Mambo ya Walawi 14:1-57

  • Kujitakasa ukoma (1-32)

  • Kutakasa nyumba zilizoathiriwa (33-57)

14  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Hii ndiyo sheria inayomhusu mtu mwenye ukoma ambayo inapaswa kufuatwa siku ambayo utakaso wake unathibitishwa, anapopelekwa kwa kuhani.+  Kuhani atatoka nje ya kambi na kumchunguza. Ikiwa mtu mwenye ukoma amepona,  kuhani atamwamuru alete ndege safi wawili walio hai, tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo ili atakaswe.+  Kuhani ataamuru ndege mmoja achinjwe kwenye chombo cha udongo chenye maji ya kijito.  Lakini anapaswa kumchukua ndege aliye hai na kumtumbukiza pamoja na tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo ndani ya damu ya ndege aliyechinjiwa kwenye maji ya kijito.  Kisha kuhani atachukua damu hiyo na kumnyunyizia mara saba mtu anayejitakasa ukoma wake na kumtangaza kuwa safi, halafu atamwachilia ndege aliye hai aende zake mashambani.+  “Ni lazima mtu anayejitakasa afue mavazi yake, anyoe nywele zake zote, na kuoga kwa maji, kisha atakuwa safi. Baada ya hayo, anaweza kurudi kambini, lakini atakaa nje ya hema lake kwa siku saba.  Siku ya saba anapaswa kunyoa nywele zote kichwani, ndevu zote, na kope zake. Baada ya kunyoa nywele zote, atafua mavazi yake na kuoga kwa maji, kisha atakuwa safi. 10  “Siku ya nane, ataleta wanakondoo dume wawili wasio na kasoro, mwanakondoo jike wa mwaka mmoja asiye na kasoro,+ na sehemu tatu za kumi za kipimo cha efa* ya unga laini uliochanganywa na mafuta kuwa toleo la nafaka,+ na logi moja* ya mafuta;+ 11  na kuhani anayemtangaza kuwa safi atamleta mtu huyo anayejitakasa na matoleo hayo mbele za Yehova kwenye mlango wa hema la mkutano. 12  Kuhani huyo atamchukua yule mwanakondoo dume na kumtoa kuwa dhabihu ya hatia+ pamoja na ile logi moja ya mafuta, naye atavitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ 13  Kisha atamchinjia mwanakondoo huyo mahali ambapo dhabihu za dhambi na dhabihu za kuteketezwa huchinjwa,+ mahali patakatifu, kwa sababu, sawa na dhabihu ya dhambi, dhabihu ya hatia ni ya kuhani.+ Ni dhabihu takatifu kabisa.+ 14  “Kisha kuhani atachukua kiasi kidogo cha damu ya dhabihu ya hatia na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia. 15  Halafu kuhani atachukua kiasi kidogo cha ile logi ya mafuta+ na kumimina kwenye kiganja chake mwenyewe cha mkono wa kushoto. 16  Kisha kuhani atachovya kidole chake cha kulia katika mafuta yaliyo kwenye kiganja chake cha kushoto, atanyunyiza mara saba kwa kidole chake kiasi kidogo cha mafuta hayo mbele za Yehova. 17  Kisha kuhani atatia kiasi kidogo cha mafuta yaliyobaki kwenye kiganja chake na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia juu ya damu ya dhabihu ya hatia. 18  Kuhani atatia mafuta yaliyobaki kwenye kiganja chake na kumpaka kichwani mtu anayejitakasa, naye kuhani atamtolea mtu huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova.+ 19  “Kuhani atatoa dhabihu ya dhambi+ na kumtolea dhabihu ya kufunika dhambi mtu anayejitakasa uchafu wake, kisha atamchinja mnyama wa dhabihu ya kuteketezwa. 20  Kuhani atatoa dhabihu ya kuteketezwa na toleo la nafaka+ kwenye madhabahu, naye atamtolea mtu huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake,+ naye atakuwa safi.+ 21  “Hata hivyo, ikiwa mtu huyo ni maskini na hawezi kupata vitu hivyo, basi ataleta mwanakondoo dume mmoja atolewe kuwa dhabihu ya hatia na toleo la kutikiswa, ili atoe dhabihu ya kufunika dhambi yake, pia ataleta sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja* ya unga laini uliochanganywa na mafuta ili uwe toleo la nafaka, logi ya mafuta, 22  na njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga, kulingana na uwezo wake. Ndege mmoja atatolewa kuwa dhabihu ya dhambi na wa pili dhabihu ya kuteketezwa.+ 23  Siku ya nane+ atawaleta kwa kuhani kwenye mlango wa hema la mkutano mbele za Yehova ili kuthibitisha utakaso wake.+ 24  “Kuhani atamchukua mwanakondoo dume wa dhabihu ya hatia+ na logi ya mafuta na kuvitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ 25  Kisha atamchinja kondoo dume mchanga wa dhabihu ya hatia na kuchukua kiasi kidogo cha damu ya dhabihu ya hatia na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia.+ 26  Kuhani atamimina kiasi kidogo cha mafuta hayo kwenye kiganja chake mwenyewe cha mkono wa kushoto,+ 27  kisha atanyunyiza kwa kidole chake cha kulia kiasi kidogo cha mafuta yaliyo kwenye kiganja chake cha kushoto mara saba mbele za Yehova. 28  Naye atatia kiasi kidogo cha mafuta yaliyo kwenye kiganja chake na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia sehemu zilezile alizompaka damu ya dhabihu ya hatia. 29  Kisha kuhani atatia mafuta yaliyobaki kwenye kiganja chake na kumpaka kichwani mtu anayejitakasa ili amtolee mtu huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova. 30  “Atatoa njiwa tetere mmoja kati ya wale wawili au hua mmoja mchanga kati ya wale wawili, kulingana na uwezo wake,+ 31  atatoa ndege anaoweza kupata, mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na mwingine kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa,+ ataleta pia toleo la nafaka; na kuhani atamtolea mtu huyo anayejitakasa dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova.+ 32  “Hiyo ndiyo sheria inayomhusu mtu aliyekuwa na ugonjwa wa ukoma lakini hana uwezo wakati wa kuthibitisha utakaso wake.” 33  Kisha Yehova akamwambia Musa na Haruni: 34  “Mtakapoingia katika nchi ya Kanaani,+ ambayo ninawapa ili mwimiliki,+ nami niipige kwa ukoma nyumba fulani katika nchi yenu,+ 35  mwenye nyumba hiyo anapaswa kwenda kwa kuhani na kumwambia, ‘Nimeona madoa fulani ndani ya nyumba yangu.’ 36  Kuhani ataagiza vitu vyote vilivyo ndani ya nyumba hiyo vitolewe nje kabla hajaja kuikagua, ili asitangaze kwamba kila kitu kilicho katika nyumba hiyo si safi; baada ya hilo ataingia ndani na kuikagua. 37  Atachunguza sehemu zilizoathiriwa, na ikiwa kuta za nyumba hiyo zina sehemu zilizobonyea zenye mchanganyiko wa rangi ya manjano na kijani au rangi nyekundu, na sehemu hizo zinaonekana zimebonyea sana ukutani, 38  basi kuhani atatoka nje ya mlango wa nyumba hiyo na kuifunga kwa siku saba.+ 39  “Kisha kuhani atarudi siku ya saba na kuikagua. Ikiwa madoa yameenea katika kuta za nyumba hiyo, 40  ndipo kuhani ataagiza mawe yaliyoathiriwa yabomolewe na kutupwa nje ya jiji, mahali pasipo safi. 41  Kisha ataagiza nyumba hiyo ikwanguliwe kabisa sehemu ya ndani, na lipu na saruji iliyoondolewa itatupwa nje ya jiji, mahali pasipo safi. 42  Kisha wataleta mawe mengine na kuyaweka mahali ambapo mawe ya kwanza yalikuwepo; anapaswa kutumia saruji nyingine kuipiga lipu nyumba hiyo. 43  “Hata hivyo, madoa yakitokea tena na kuenea ndani ya nyumba hiyo baada ya mawe kubomolewa na nyumba kukwanguliwa na kupigwa lipu tena, 44  kuhani ataingia ndani na kuikagua. Ikiwa madoa hayo yameenea, nyumba hiyo ina ukoma hatari.+ Si safi. 45  Ataagiza nyumba hiyo ibomolewe, yaani, mawe yake, mbao zake, na lipu yote katika nyumba hiyo, kisha vitu hivyo vitatupwa nje ya jiji, mahali pasipo safi.+ 46  Lakini mtu yeyote atakayeingia ndani ya nyumba hiyo siku yoyote itakapokuwa imetengwa,+ hatakuwa safi mpaka jioni;+ 47  na yeyote anayelala katika nyumba hiyo anapaswa kufua mavazi yake, na yeyote anayekula chakula katika nyumba hiyo anapaswa kufua mavazi yake. 48  “Hata hivyo, kuhani akija na kuona kwamba madoa hayajaenea baada ya nyumba hiyo kupigwa lipu tena, ataitangaza nyumba hiyo kuwa safi, kwa sababu ukoma umekwisha. 49  Ili kuitakasa nyumba hiyo isiyo safi,* atachukua ndege wawili, tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo.+ 50  Atamchinjia ndege mmoja kwenye chombo cha udongo chenye maji ya kijito. 51  Kisha atamchukua ndege aliye hai na kumtumbukiza pamoja na tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo ndani ya damu ya ndege aliyechinjiwa kwenye maji ya kijito, naye atainyunyiza kuelekea nyumba hiyo mara saba.+ 52  Naye ataitakasa nyumba hiyo isiyo safi* kwa kutumia damu ya ndege huyo, maji ya kijito, yule ndege aliye hai, tawi la mwerezi, tawi la hisopo, na kitambaa cha rangi nyekundu. 53  Kisha atamwachilia ndege aliye hai aende zake mashambani nje ya jiji, naye ataitolea nyumba hiyo dhabihu ya kufunika dhambi, nayo itakuwa safi. 54  “Hiyo ndiyo sheria kuhusu aina mbalimbali za ukoma: ukoma wa kichwa au kidevu,+ 55  ukoma wa mavazi+ au nyumba,+ 56  uvimbe, vigaga, na madoa,+ 57  ili kuthibitisha ikiwa kitu ni safi au si safi.+ Hiyo ndiyo sheria kuhusu ukoma.”+

Maelezo ya Chini

Sehemu tatu za kumi za efa zilikuwa sawa na lita 6.6 au kilogramu 3.9 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Logi ilikuwa sawa na lita 0.3. Angalia Nyongeza B14.
Sehemu ya kumi ya efa ilikuwa sawa na lita 2.2 au kilogramu 1.3 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “yenye dhambi.”
Tnn., “yenye dhambi.”