Mambo ya Walawi 24:1-23

  • Mafuta kwa ajili ya taa za hema la ibada (1-4)

  • Mikate ya wonyesho (5-9)

  • Aliyelitukana jina la Mungu apigwa mawe (10-23)

24  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Waamuru Waisraeli wakuletee mafuta safi ya zeituni zilizopondwa ili taa ziwake daima.+  Katika hema la mkutano, nje ya pazia lililo karibu na sanduku la ushahidi, Haruni atahakikisha kwamba taa hizo zinawaka daima kuanzia jioni mpaka asubuhi mbele za Yehova. Hiyo ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote.  Haruni anapaswa kupanga taa hizo kwa utaratibu kwenye kinara cha taa+ cha dhahabu safi mbele za Yehova daima.  “Utachukua unga laini na kuoka mikate 12 ya mviringo. Utatumia sehemu mbili za kumi za kipimo cha efa* cha unga laini kuoka kila mkate.  Utaipanga mikate hiyo kwenye safu* mbili juu ya meza ya dhahabu safi mbele za Yehova,+ kila safu itakuwa na mikate sita.+  Unapaswa kuweka ubani safi juu ya kila safu, na mikate hiyo itakuwa dhabihu ya kumbukumbu*+ inayochomwa kwa moto mbele za Yehova.  Kila siku ya Sabato, anapaswa kupanga mikate hiyo mbele za Yehova kwa ukawaida.+ Ni agano linalodumu kati yangu na Waisraeli.  Itakuwa ya Haruni na wanawe,+ nao wataila mahali patakatifu,+ kwa sababu ni kitu kitakatifu kabisa kwa ajili ya kuhani kutoka kwa dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto; itakuwa sheria ya kudumu.” 10  Siku moja, miongoni mwa Waisraeli, mwana fulani ambaye mama yake ni Mwisraeli na baba yake ni Mmisri+ alipigana na mwanamume Mwisraeli kambini. 11  Mwana huyo wa mwanamke Mwisraeli akaanza kulikufuru lile Jina* na kulitukana.+ Basi wakamleta kwa Musa.+ Kumbe mama yake alikuwa Shelomithi, binti ya Dibri wa kabila la Dani. 12  Kwa hiyo wakamtia kifungoni mpaka walipojulishwa uamuzi wa Yehova.+ 13  Kisha Yehova akamwambia Musa: 14  “Mtoeni nje ya kambi yule aliyelitukana, na wale wote waliomsikia wanapaswa kuweka mikono yao juu ya kichwa chake, kisha Waisraeli wote watampiga mawe.+ 15  Nawe utawaambia hivi Waisraeli: ‘Mtu yeyote akimtukana Mungu wake, atawajibika kwa sababu ya dhambi yake. 16  Kwa hiyo yule aliyelitukana jina la Yehova lazima auawe.+ Kwa hakika kusanyiko lote linapaswa kumpiga mawe. Mgeni anapaswa kuuawa sawasawa na mwenyeji kwa sababu ya kulitukana lile Jina. 17  “‘Mtu anayemuua mwanadamu mwenzake* lazima auawe.+ 18  Mtu yeyote anayempiga na kumuua mnyama wa kufugwa* anapaswa kulipa fidia, uhai kwa uhai.* 19  Mtu akimjeruhi mwanadamu mwenzake, basi anapaswa kutendewa jambo alilotenda.+ 20  Mfupa uliovunjika kwa mfupa uliovunjika, jicho kwa jicho, jino kwa jino, atajeruhiwa kama alivyomjeruhi mwenzake.+ 21  Mtu anayempiga na kumuua mnyama anapaswa kulipa fidia,+ lakini mtu anayempiga na kumuua mwanadamu anapaswa kuuawa.+ 22  “‘Sheria itakuwa moja kwenu, iwe ni mgeni au mwenyeji,+ kwa sababu mimi ni Yehova Mungu wenu.’” 23  Basi Musa akawaambia Waisraeli mambo hayo, wakamtoa nje ya kambi yule aliyelitukana lile Jina, wakampiga mawe.+ Kwa hiyo Waisraeli wakafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa.

Maelezo ya Chini

Sehemu mbili za kumi za efa zilikuwa sawa na lita 4.4 au kilogramu 2.6 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Au “tabaka.”
Au “itakuwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”
Yaani, jina Yehova, kulingana na mstari wa 15 na 16.
Au “anayeua nafsi yoyote ya mwanadamu.”
Au “anayepiga na kuua nafsi ya mnyama.”
Au “nafsi kwa nafsi.”