Kulingana na Luka 5:1-39

  • Wavua samaki kimuujiza; wanafunzi wa kwanza (1-11)

  • Mtu mwenye ukoma aponywa (12-16)

  • Yesu amponya mtu aliyepooza (17-26)

  • Yesu amwita Lawi (27-32)

  • Swali kuhusu kufunga (33-39)

5  Pindi moja, Yesu alikuwa amesimama kando ya ziwa la Genesareti*+ na umati ulikuwa umemsonga ili kusikiliza neno la Mungu.  Akaona mashua mbili zikiwa zimeegeshwa kando ya ziwa, lakini wavuvi walikuwa wametoka na walikuwa wakiosha nyavu zao.+  Akaingia katika mashua moja iliyokuwa ya Simoni, akamwomba aivute mbali kidogo na nchi kavu. Kisha akaketi na kuanza kuwafundisha watu akiwa kwenye mashua.  Alipoacha kuzungumza, akamwambia Simoni: “Peleka mashua mahali penye kina, kisha mshushe nyavu zenu, mvue samaki.”  Simoni akamjibu: “Mwalimu, tumejitahidi kuvua samaki usiku wote na hatukupata chochote,+ lakini nitazishusha nyavu kama ulivyoniagiza.”  Basi walipofanya hivyo, wakavua* samaki wengi sana hivi kwamba nyavu zao zikaanza kukatika.+  Wakawaita wenzao waliokuwa katika ile mashua nyingine waje kuwasaidia, wakaja na kujaza mashua zote mbili, nazo zikaanza kuzama.  Simoni Petro alipoona hivyo, akaanguka magotini pa Yesu na kusema: “Bwana ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi.”  Kwa maana yeye na wenzake walishangazwa sana na samaki wengi waliovua. 10  Pia, Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo,+ ambao walishirikiana na Simoni wakashangaa. Lakini Yesu akamwambia Simoni: “Acha kuogopa. Kuanzia sasa utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.”+ 11  Basi wakazirudisha mashua kwenye nchi kavu, wakaacha kila kitu na kumfuata.+ 12  Pindi nyingine alipokuwa katika jiji fulani, tazama! kulikuwa na mwanamume aliyejaa ukoma! Alipomwona Yesu, akajiangusha kifudifudi na kumwomba: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.”+ 13  Basi Yesu akanyoosha mkono wake akamgusa na kusema: “Ninataka! Takasika.” Mara moja ule ukoma ukaisha.+ 14  Kisha akamwagiza mtu huyo asimwambie mtu yeyote: “Bali nenda ukajionyeshe kwa kuhani, kisha utoe toleo la kutakaswa kwako, kama alivyoagiza Musa,+ ili kuwa ushahidi kwao.”+ 15  Lakini habari kumhusu zikazidi kuenea, na umati mkubwa ulikuwa ukikusanyika ili kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao.+ 16  Hata hivyo, mara kwa mara alienda mahali pasipo na watu ili kusali. 17  Siku moja alipokuwa akifundisha, Mafarisayo na walimu wa sheria kutoka kila kijiji cha Galilaya na Yudea na kutoka Yerusalemu walikuwa wameketi hapo; na Yehova* alikuwa amempa nguvu za kuponya.+ 18  Na tazama! kulikuwa na wanaume waliombeba kwenye kitanda* mtu aliyepooza, nao wakajaribu kumwingiza ndani na kumweka mbele ya Yesu.+ 19  Waliposhindwa kumwingiza kwa sababu ya umati, wakapanda kwenye paa, wakaondoa vigae na kumshusha akiwa kwenye kitanda kati ya wale waliokuwa mbele ya Yesu. 20  Alipoona imani yao, akamwambia yule mtu: “Ewe mtu, umesamehewa dhambi zako.”+ 21  Ndipo waandishi na Mafarisayo wakaanza kujadiliana: “Huyu ni nani anayesema makufuru? Ni nani anayeweza kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”+ 22  Lakini Yesu, akifahamu mawazo yao akawauliza: “Mnawaza nini katika mioyo yenu? 23  Ni jambo gani rahisi zaidi kusema, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama utembee’? 24  Lakini ili mjue kwamba Mwana wa binadamu ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani—” akamwambia yule mtu aliyepooza: “Ninakuambia, Simama, uchukue kitanda chako, uende nyumbani.”+ 25  Ndipo akasimama mbele yao, akachukua kitanda chake, akaenda nyumbani, akimtukuza Mungu. 26  Kisha wote wakashangaa wakaanza kumtukuza Mungu, wakastaajabu na kusema: “Leo tumeona mambo ya ajabu!” 27  Baada ya mambo hayo akaenda nje na kumwona mkusanya kodi anayeitwa Lawi akiwa ameketi kwenye ofisi ya kodi, akamwambia: “Njoo uwe mfuasi wangu.”+ 28  Naye akasimama, akaacha kila kitu na kuanza kumfuata. 29  Kisha Lawi akamwandalia Yesu karamu kubwa nyumbani kwake, na kulikuwa na umati mkubwa wa wakusanya kodi na wengine waliokuwa wakila* pamoja nao.+ 30  Ndipo Mafarisayo na waandishi wao wakaanza kuwalalamikia wanafunzi wake, wakisema: “Kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi?”+ 31  Yesu akawajibu: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.+ 32  Sikuja kuwaita waadilifu, bali kuwahimiza watenda dhambi watubu.”+ 33  Wakamwambia: “Wanafunzi wa Yohana hufunga mara nyingi na kutoa dua, na pia wanafunzi wa Mafarisayo, lakini wanafunzi wako hula na kunywa.”+ 34  Yesu akawaambia: “Hamwezi kuwafanya rafiki za bwana harusi wafunge bwana harusi akiwa pamoja nao, sivyo? 35  Lakini siku zitakuja ambapo kwa kweli bwana harusi+ ataondolewa kwao; ndipo watakapofunga siku hizo.”+ 36  Pia, akawapa mfano: “Hakuna mtu anayekata kiraka cha vazi jipya la nje na kukishona kwenye vazi la zamani. Akifanya hivyo, kiraka kipya hurarua vazi la zamani na kiraka kipya hakilingani na vazi la zamani.+ 37  Pia, hakuna mtu anayeweka divai mpya katika viriba vya divai vilivyochakaa. Akifanya hivyo, divai mpya itavipasua viriba, nayo itamwagika na viriba vitaharibika. 38  Lakini divai mpya lazima iwekwe katika viriba vipya vya divai. 39  Mtu anapokunywa divai ya zamani hapendi divai mpya, kwa maana husema, ‘Ile ya zamani ndiyo nzuri.’”

Maelezo ya Chini

Yaani, Bahari ya Galilaya.
Tnn., “wakazingira.”
Au “machela.”
Au “walikuwa wameketi mezani.”