Kulingana na Luka 24:1-53

  • Yesu afufuliwa (1-12)

  • Wakiwa njiani kuelekea Emau (13-35)

  • Yesu awatokea wanafunzi (36-49)

  • Yesu apaa mbinguni (50-53)

24  Hata hivyo, siku ya kwanza ya juma asubuhi na mapema, walienda kwenye kaburi,* wakiwa na manukato waliyotayarisha.+  Lakini wakakuta jiwe limeviringishwa kutoka kwenye kaburi,*+  nao walipoingia, hawakuupata mwili wa Bwana Yesu.+  Wakiwa wameshangazwa na jambo hilo, tazama! wanaume wawili waliovaa mavazi yanayong’aa wakasimama kando yao.  Wanawake hao wakaogopa sana wakainamisha nyuso zao, basi wale wanaume wakawaambia: “Kwa nini mnamtafuta yule aliye hai kati ya wafu?+  Hayupo hapa, amefufuliwa. Kumbukeni jinsi alivyowaambia alipokuwa Galilaya,  kwamba Mwana wa binadamu lazima atiwe mikononi mwa wenye dhambi na kuuawa kwenye mti na siku ya tatu afufuliwe.”+  Ndipo wakakumbuka maneno yake,+  wakarudi kutoka kaburini,* wakawaambia mambo hayo yote wale 11 na wengine wote.+ 10  Walikuwa Maria Magdalene, Yoana, na Maria mama ya Yakobo. Pia, wanawake wengine waliokuwa pamoja nao waliwaambia mitume mambo hayo. 11  Hata hivyo, waliyaona maneno hayo kama upuuzi, nao hawakuwaamini wanawake hao. 12  Lakini Petro akatoka, akakimbia hadi kwenye kaburi,* na alipoinama mbele, akaona vile vitambaa vya kitani peke yake. Kwa hiyo akaondoka akiwa ameshangazwa na mambo yaliyotokea. 13  Lakini tazama! siku hiyohiyo wanafunzi wawili walikuwa wakisafiri kwenda kijiji kinachoitwa Emau, kilicho karibu kilomita 11* kutoka Yerusalemu, 14  nao walikuwa wakizungumza kuhusu mambo hayo yote yaliyotukia. 15  Sasa walipokuwa wakiongea na kujadiliana kuhusu mambo hayo, Yesu akakaribia na kuanza kutembea pamoja nao, 16  lakini macho yao yalizuiwa wasiweze kumtambua.+ 17  Akawauliza: “Ni mambo gani haya mnayojadiliana huku mkitembea?” Nao wakasimama tuli, wakiwa na huzuni. 18  Yule aliyeitwa Kleopa akamjibu: “Je, wewe ni mgeni anayekaa peke yake Yerusalemu hivi kwamba hujui* mambo ambayo yametukia huko siku hizi?” 19  Akawauliza: “Mambo gani?” Wakamjibu: “Kuhusu Yesu Mnazareti,+ yule nabii aliyefanya miujiza na kusema maneno yenye nguvu mbele za Mungu na watu wote;+ 20  na jinsi wakuu wa makuhani wetu na watawala walivyomtoa ili ahukumiwe kifo,+ kisha wakamtundika kwenye mti. 21  Tulitazamia kwamba yeye ndiye angekomboa Israeli.+ Ndiyo, isitoshe hii ni siku ya tatu tangu mambo hayo yatokee. 22  Pia, wanawake fulani miongoni mwetu walitushangaza, kwa sababu walienda mapema kwenye kaburi*+ 23  na walipokosa kuuona mwili wake, wakarudi wakisema pia waliona maono yasiyo ya kawaida ya malaika waliowaambia kwamba Yesu yuko hai. 24  Kisha baadhi ya wenzetu wakaenda kwenye kaburi,*+ wakalikuta kama vile wale wanawake walivyosema, lakini hawakumwona.” 25  Basi akawaambia: “Enyi wasio na akili na wagumu kuamini mambo yote yaliyosemwa na manabii! 26  Je, haikuwa lazima Kristo kupatwa na mateso haya+ kisha aingie kwenye utukufu wake?”+ 27  Naye akawafafanulia kuanzia Musa na Manabii wote,+ mambo yote ambayo Maandiko yalisema kumhusu. 28  Mwishowe walipokaribia kijiji walichokuwa wakienda, Yesu akajifanya kana kwamba anaendelea na safari. 29  Lakini wakamsihi asiende, wakisema: “Kaa pamoja nasi, kwa sababu ni jioni, na siku inakaribia kwisha.” Basi akaingia ili akae pamoja nao. 30  Naye alipokuwa akila* pamoja nao akauchukua mkate, akaubariki, akaumega na kuanza kuwapa.+ 31  Ndipo macho yao yakafunguliwa kikamili nao wakamtambua; lakini akatoweka.+ 32  Wakaambiana: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akizungumza nasi barabarani, na alipokuwa akitufungulia* Maandiko waziwazi?” 33  Saa hiyohiyo wakaondoka na kurudi Yerusalemu, wakawakuta wale 11 na watu waliokusanyika pamoja nao, 34  wakasema: “Kwa kweli Bwana alifufuliwa naye alimtokea Simoni!”+ 35  Kisha wakasimulia mambo yaliyotokea barabarani na jinsi walivyomtambua alipoumega mkate.+ 36  Walipokuwa wakisema mambo hayo Yesu akasimama katikati yao na kuwaambia: “Na muwe na amani.”+ 37  Lakini kwa sababu walikuwa wameshtuka na kuogopa, walidhani kwamba wanaona roho. 38  Basi akawauliza: “Kwa nini mnahangaika, na kwa nini mna shaka mioyoni mwenu? 39  Angalieni mikono na miguu yangu, kwamba ni mimi; niguseni mwone, kwa maana roho haina nyama na mifupa kama vile mnavyoona nilivyo.” 40  Alipokuwa akisema hayo, akawaonyesha mikono yake na miguu yake. 41  Wakiwa bado hawaamini kwa sababu ya shangwe nyingi na mshangao, akawauliza: “Mna chakula chochote hapa?” 42  Basi wakampa kipande cha samaki wa kuchomwa, 43  akakichukua, akala wakimtazama. 44  Kisha akawaambia: “Haya ndiyo maneno niliyowaambia nilipokuwa bado pamoja nanyi,+ kwamba mambo yote yaliyoandikwa kunihusu katika Sheria ya Musa, Manabii, na Zaburi lazima yatimizwe.”+ 45  Ndipo akafungua akili zao ili waelewe kabisa maana ya Maandiko,+ 46  naye akawaambia: “Imeandikwa kwamba Kristo atateseka na kufufuliwa kutoka kwa wafu siku ya tatu,+ 47  na kwa msingi wa jina lake, toba kwa msamaha wa dhambi+ ingehubiriwa katika mataifa yote+—kuanzia Yerusalemu.+ 48  Ninyi mtakuwa mashahidi wa mambo haya.+ 49  Na tazama! Nitawatumia kile ambacho Baba yangu ameahidi. Hata hivyo, kaeni jijini mpaka mtakapovikwa nguvu kutoka juu.”+ 50  Kisha akawaongoza mpaka Bethania, naye akainua mikono yake na kuwabariki. 51  Alipokuwa akiwabariki akatenganishwa nao, akaanza kuchukuliwa juu mbinguni.+ 52  Wakamsujudia* na kurudi Yerusalemu wakiwa na shangwe kubwa.+ 53  Nao walikuwa hekaluni kila siku wakimsifu Mungu.+

Maelezo ya Chini

Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kwenye kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Tnn., “stadia 60.” Stadia moja ilikuwa sawa na mita 185 (futi 606.95). Angalia Nyongeza B14.
Au labda, “Je, wewe ni mgeni pekee katika Yerusalemu ambaye hajui?”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “alipokuwa ameketi mezani.”
Au “akitufafanulia.”
Au “Wakamwinamia.”