Mambo ya Walawi 2:1-16

  • Toleo la nafaka (1-16)

2  “‘Sasa ikiwa mtu atamtolea Yehova toleo la nafaka,+ ni lazima toleo lake liwe la unga laini, naye anapaswa kumimina mafuta juu yake na kuweka ubani juu yake.+  Kisha atalipeleka kwa wana wa Haruni, makuhani, naye kuhani atachukua mkono mmoja wa unga huo laini, mafuta, pamoja na ubani wake wote, naye atauteketeza ili ufuke moshi ikiwa dhabihu ya kumbukumbu*+ juu ya madhabahu. Ni dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.  Chochote kinachobaki cha toleo hilo la nafaka kitakuwa cha Haruni na wanawe,+ kitakuwa kitu kitakatifu kabisa+ kutoka kwa dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto.  “‘Mkitoa nafaka ambayo imeokwa kwenye jiko, inapaswa kuwa ya unga laini, mikate ya mviringo isiyo na chachu na iliyokandwa kwa mafuta, au mikate myembamba isiyo na chachu ambayo imepakwa mafuta.+  “‘Mkitoa toleo la nafaka kutoka katika kiokeo,+ inapaswa kuwa ya unga laini usio na chachu, uliokandwa kwa mafuta.  Toleo hilo litavunjwa vipandevipande na mafuta yatamiminwa juu yake.+ Ni toleo la nafaka.  “‘Mkitoa toleo la nafaka iliyokaangwa kwenye kikaangio, linapaswa kuwa la unga laini uliokandwa kwa mafuta.  Mnapaswa kumletea Yehova toleo la nafaka lililotengenezwa kwa vitu hivyo, nalo litapelekwa kwa kuhani ambaye atalipeleka karibu na madhabahu.  Naye kuhani atachukua sehemu ya toleo hilo la nafaka ikiwa dhabihu ya kumbukumbu*+ na kuiteketeza juu ya madhabahu ili ifuke moshi. Ni dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.+ 10  Chochote kinachobaki cha toleo hilo la nafaka kitakuwa cha Haruni na wanawe, kitakuwa kitu kitakatifu kabisa kutoka kwa dhabihu za Yehova zinazoteketezwa.+ 11  “‘Toleo lolote la nafaka mnalomtolea Yehova halipaswi kutiwa chachu,+ kwa maana hampaswi kuuteketeza unga wowote uliokandwa ulio na chachu au kuiteketeza asali ili ifuke moshi ikiwa toleo la Yehova linalochomwa kwa moto. 12  “‘Mnaweza kumtolea Yehova vitu hivyo vikiwa mazao ya kwanza,+ lakini hampaswi kuvileta kwenye madhabahu vikiwa dhabihu ya kuteketezwa yenye harufu inayopendeza.* 13  “‘Kila toleo la nafaka mnalotoa linapaswa kukolezwa kwa chumvi; na msiruhusu kamwe chumvi ya agano la Mungu wenu ikosekane katika toleo lenu la nafaka. Kila toleo mtakalotoa, mtalitoa pamoja na chumvi.+ 14  “‘Mkimtolea Yehova mavuno ya kwanza ya nafaka iliyokomaa yakiwa toleo la nafaka, mnapaswa kutoa masuke mabichi yaliyokaangwa kwa moto, chengachenga za nafaka mbichi iliyopondwa, kuwa toleo la nafaka la mavuno yenu ya kwanza yaliyokomaa.+ 15  Mnapaswa kutia mafuta na ubani juu yake. Ni toleo la nafaka. 16  Kuhani ataiteketeza ikiwa dhabihu ya kumbukumbu*+ ili ifuke moshi, yaani, baadhi ya chengachenga za nafaka pamoja na mafuta na ubani wake wote. Ni dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.

Maelezo ya Chini

Au “ikiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Au “ikiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”
Au “inayotuliza.”
Au “ikiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”