Mambo ya Walawi 1:1-17

  • Dhabihu ya kuteketezwa (1-17)

1  Na Yehova akamwita Musa na kuzungumza naye katika hema la mkutano,+ akamwambia:  “Zungumza na Waisraeli* uwaambie, ‘Ikiwa yeyote kati yenu atamtolea Yehova mnyama wa kufugwa, anapaswa kumtolea dhabihu kutoka kati ya mifugo yake au kundi lake.+  “‘Ikiwa anatoa dhabihu ya kuteketezwa kutoka kati ya mifugo yake, anapaswa kutoa mnyama dume asiye na kasoro.+ Atamtoa kwa hiari yake mwenyewe+ mbele za Yehova kwenye mlango wa hema la mkutano.  Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha dhabihu hiyo ya kuteketezwa, nayo itakubaliwa kwa niaba yake ili kufunika dhambi zake.  “‘Kisha huyo ng’ombe dume mchanga atachinjwa mbele za Yehova, nao wana wa Haruni, makuhani,+ wataleta damu ya mnyama huyo na kuinyunyiza pande zote za madhabahu,+ kwenye mlango wa hema la mkutano.  Mnyama huyo wa dhabihu ya kuteketezwa anapaswa kuchunwa ngozi na kukatwa vipandevipande.+  Wana wa Haruni, makuhani, wataweka moto kwenye madhabahu+ na kupanga kuni kwenye moto huo.  Wana wa Haruni, makuhani, watapanga vile vipande vya mnyama wa dhabihu+ pamoja na kichwa na mafuta yanayofunika figo juu ya kuni kwenye moto wa madhabahu.  Matumbo na miguu yake itaoshwa kwa maji, na kuhani atachoma moto vitu hivyo vyote ili vifuke moshi kwenye madhabahu. Ni dhabihu ya kuteketezwa, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.+ 10  “‘Ikiwa anatoa dhabihu kutoka katika kundi,+ yaani, kutoka kati ya wanakondoo dume au mbuzi, anapaswa kutoa dume asiye na kasoro.+ 11  Atachinjiwa upande wa kaskazini wa madhabahu mbele za Yehova, nao wana wa Haruni, makuhani, watanyunyiza damu yake pande zote za madhabahu.+ 12  Atamkata vipandevipande, naye kuhani atavipanga vipande hivyo pamoja na kichwa na mafuta yaliyo kwenye figo juu ya kuni kwenye moto wa madhabahu. 13  Ataosha matumbo na miguu yake kwa maji, kisha kuhani atavileta vyote na kuvichoma moto ili vifuke moshi kwenye madhabahu. Ni dhabihu ya kuteketezwa, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova. 14  “‘Hata hivyo, ikiwa anamtoa ndege kuwa dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova, atamtoa njiwa tetere au hua mchanga.+ 15  Kuhani atamtoa kwenye madhabahu, atamvunja shingo na kuacha kichwa kikining’inia, kisha atamchoma moto juu ya madhabahu ili afuke moshi, lakini damu yake itamwagwa kando ya madhabahu. 16  Ataondoa kifuko cha chakula kilicho kooni mwake pamoja na manyoya yake na kuvitupa vitu hivyo kando ya madhabahu, upande wa mashariki, mahali panapowekwa majivu.*+ 17  Atampasua kwenye mabawa yake bila kumkata vipande viwili. Kisha kuhani atamchoma moto juu ya kuni zilizo kwenye madhabahu ili afuke moshi. Ni dhabihu ya kuteketezwa, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.

Maelezo ya Chini

Tnn., “wana wa Israeli.”
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.
Au “inayomtuliza.”