Mambo ya Walawi 10:1-20

  • Moto kutoka kwa Yehova wawaangamiza Nadabu

    na Abihu (1-7)

  • Sheria ya makuhani kuhusu kula na kunywa (8-20)

10  Baadaye Nadabu na Abihu,+ wana wa Haruni, walichukua kila mmoja wao chetezo chake, wakaweka moto ndani yake na kutia uvumba.+ Wakaanza kumtolea Yehova moto haramu,+ jambo ambalo hakuwaamuru wafanye.  Ndipo moto ukashuka kutoka kwa Yehova, ukawateketeza,+ wakafa mbele za Yehova.+  Musa akamwambia Haruni: “Yehova amesema hivi: ‘Nitatakaswa miongoni mwa wale walio karibu nami,+ nami nitatukuzwa mbele ya watu wote.’” Haruni akanyamaza kimya.  Basi Musa akamwita Mishaeli na Elsafani, wana wa Uzieli,+ ndugu ya baba ya Haruni, akawaambia: “Njooni hapa, waondoeni ndugu zenu mbele ya mahali patakatifu muwapeleke nje ya kambi.”  Kwa hiyo wakaja, wakawabeba wakiwa na kanzu zao na kuwapeleka nje ya kambi, kama Musa alivyowaambia.  Kisha Musa akamwambia Haruni na wanawe waliobaki, Eleazari na Ithamari: “Msikose kutunza nywele zenu na msirarue mavazi yenu,+ msije mkafa na kumfanya Mungu awakasirikie Waisraeli wote. Ndugu zenu wote wa nyumba ya Israeli watawaombolezea wale ambao Yehova amewaangamiza kwa moto.  Msitoke nje ya mlango wa hema la mkutano msije mkafa, kwa sababu Yehova amewatia mafuta.”+ Basi wakafanya kama Musa alivyosema.  Kisha Yehova akamwambia Haruni:  “Wewe na wanao msinywe divai au kileo chochote mnapoingia katika hema la mkutano,+ msije mkafa. Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu. 10  Ili muweze kutofautisha mambo matakatifu na mambo yaliyo najisi, mambo safi na mambo yasiyo safi,+ 11  na ili muwafundishe Waisraeli wote sheria zote ambazo* Yehova amewaambia kupitia Musa.”+ 12  Kisha Musa akamwambia Haruni na wanawe waliobaki, Eleazari na Ithamari: “Chukueni toleo la nafaka lililobaki kutoka katika dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto, mle toleo hilo karibu na madhabahu kama mkate usio na chachu,+ kwa sababu ni toleo takatifu kabisa.+ 13  Mtakula toleo hilo mahali patakatifu,+ kwa sababu ni posho yenu na posho ya wana wenu kutoka kwenye dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto, kwa maana hivyo ndivyo nilivyoamriwa. 14  Pia, wewe na wanao na binti zako+ mtakula kidari cha toleo la kutikiswa na mguu wa fungu takatifu+ mkiwa mahali safi kwa sababu vitu hivyo vimetolewa ili kuwa posho yako na posho ya wanao kutoka kwenye dhabihu za ushirika za Waisraeli. 15  Watauleta mguu wa fungu takatifu na kidari cha toleo la kutikiswa pamoja na dhabihu za mafuta zinazochomwa kwa moto, ili vitikiswe mbele za Yehova vikiwa toleo la kutikiswa kwenda mbele na nyuma; hilo litakuwa posho yako na posho ya kudumu ya wanao,+ kama Yehova alivyoamuru.” 16  Musa akamtafuta sana mbuzi wa dhabihu ya dhambi,+ lakini akagundua kwamba alikuwa ameteketezwa. Kwa hiyo akawakasirikia sana Eleazari na Ithamari, wana waliobaki wa Haruni, akawauliza: 17  “Kwa nini hamkula dhabihu ya dhambi mkiwa mahali patakatifu,+ wakati ni dhabihu takatifu kabisa ambayo amewapa ili mbebe dhambi za Waisraeli wote na kuwatolea dhabihu ya kufunika dhambi zao mbele za Yehova? 18  Sasa angalieni! Damu yake haijaletwa mahali patakatifu.+ Mlipaswa kula dhabihu hiyo mahali patakatifu, kama nilivyoamriwa.” 19  Haruni akamjibu Musa: “Tazama! Leo walimtolea Yehova dhabihu yao ya dhambi na dhabihu yao ya kuteketezwa,+ na bado mambo haya yamenipata. Kama ningekula dhabihu ya dhambi leo, je, jambo hilo lingempendeza Yehova?” 20  Musa aliposikia hayo, akaridhika.

Maelezo ya Chini

Au “masharti yote ambayo.”