Mambo ya Walawi 27:1-34

  • Kukomboa vitu vilivyowekwa nadhiri (1-27)

  • Vitu vilivyotolewa kwa Yehova bila masharti (28, 29)

  • Kukomboa sehemu za kumi (30-34)

27  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Waambie hivi Waisraeli: ‘Mtu akiweka nadhiri ya pekee+ ya kumtolea Yehova thamani inayokadiriwa ya mtu,*  thamani ya mwanamume mwenye umri wa kuanzia miaka 20 mpaka miaka 60 itakadiriwa kuwa shekeli 50* za fedha kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.*  Lakini ikiwa ni mwanamke, thamani yake itakadiriwa kuwa shekeli 30.  Ikiwa mtu ana umri wa kuanzia miaka 5 mpaka miaka 20, thamani ya mwanamume itakadiriwa kuwa shekeli 20 na ya mwanamke shekeli 10.  Ikiwa mtu ana umri wa kuanzia mwezi mmoja mpaka miaka mitano, thamani ya mtoto wa kiume itakadiriwa kuwa shekeli tano za fedha na ya mtoto wa kike shekeli tatu za fedha.  “‘Ikiwa mtu ana umri wa miaka 60 na zaidi, thamani ya mwanamume itakadiriwa kuwa shekeli 15 na ya mwanamke shekeli 10.  Lakini ikiwa mtu anayeweka nadhiri hawezi kulipa thamani iliyokadiriwa kwa sababu ni maskini sana,+ mtu huyo atasimama mbele ya kuhani, naye kuhani atakadiria thamani yake. Atakadiria thamani yake kulingana na kiasi ambacho mtu anayeweka nadhiri anaweza kulipa.+  “‘Ikiwa nadhiri inahusisha mnyama anayestahili kutolewa kwa Yehova, basi chochote kinachotolewa kwa Yehova kitakuwa kitu kitakatifu. 10  Hawezi kumbadilisha mnyama aliyemweka kuwa nadhiri, yaani, achukue mnyama mzuri na kumtoa mbaya, au achukue mbaya na kumtoa mzuri. Lakini akimbadilisha mnyama huyo na mwingine, wanyama wote wawili watakuwa watakatifu. 11  Ikiwa ni mnyama asiye safi+ ambaye hawezi kutolewa kwa Yehova, mnyama huyo atapelekwa mbele ya kuhani. 12  Halafu kuhani atakadiria thamani yake, ataamua ikiwa ni mzuri au mbaya. Thamani itakayokadiriwa na kuhani ndiyo itakayokuwa thamani ya mnyama huyo. 13  Lakini ikiwa mtu huyo anataka kumnunua tena mnyama huyo, ni lazima alipe thamani ya mnyama huyo pamoja na sehemu ya tano ya thamani iliyokadiriwa.+ 14  “‘Sasa ikiwa mtu ataitakasa nyumba yake ili iwe takatifu kwa Yehova, kuhani atakadiria thamani ya nyumba hiyo, iwapo ni nzuri au ni mbaya. Thamani itakayokadiriwa na kuhani ndiyo itakayokuwa bei yake.+ 15  Lakini ikiwa mtu anayetakasa nyumba yake anataka kuinunua tena, ni lazima alipe thamani iliyokadiriwa pamoja na sehemu ya tano ya thamani hiyo, kisha itakuwa yake. 16  “‘Mtu akitakasa sehemu fulani ya shamba lake ili iwe ya Yehova, thamani yake itakadiriwa kulingana na kiasi cha mbegu zinazohitajika kupandwa: thamani ya homeri moja* ya mbegu za shayiri itakuwa shekeli 50 za fedha. 17  Ikiwa atalitakasa shamba lake kuanzia mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50,+ thamani yake itabaki kama ilivyokadiriwa. 18  Ikiwa atalitakasa shamba lake baada ya mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, kuhani atakadiria bei kulingana na miaka inayobaki kabla ya mwadhimisho unaofuata wa miaka 50, naye atapunguza thamani iliyokadiriwa.+ 19  Lakini ikiwa yule aliyelitakasa shamba hilo anataka kulinunua tena, ni lazima alipe thamani yake pamoja na sehemu ya tano ya thamani iliyokadiriwa, kisha litakuwa lake. 20  Asipolinunua, kisha mtu mwingine auziwe shamba hilo, haliwezi kununuliwa tena. 21  Yule aliyenunua shamba hilo akiliacha wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50, litakuwa kitu kitakatifu kwa Yehova, shamba lililotolewa kwa ajili yake. Litakuwa mali ya makuhani.+ 22  “‘Mtu akitakasa shamba alilonunua ambalo si sehemu ya urithi wake na kulitoa liwe mali ya Yehova,+ 23  kuhani atamhesabia thamani ya shamba hilo kufikia mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, na mtu huyo atalipa siku hiyo thamani iliyokadiriwa.+ Ni kitu kitakatifu kwa Yehova. 24  Katika mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, shamba litarudishwa kwa yule aliyeliuza, kwa mtu ambaye shamba hilo ni mali yake.+ 25  “‘Thamani ya kila kitu itakadiriwa kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu. Shekeli moja ni sawa na gera 20.* 26  “‘Hata hivyo, hakuna mtu yeyote anayepaswa kumtakasa mzaliwa wa kwanza wa wanyama, kwa sababu mzaliwa wa kwanza ni wa Yehova.+ Awe ni ng’ombe dume au kondoo, tayari ni wa Yehova.+ 27  Ikiwa mtu anamkomboa mnyama asiye safi kulingana na thamani iliyokadiriwa, anapaswa kulipa thamani ya mnyama huyo pamoja na sehemu ya tano ya thamani hiyo.+ Lakini asipomkomboa, mnyama huyo atauzwa kulingana na thamani iliyokadiriwa. 28  “‘Lakini kitu chochote ambacho mtu anamtolea Yehova bila masharti,* iwe ni mwanadamu au mnyama au shamba lake, hakiwezi kuuzwa au kununuliwa tena. Kitu chochote kilichowekwa wakfu ni kitakatifu kabisa kwa Yehova.+ 29  Zaidi ya hayo, mtu yeyote aliyehukumiwa na kutengwa ili aangamizwe hawezi kukombolewa.+ Ni lazima auawe.+ 30  “‘Kila sehemu ya kumi+ ya mazao ya ardhi au matunda ni mali ya Yehova. Sehemu hiyo ni takatifu kwa Yehova. 31  Ikiwa mtu anataka kununua tena sehemu yoyote ya kumi aliyotoa, anapaswa kulipa thamani yake pamoja na sehemu ya tano ya thamani hiyo. 32  Kila sehemu ya kumi ya mifugo na ya kundi, yaani, kila mnyama wa kumi anayepita* chini ya fimbo ya mchungaji atakuwa mtakatifu kwa Yehova. 33  Mtu huyo hapaswi kuchunguza ikiwa mnyama huyo ni mzuri au mbaya, wala hapaswi kumbadilisha na mwingine. Ikiwa atambadilisha na mwingine, basi wanyama wote wawili watakuwa watakatifu.+ Hawawezi kununuliwa tena.’” 34  Hizo ndizo sheria ambazo Yehova alimpa Musa kwenye Mlima Sinai ili awape Waisraeli.+

Maelezo ya Chini

Au “nafsi.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “shekeli takatifu.”
Homeri ni kipimo sawa na lita 220. Angalia Nyongeza B14.
Gera moja ilikuwa na uzito wa gramu 0.57. Angalia Nyongeza B14.
Au “ili kiangamizwe.”
Au “kichwa cha kumi kinachopita.”