Mambo ya Walawi 25:1-55

  • Mwaka wa Sabato (1-7)

  • Mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50 (8-22)

  • Kurudishwa kwa mali (23-34)

  • Jinsi ya kuwatendea maskini (35-38)

  • Sheria kuhusu utumwa (39-55)

25  Yehova akaendelea kumwambia Musa kwenye Mlima Sinai,  “Waambie hivi Waisraeli: ‘Hatimaye mtakapoingia katika nchi ninayowapa,+ nchi hiyo itashika sabato ya Yehova.+  Kwa miaka sita mtapanda mbegu katika mashamba yenu, mtapunguza matawi ya mizabibu yenu, na kuvuna mazao ya nchi.+  Lakini katika mwaka wa saba nchi itakuwa na pumziko kamili la sabato, sabato ya Yehova. Hampaswi kupanda mbegu wala kupunguza matawi ya mizabibu yenu.  Hampaswi kuvuna nafaka yoyote inayoota yenyewe baada ya mavuno, nanyi hampaswi kuchuma zabibu kutoka kwenye mizabibu yenu ambayo haijapunguzwa matawi. Ni lazima nchi iwe na mwaka wa pumziko kamili.  Hata hivyo, mnaweza kula mazao yanayoota nchini mwaka huo wa sabato, yaani, mtayala ninyi wenyewe, na pia watumwa wenu wa kike na wa kiume, vibarua wenu, wageni wanaoishi nanyi,  na pia wanyama wenu wa kufugwa na wanyama wa mwituni walio katika nchi yenu. Mnaweza kula mazao yote nchini.  “‘Mtahesabu miaka saba ya sabato, miaka saba mara saba, jumla ya miaka 49.  Kisha mtapiga pembe kwa sauti kubwa katika mwezi wa saba, siku ya kumi ya mwezi huo; katika Siku ya Kufunika Dhambi+ mnapaswa kupiga pembe katika nchi yenu yote. 10  Mtautakasa mwaka wa 50 na kutangaza uhuru kwa wakaaji wote nchini.+ Utakuwa Mwadhimisho wa Miaka 50, na kila mmoja atarudi kwenye urithi wake na kila mmoja wenu atarudi kwa familia yake.+ 11  Mwaka huo utakuwa mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50. Hamtapanda mbegu wala kuvuna nafaka iliyoota yenyewe wala kuchuma zabibu kutoka kwenye mizabibu ambayo haijapunguzwa matawi.+ 12  Kwa maana ni Mwadhimisho wa Miaka 50, ni mwaka mtakatifu kwenu. Mnaweza kula tu mazao yanayoota yenyewe nchini.+ 13  “‘Katika mwaka huo wa 50, kila mmoja wenu anapaswa kurudi kwenye urithi wake.+ 14  Ukiuza au kununua chochote kutoka kwa mwenzako, usimpunje.+ 15  Bei ya unachonunua inapaswa kulingana na idadi ya miaka ambayo imepita baada ya Mwadhimisho wa Miaka 50, naye anapaswa kukuuzia kulingana na idadi ya miaka inayobaki ya mazao.+ 16  Ikiwa miaka inayobaki ni mingi, anaweza kuongeza bei, na ikiwa ni michache anapaswa kupunguza bei kwa sababu anakuuzia idadi ya mazao utakayovuna. 17  Hakuna yeyote kati yenu anayepaswa kumpunja mwenzake,+ ni lazima mmwogope Mungu wenu,+ kwa sababu mimi ni Yehova Mungu wenu.+ 18  Mkishika amri zangu na kufuata sheria zangu,* mtaishi kwa usalama nchini.+ 19  Nchi itazaa mazao yake,+ nanyi mtakula na kushiba na kuishi humo kwa usalama.+ 20  “‘Iwapo mtauliza: “Tutakula nini katika mwaka wa saba tusipopanda mbegu au kuvuna mazao yetu?”+ 21  Nitaamuru baraka zangu zije juu yenu katika mwaka wa sita, nayo nchi itazaa mazao ya kutosha kwa miaka mitatu.+ 22  Nanyi mtapanda mbegu mwaka wa nane na kula mavuno ya miaka iliyotangulia mpaka mwaka wa tisa. Mtakula mavuno hayo mpaka mtakapovuna mwaka huo. 23  “‘Kwa hiyo ardhi haipaswi kuuzwa kwa muda wa kudumu,+ kwa sababu nchi ni yangu.+ Kwa maana ninyi ni wageni na wahamiaji machoni pangu.+ 24  Katika nchi yote mnayomiliki, mtakuwa na haki ya kukomboa* ardhi mliyouza. 25  “‘Ikiwa ndugu yako atakuwa maskini na hivyo alazimike kuuza sehemu fulani ya urithi wake, basi mkombozi ambaye ni mtu wake wa karibu wa ukoo atakuja na kununua sehemu iliyouzwa na ndugu yake.+ 26  Ikiwa mtu hana mkombozi lakini anapata ufanisi na kupata uwezo wa kuikomboa, 27  anapaswa kuhesabu thamani yake kulingana na miaka iliyopita tangu alipoiuza na kumrudishia yule aliyeinunua kiasi kinachobaki. Kisha atarudi kwenye urithi wake.+ 28  “‘Lakini ikiwa hana uwezo wa kuikomboa sehemu aliyouza, sehemu hiyo itabaki mikononi mwa mnunuzi mpaka mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50;+ kisha atarudishiwa sehemu hiyo mwaka huo, naye atarudi kwenye urithi wake.+ 29  “‘Mtu akiuza nyumba yake iliyo katika jiji lililozingirwa na ukuta, anaweza kuikomboa mwaka mmoja tangu alipoiuza; kwa mwaka mzima atakuwa na haki ya kuikomboa.+ 30  Lakini ikiwa haitakombolewa katika muda wa mwaka mzima, nyumba hiyo iliyozingirwa na ukuta itakuwa mali ya kudumu ya yule aliyeinunua katika vizazi vyake vyote. Haipaswi kurudishwa wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50. 31  Hata hivyo, nyumba zilizo katika vijiji ambavyo havijazingirwa na ukuta zinapaswa kuhesabiwa kama mashamba. Zinaweza kukombolewa, nazo zinapaswa kurudishwa wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50. 32  “‘Lakini Walawi wana haki ya kukomboa nyumba zao zilizo katika majiji yao+ wakati wowote. 33  Mlawi asipokomboa nyumba yake, nyumba hiyo iliyouzwa katika jiji la Walawi itarudishwa wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50,+ kwa sababu nyumba zilizo katika majiji ya Walawi ni urithi wao miongoni mwa Waisraeli.+ 34  Isitoshe, malisho+ yanayozunguka majiji yao hayapaswi kuuzwa, kwa sababu ni urithi wao wa kudumu. 35  “‘Ikiwa ndugu yako aliye karibu nawe amekuwa maskini na hawezi kujiruzuku, unapaswa kumsaidia,+ kama ambavyo ungemsaidia mgeni na pia mhamiaji,+ ili aendelee kuwa hai kama wewe. 36  Usimtoze riba au kujipatia faida kutoka kwake.+ Ni lazima umwogope Mungu wako,+ na ndugu yako ataendelea kuwa hai kama wewe. 37  Usimkopeshe pesa kwa riba+ au kumpa chakula ili upate faida. 38  Mimi ni Yehova Mungu wenu, niliyewatoa nchini Misri+ ili kuwapa nchi ya Kanaani, ili nijithibitishe kuwa Mungu wenu.+ 39  “‘Ikiwa ndugu yako anayeishi karibu nawe amelazimika kujiuza kwako+ kwa sababu amekuwa maskini, usimlazimishe akutumikie kama mtumwa.+ 40  Unapaswa kumtendea kama kibarua,+ kama mhamiaji. Atakutumikia mpaka wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50. 41  Kisha atakuacha, yeye na watoto* wake, na kurudi kwa watu wake wa ukoo. Anapaswa kurudi kwenye urithi wa mababu zake.+ 42  Kwa maana wao ni watumwa wangu niliowatoa nchini Misri.+ Hawapaswi kujiuza kama mtumwa anavyouzwa. 43  Usimtendee kwa ukatili,+ ni lazima umwogope Mungu wako.+ 44  Utawachukua watumwa wa kike na wa kiume kutoka katika mataifa jirani, unaweza kumnunua mtumwa wa kiume au wa kike kutoka katika mataifa hayo. 45  Pia unaweza kununua watumwa kutoka miongoni mwa wana wa wageni wanaoishi nawe+ na kutoka kati ya watu wa familia zao waliozaliwa katika nchi yenu, nao watakuwa mali yako. 46  Unaweza kuwarithisha kwa wana wako ili wawe mali yao ya kudumu. Unaweza kuwatumia watumwa hao kama wafanyakazi, lakini usiwatendee ndugu zako Waisraeli kwa ukatili.+ 47  “‘Lakini ikiwa mgeni au mhamiaji miongoni mwenu amekuwa tajiri na ndugu yako amekuwa maskini kando yake na hivyo analazimika kujiuza kwa mgeni au mhamiaji huyo anayeishi miongoni mwenu, au kwa mtu wa ukoo wa mgeni huyo, 48  ndugu yako ambaye amejiuza ataendelea kuwa na haki ya ukombozi hata baada ya kujiuza. Mmoja wa ndugu zake anaweza kumkomboa,+ 49  au anaweza kukombolewa na ndugu ya baba yake au binamu yake, au na mtu yeyote wa karibu wa ukoo,* yaani, mtu wa familia yake. “‘Au anaweza kujikomboa mwenyewe akipata utajiri.+ 50  Yeye pamoja na mtu aliyemnunua watahesabu idadi ya miaka tangu mwaka aliojiuza mpaka mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50,+ na bei ya kukombolewa kwake itahesabiwa kulingana na idadi hiyo ya miaka.+ Muda aliofanya kazi utapimwa kama muda wa mtu anayefanya kazi ya kibarua.+ 51  Ikiwa miaka inayobaki ni mingi, anapaswa kulipa bei yake ya ukombozi kulingana na miaka inayobaki. 52  Lakini ikiwa ni miaka michache tu inayobaki kabla ya mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, anapaswa kuhesabu mwenyewe bei yake ya ukombozi na kulipa kulingana na miaka inayobaki. 53  Ataendelea kumtumikia kama kibarua mwaka baada ya mwaka; mnapaswa kuhakikisha kwamba yule aliyemnunua hamtendei kwa ukatili.+ 54  Hata hivyo, ikiwa hawezi kujinunua kulingana na masharti hayo, ataachiliwa huru pamoja na watoto* wake wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50.+ 55  “‘Kwa maana Waisraeli ni watumwa wangu mwenyewe. Ni watumwa wangu niliowatoa nchini Misri.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.

Maelezo ya Chini

Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Au “kununua tena.”
Tnn., “wana.”
Au “mwenye uhusiano wa damu naye.”
Tnn., “wana.”