamu+ atakavyokuwa katika siku yake.+ 25  Hata hivyo, kwanza lazima apatwe na mateso mengi na kukataliwa na kizazi hiki.+ 26  Isitoshe, kama ilivyokuwa katika siku za Noa,+ ndivyo itakavyokuwa katika siku za Mwana wa binadamu:+ 27  walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, wanaume walikuwa wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina,+ na Gharika ikaja na kuwaangamiza wote.+ 28  Vivyo hivyo, kama ilivyokuwa katika siku za Loti:+ walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, walikuwa wakinunua, walikuwa wakiuza, walikuwa wakipanda, na walikuwa wakijenga. 29  Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma, kulinyesha mvua ya moto na kiberiti kutoka mbinguni na wote wakaangamizwa.+ 30  Ndivyo itakavyokuwa siku ambayo Mwana wa binadamu atafunuliwa.+ 31  “Siku hiyo mtu aliye kwenye paa la nyumba asishuke kuchukua mali iliyo ndani ya nyumba yake, vivyo hivyo mtu aliye shambani, asirudi kwenye vitu vilivyo nyuma. 32  Mkumbukeni mke wa Loti.+ 33  Yeyote anayetaka kuuokoa uhai wake* ataupoteza, lakini yeyote anayeupoteza atauokoa.+ 34  Ninawaambia, usiku huo watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja atachukuliwa, lakini mwingine ataachwa.+ 35  Wanawake wawili watakuwa wakisaga kwenye jiwe moja la kusagia; mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.” 36 * —— 37  Basi wakamuuliza: “Wapi, Bwana?” Akawajibu: “Mahali palipo na mzoga, hapo ndipo tai watakapokusanyika.”+

Maelezo ya Chini

Au “tuonyeshe rehema!”
Au “uko miongoni mwenu.”
Au “nafsi yake.”