Mambo ya Walawi 9:1-24

  • Haruni atoa dhabihu za kumweka rasmi kuwa kuhani (1-24)

9  Siku ya nane,+ Musa akamwita Haruni na wanawe na wazee wa Israeli.  Akamwambia Haruni: “Chukua ndama mchanga kwa ajili ya dhabihu ya dhambi+ na kondoo dume kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa, wanyama wasio na kasoro, nawe uwatoe mbele za Yehova.  Lakini utawaambia Waisraeli ‘Chukueni mbuzi dume kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na ndama na mwanakondoo dume, wote wa umri wa mwaka mmoja na wasio na kasoro, kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa,  na ng’ombe dume na kondoo dume kwa ajili ya dhabihu za ushirika,+ ili muwatoe dhabihu mbele za Yehova, na pia toleo la nafaka+ lililochanganywa na mafuta, kwa sababu leo Yehova atawatokea.’”+  Basi wakapeleka vitu ambavyo Musa aliamuru mbele ya hema la mkutano. Halafu Waisraeli wote wakaja na kusimama mbele za Yehova.  Musa akasema: “Hili ndilo jambo ambalo Yehova amewaamuru mfanye, ili muone utukufu wa Yehova.”+  Kisha Musa akamwambia Haruni: “Nenda kwenye madhabahu, utoe dhabihu yako ya dhambi+ na dhabihu yako ya kuteketezwa, utoe dhabihu ya kufunika dhambi zako mwenyewe+ na za nyumba yako; kisha uwatolee watu dhabihu ya kufunika dhambi zao,+ kama Yehova alivyoamuru.”  Haruni akaenda mara moja kwenye madhabahu na kumchinja yule ndama wa dhabihu ya dhambi kwa ajili yake mwenyewe.+  Kisha wanawe wakamletea damu,+ naye akachovya kidole chake katika damu hiyo na kupaka pembe za madhabahu, na damu iliyobaki akaimwaga kwenye msingi wa madhabahu.+ 10  Akateketeza mafuta na figo na mafuta yaliyo juu ya ini kutoka katika dhabihu ya dhambi ili vifuke moshi kwenye madhabahu, kama Yehova alivyomwamuru Musa.+ 11  Naye akateketeza nyama na ngozi nje ya kambi.+ 12  Kisha Haruni akamchinja mnyama wa dhabihu ya kuteketezwa na wanawe wakampa damu, naye akainyunyiza pande zote za madhabahu.+ 13  Wakampa vipande vya mnyama wa dhabihu ya kuteketezwa pamoja na kichwa, naye akaviteketeza ili vifuke moshi kwenye madhabahu. 14  Pia, akaosha matumbo na miguu, akaviteketeza vitu hivyo kwenye madhabahu juu ya dhabihu ya kuteketezwa ili vifuke moshi. 15  Kisha akatoa dhabihu kwa ajili ya watu; akamchukua yule mbuzi wa dhabihu ya dhambi aliyepaswa kutolewa kwa ajili ya watu, akamchinja na kutoa dhabihu ya dhambi kama alivyofanya kwa yule wa kwanza. 16  Akatoa dhabihu ya kuteketezwa akifuata utaratibu wa kawaida.+ 17  Kisha akatoa toleo la nafaka;+ akachukua mkono mmoja wa toleo hilo na kuliteketeza ili lifuke moshi kwenye madhabahu pamoja na dhabihu ya kuteketezwa ya asubuhi.+ 18  Baada ya hayo Haruni akamchinja yule ng’ombe dume na kondoo dume wa dhabihu ya ushirika aliyepaswa kutolewa kwa ajili ya watu. Kisha wanawe wakampa damu, akainyunyiza pande zote za madhabahu.+ 19  Lakini vipande vyenye mafuta vya ng’ombe dume,+ mkia wenye mafuta wa kondoo dume, mafuta yaliyofunika matumbo, na figo, na mafuta yaliyokuwa juu ya ini,+ 20  waliviweka vipande hivyo vyote vyenye mafuta juu ya vidari, kisha akaviteketeza vipande hivyo ili vifuke moshi kwenye madhabahu.+ 21  Hata hivyo, Haruni akatikisa vidari na mguu wa kulia kwenda mbele na nyuma kuwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova, kama Musa alivyoamuru.+ 22  Kisha Haruni akainua mikono yake kuelekea watu, akawabariki,+ naye akashuka chini baada ya kutoa dhabihu ya dhambi na dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu za ushirika. 23  Mwishowe Musa na Haruni wakaingia katika hema la mkutano, kisha wakatoka nje na kuwabariki watu.+ Ndipo watu wote wakauona utukufu wa Yehova,+ 24  na moto ukashuka kutoka kwa Yehova+ na kuanza kuteketeza ile dhabihu ya kuteketezwa na vile vipande vyenye mafuta vilivyokuwa kwenye madhabahu. Watu wote walipoona hilo, wakaanza kupaza sauti na kuanguka kifudifudi.+

Maelezo ya Chini