Mambo ya Walawi 4:1-35

  • Dhabihu ya dhambi (1-35)

4  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Waambie Waisraeli, ‘Mtu akitenda dhambi bila kukusudia+ kwa kufanya jambo lolote ambalo Yehova ameamuru lisifanywe:  “‘Kuhani aliyetiwa mafuta+ akitenda dhambi+ na kuwaletea watu hatia, basi atamtolea Yehova ng’ombe dume mchanga asiye na kasoro, kuwa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya dhambi aliyotenda.+  Atamleta huyo ng’ombe dume kwenye mlango wa hema la mkutano+ mbele za Yehova na kuweka mkono wake juu ya kichwa cha ng’ombe dume huyo, naye atamchinja mbele za Yehova.+  Kisha kuhani aliyetiwa mafuta+ atachukua kiasi fulani cha damu ya ng’ombe dume huyo na kuileta ndani ya hema la mkutano;  naye atachovya kidole chake ndani ya damu+ hiyo na kunyunyiza kiasi fulani mara saba+ mbele za Yehova, mbele ya pazia la mahali patakatifu.  Pia, kuhani atatia kiasi fulani cha damu hiyo kwenye pembe za madhabahu ya uvumba uliotiwa manukato,+ mbele za Yehova katika hema la mkutano; naye atamwaga damu yote iliyobaki ya huyo ng’ombe dume kwenye msingi wa madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa,+ kwenye mlango wa hema la mkutano.  “‘Kisha ataondoa mafuta yote ya huyo ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi, pamoja na mafuta yanayofunika matumbo na mafuta yanayozunguka matumbo,  na figo zake mbili pamoja na mafuta yake yaliyo karibu na kiuno. Ataondoa pia figo pamoja na mafuta yaliyo juu ya ini.+ 10  Ataondoa sehemu zilezile zinazoondolewa katika ng’ombe dume wa dhabihu ya ushirika.+ Na kuhani ataviteketeza kwenye madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa ili vifuke moshi. 11  “‘Lakini ngozi ya ng’ombe dume huyo na nyama yake yote pamoja na kichwa chake, miguu yake, matumbo yake, na mavi yake+ 12  sehemu zote zinazobaki za ng’ombe dume huyo—atazipeleka mahali safi nje ya kambi, mahali ambapo majivu* hutupwa, naye ataziteketeza kwa moto juu ya kuni.+ Zinapaswa kuteketezwa mahali ambapo majivu hutupwa. 13  “‘Sasa ikiwa kusanyiko lote la Waisraeli lina hatia ya kutenda dhambi bila kukusudia,+ lakini halikujua kwamba limefanya jambo ambalo Yehova aliamuru lisifanywe,+ 14  kisha dhambi hiyo ijulikane, ni lazima kusanyiko litoe ng’ombe dume mchanga kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na kumleta mbele ya hema la mkutano. 15  Wazee wa kusanyiko hilo wataweka mikono yao juu ya kichwa cha ng’ombe dume huyo mbele za Yehova, naye atachinjwa mbele za Yehova. 16  “‘Kisha kuhani aliyetiwa mafuta ataleta kiasi fulani cha damu ya ng’ombe dume huyo katika hema la mkutano. 17  Naye atachovya kidole chake ndani ya damu hiyo na kunyunyiza kiasi fulani mara saba mbele za Yehova, mbele ya pazia.+ 18  Kisha atatia kiasi fulani cha damu hiyo kwenye pembe za madhabahu+ iliyo mbele za Yehova, katika hema la mkutano; naye atamwaga damu yote iliyobaki kwenye msingi wa madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, iliyo kwenye mlango wa hema la mkutano.+ 19  Ataondoa mafuta yake yote na kuyateketeza kwenye madhabahu ili yafuke moshi.+ 20  Atamfanya ng’ombe dume huyo kama alivyomfanya yule ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi. Hivyo ndivyo atakavyomfanya, kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi zao,+ nao watasamehewa. 21  Atampeleka ng’ombe dume huyo nje ya kambi na kumteketeza kama alivyomteketeza ng’ombe dume wa kwanza.+ Ni dhabihu ya dhambi kwa ajili ya kusanyiko lote.+ 22  “‘Ikiwa mkuu+ ametenda dhambi bila kukusudia na hivyo ana hatia ya kufanya jambo lolote ambalo Yehova Mungu wake ameamuru lisifanywe, 23  au akigundua dhambi aliyotenda kinyume cha amri, basi anapaswa kumleta mwanambuzi dume asiye na kasoro ili atolewe dhabihu kwa ajili yake. 24  Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mwanambuzi huyo na kumchinjia mahali ambapo dhabihu za kuteketezwa huchinjwa mbele za Yehova.+ Hiyo ni dhabihu ya dhambi. 25  Kuhani atachukua kwa kidole chake kiasi kidogo cha damu ya dhabihu ya dhambi na kuitia kwenye pembe+ za madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, naye atamwaga damu inayobaki kwenye msingi wa madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa.+ 26  Naye atayateketeza mafuta yake yote kwenye madhabahu ili yafuke moshi kama yale mafuta ya dhabihu ya ushirika;+ naye kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi ya mtu huyo, naye atasamehewa. 27  “‘Mtu yeyote miongoni mwa watu walio nchini akitenda dhambi bila kukusudia na hivyo kuwa na hatia ya kufanya jambo lolote ambalo Yehova ameamuru lisifanywe,+ 28  au akigundua dhambi aliyotenda, basi atamleta mwanambuzi jike asiye na kasoro ili atolewe dhabihu kwa ajili ya dhambi aliyotenda. 29  Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama wa dhabihu ya dhambi na kumchinjia mahali ambapo dhabihu za kuteketezwa huchinjwa.+ 30  Kuhani atachukua kwa kidole chake kiasi kidogo cha damu ya mnyama huyo na kuitia kwenye pembe za madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, naye atamwaga damu yote inayobaki kwenye msingi wa madhabahu.+ 31  Ataondoa mafuta yake yote+ kama mafuta ya dhabihu ya ushirika+ yanavyoondolewa, na kuhani atayateketeza kwenye madhabahu ili yafuke moshi yakiwa harufu inayompendeza* Yehova; naye kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi ya mtu huyo, naye atasamehewa. 32  “‘Lakini akitoa mwanakondoo ili awe dhabihu yake ya dhambi, anapaswa kuleta mwanakondoo jike asiye na kasoro. 33  Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama wa dhabihu ya dhambi na kumchinjia mahali ambapo dhabihu za kuteketezwa huchinjwa.+ 34  Kuhani atachukua kwa kidole chake kiasi kidogo cha damu ya mnyama huyo na kuitia kwenye pembe za madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa,+ naye atamwaga damu yote inayobaki kwenye msingi wa madhabahu. 35  Ataondoa mafuta yake yote kama mafuta ya mwanakondoo dume wa dhabihu ya ushirika yanavyoondolewa, na kuhani atayateketeza kwenye madhabahu juu ya dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto;+ naye kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi ambayo mtu huyo alitenda, naye atasamehewa.+

Maelezo ya Chini

Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.
Au “inayomtuliza.”