Mambo ya Walawi 8:1-36

  • Haruni na wanawe wawekwa rasmi kuwa makuhani (1-36)

8  Yehova akaendelea kumwambia Musa:   “Mchukue Haruni na wanawe,+ pamoja na mavazi yao,+ na mafuta yanayotumiwa kutia mafuta,+ ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi, kondoo dume wawili, na kikapu cha mikate isiyo na chachu,+  uwakusanye Waisraeli wote kwenye mlango wa hema la mkutano.”  Basi Musa akafanya kama Yehova alivyomwamuru, Waisraeli wote wakakusanyika kwenye mlango wa hema la mkutano.  Musa akawaambia: “Hili ndilo jambo ambalo Yehova ameamuru tufanye.”  Kwa hiyo Musa akamleta Haruni na wanawe na kuwaosha kwa maji.+  Kisha akamvisha kanzu,+ akamfunga ukumbuu,+ akamvisha lile joho lisilo na mikono,+ akamvisha efodi+ na kumfunga vizuri kabisa mshipi wa efodi uliofumwa.+  Halafu akamvisha kifuko cha kifuani+ na kutia Urimu na Thumimu+ ndani ya kifuko hicho.  Kisha akamvisha kilemba+ kichwani na kuweka lile bamba linalong’aa la dhahabu upande wa mbele wa kilemba hicho, ile ishara takatifu ya wakfu,*+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 10  Kisha Musa akachukua mafuta yanayotumiwa kutia mafuta akalitia mafuta hema la ibada na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake,+ akavitakasa. 11  Baada ya hayo akanyunyiza kiasi fulani cha mafuta hayo juu ya madhabahu mara saba na kuitia mafuta madhabahu, vyombo vyake vyote, na pia beseni na kinara chake, ili kuvitakasa. 12  Mwishowe akamimina juu ya kichwa cha Haruni kiasi fulani cha mafuta hayo yanayotumiwa kutia mafuta, akamtia mafuta ili kumtakasa.+ 13  Halafu Musa akawaleta wana wa Haruni, akawavisha kanzu, akawafunga ukumbuu, na kuwavisha kofia,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 14  Kisha akamleta ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi, Haruni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha ng’ombe dume huyo wa dhabihu ya dhambi.+ 15  Musa akamchinja, akachukua damu yake+ kwa kidole chake na kuzipaka pembe zote za madhabahu, akaitakasa madhabahu kutokana na dhambi, lakini damu iliyobaki aliimwaga kwenye msingi wa madhabahu, ili aitakase na kutoa juu yake dhabihu ya kufunika dhambi. 16  Kisha Musa akachukua mafuta yote yaliyofunika matumbo, mafuta yaliyo juu ya ini, na figo mbili pamoja na mafuta yake, akateketeza vitu hivyo juu ya madhabahu ili vifuke moshi.+ 17  Kisha akachukua sehemu zilizobaki za ng’ombe dume huyo, ngozi yake, nyama yake, na mavi yake, akateketeza sehemu hizo nje ya kambi,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 18  Halafu akamleta kondoo dume wa dhabihu ya kuteketezwa, Haruni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo dume huyo.+ 19  Musa akamchinja na kunyunyiza damu yake pande zote za madhabahu. 20  Akamkata kondoo huyo vipandevipande, akateketeza kichwa, vipande alivyokata, na mafuta yaliyo kwenye figo, ili vifuke moshi. 21  Akaosha matumbo na miguu kwa maji na kumteketeza kondoo dume mzima kwenye madhabahu ili afuke moshi. Ilikuwa dhabihu ya kuteketezwa yenye harufu inayopendeza.* Ilikuwa dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto, kama Yehova alivyomwamuru Musa. 22  Kisha akamleta kondoo dume wa pili, kondoo wa kuwaweka rasmi makuhani,+ basi Haruni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.+ 23  Musa akamchinja na kuchukua kiasi fulani cha damu yake na kuipaka kwenye ncha ya sikio la kulia la Haruni na kwenye kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kwenye kidole gumba cha mguu wake wa kulia. 24  Kisha Musa akawaleta wana wa Haruni na kuwapaka damu hiyo kwenye ncha za masikio yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya mikono yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya miguu yao ya kulia; lakini damu iliyobaki Musa aliinyunyiza pande zote za madhabahu.+ 25  Kisha akachukua yale mafuta, mkia wenye mafuta, mafuta yote yaliyofunika matumbo, mafuta yote yaliyokuwa juu ya ini, zile figo mbili na mafuta yake, na mguu wa kulia.+ 26  Akachukua mkate mmoja wa mviringo usio na chachu,+ mkate mmoja wa mviringo wenye mafuta,+ na mkate mmoja mwembamba kutoka katika kikapu cha mikate isiyo na chachu kilichokuwa mbele za Yehova. Akaiweka mikate hiyo juu ya vipande vya mafuta na juu ya mguu wa kulia. 27  Baada ya hayo akaviweka vitu hivyo vyote katika mikono ya Haruni na mikono ya wanawe na kuanza kuvitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova. 28  Kisha Musa akavichukua kutoka mikononi mwao na kuviteketeza kwenye madhabahu juu ya dhabihu ya kuteketezwa ili vifuke moshi. Vitu hivyo vilikuwa dhabihu ya kuwaweka rasmi makuhani, dhabihu yenye harufu ya kupendeza.* Vilikuwa dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto. 29  Kisha Musa akachukua kidari na kukitikisa kwenda mbele na nyuma kikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ Sehemu hiyo ya kondoo wa kuwaweka rasmi makuhani ilikuwa fungu la Musa, kama Yehova alivyomwamuru Musa.+ 30  Halafu Musa akachukua kiasi kidogo cha mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na kiasi kidogo cha damu iliyokuwa kwenye madhabahu, akamnyunyizia Haruni na mavazi yake na pia wanawe na mavazi yao. Basi akamtakasa Haruni na mavazi yake na pia wanawe+ na mavazi yao.+ 31  Kisha Musa akamwambia Haruni na wanawe: “Chemsheni+ nyama hiyo kwenye mlango wa hema la mkutano, na muile hapo mlangoni pamoja na mikate iliyo katika kikapu cha kuwaweka rasmi makuhani, kama nilivyoamriwa kwamba, ‘Haruni na wanawe wataila.’+ 32  Mtateketeza nyama na mikate itakayobaki.+ 33  Hampaswi kutoka nje ya mlango wa hema la mkutano kwa siku saba, mpaka siku zenu za kuwekwa rasmi kuwa makuhani zitakapokwisha, kwa sababu itachukua muda wa siku saba kuwaweka rasmi kuwa makuhani.+ 34  Yehova alituamuru tufanye mambo tuliyofanya leo ili tuwatolee dhabihu ya kufunika dhambi zenu.+ 35  Mtakaa kwenye mlango wa hema la mkutano kwa siku saba,+ mchana na usiku, nanyi mtatimiza wajibu wenu mbele za Yehova,+ msije mkafa; hivyo ndivyo nilivyoamriwa.” 36  Basi Haruni na wanawe wakafanya mambo yote ambayo Yehova aliamuru kupitia Musa.

Maelezo ya Chini

Au “lile taji takatifu.”
Au “inayotuliza.”
Au “kutuliza.”