Kulingana na Marko 10:1-52

  • Ndoa na talaka (1-12)

  • Yesu awabariki watoto (13-16)

  • Swali la mwanamume tajiri (17-25)

  • Kujidhabihu kwa ajili ya Ufalme (26-31)

  • Kifo cha Yesu chatabiriwa tena (32-34)

  • Ombi la Yakobo na Yohana (35-45)

    • Yesu fidia kwa ajili ya wengi (45)

  • Bartimayo aliyekuwa kipofu aponywa (46-52)

10  Alipotoka hapo akaenda kwenye mipaka* ya Yudea, ng’ambo ya Yordani, na umati ukakusanyika tena karibu naye. Kama kawaida yake, akaanza tena kuwafundisha.+  Mafarisayo wakaja, wakikusudia kumjaribu, wakamuuliza kama ni halali kwa mwanamume kumtaliki mke wake.+  Akawajibu: “Musa aliwapa amri gani?”  Wakasema: “Musa aliruhusu kumwandikia cheti cha kumfukuza na kumtaliki.”+  Lakini Yesu akawaambia: “Aliwaandikia amri hiyo+ kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu.+  Hata hivyo, tangu mwanzo wa uumbaji ‘Aliwaumba mwanamume na mwanamke.+  Kwa sababu hiyo, mwanamume atamwacha baba yake na mama yake,+  na hao wawili watakuwa mwili mmoja,’+ basi wao si wawili tena, bali mwili mmoja.  Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha, mtu yeyote asikitenganishe.”+ 10  Walipoingia tena ndani ya nyumba wanafunzi wakaanza kumuuliza kuhusu jambo hilo. 11  Akawaambia: “Yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine anafanya uzinzi+ dhidi yake, 12  na ikiwa mwanamke baada ya kumtaliki mume wake anaolewa na mwingine, anafanya uzinzi.”+ 13  Watu wakaanza kumletea watoto wadogo ili awaguse, lakini wanafunzi wakawakemea.+ 14  Alipoona hivyo, Yesu akakasirika na kuwaambia: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.+ 15  Kwa kweli ninawaambia, yeyote asiyeupokea Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hataingia kamwe ndani yake.”+ 16  Akawachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.+ 17  Alipokuwa akiondoka, mwanamume fulani akamkimbilia, akapiga magoti mbele yake na kumuuliza: “Mwalimu Mwema, ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 18  Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna aliye mwema, isipokuwa mmoja, Mungu.+ 19  Unazijua amri hizi: ‘Usiue,+ usifanye uzinzi,+ usiibe,+ usitoe ushahidi wa uwongo,+ usipunje,+ mheshimu baba yako na mama yako.’”+ 20  Mtu huyo akamwambia: “Mwalimu, nimeyashika mambo hayo yote tangu nilipokuwa kijana.” 21  Yesu akamtazama, akampenda na kumwambia: “Bado unahitaji kufanya jambo moja: Nenda ukauze vitu ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 22  Lakini akasikitishwa na jibu hilo, akaenda zake akiwa na huzuni, kwa maana alikuwa na mali nyingi.+ 23  Yesu akatazama huku na huku na kuwaambia wanafunzi wake: “Itakuwa vigumu sana kwa wale walio na pesa kuingia katika Ufalme wa Mungu!”+ 24  Lakini wanafunzi wakashangazwa na maneno yake. Naye Yesu akawaambia: “Wanangu, ni vigumu sana kuingia katika Ufalme wa Mungu! 25  Ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”+ 26  Wakazidi kushangaa wakamwambia:* “Ni nani anayeweza kuokolewa?”+ 27  Akawatazama moja kwa moja na kusema: “Kwa wanadamu haiwezekani, lakini sivyo ilivyo kwa Mungu, kwa maana mambo yote yanawezekana kwa Mungu.”+ 28  Petro akaanza kumwambia: “Tazama! Tumeacha kila kitu na kukufuata.”+ 29  Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia, hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema+ 30  ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso+—na katika mfumo wa mambo* unaokuja, uzima wa milele. 31  Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wa mwisho watakuwa wa kwanza.”+ 32  Sasa walikuwa barabarani wakipanda kwenda Yerusalemu, Yesu alikuwa akiwatangulia, nao walikuwa wameshangaa, lakini wale waliofuata wakaanza kuogopa. Akawapeleka kando tena wale 12 na kuanza kuwaambia mambo yaliyokuwa karibu kumpata:+ 33  “Tazama! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi. Nao watamhukumia kifo na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa, 34  nao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga mijeledi na kumuua, lakini baada ya siku tatu atafufuka.”+ 35  Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo,+ wakaenda na kumwambia: “Mwalimu, tunataka utufanyie chochote tutakachokuomba.”+ 36  Akawauliza: “Mnataka niwafanyie nini?” 37  Wakamwambia: “Turuhusu tuketi, mmoja upande wako wa kuume na mwingine upande wako wa kushoto, katika utukufu wako.”+ 38  Lakini Yesu akawaambia: “Hamjui kile mnachoomba. Je, mnaweza kunywa kikombe ambacho ninakunywa au kubatizwa kwa ubatizo ninaobatizwa?”+ 39  Wakamwambia: “Tunaweza.” Ndipo Yesu akawaambia: “Kikombe ninachokunywa mtakunywa, na ubatizo ninaobatizwa mtabatizwa.+ 40  Hata hivyo, kuketi upande wangu wa kuume au wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao wametayarishiwa.” 41  Wale wengine kumi waliposikia jambo hilo, wakawakasirikia Yakobo na Yohana.+ 42  Lakini Yesu akawaita akawaambia: “Mnajua kwamba wale wanaotawala* mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu wao hutumia mamlaka juu yao.+ 43  Haipaswi kuwa hivyo kati yenu; lakini yeyote anayetaka kuwa mkubwa kati yenu lazima awe mhudumu wenu,+ 44  na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kati yenu lazima awe mtumwa wa wote. 45  Kwa maana hata Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu+ na kutoa uhai wake uwe* fidia badala ya wengi.”+ 46  Kisha wakafika Yeriko. Lakini yeye na wanafunzi wake na umati mkubwa walipokuwa wakitoka Yeriko, Bartimayo (mwana wa Timayo), kipofu aliyekuwa akiombaomba, alikuwa ameketi kando ya barabara.+ 47  Aliposikia kwamba ni Yesu Mnazareti, akaanza kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi,+ Yesu, nihurumie!”*+ 48  Ndipo wengi wakaanza kumkemea, wakimwambia anyamaze, lakini akazidi kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi, nihurumie!”* 49  Basi Yesu akasimama na kusema: “Mwiteni.” Nao wakamwita yule kipofu, wakamwambia: “Jipe moyo! Simama; anakuita.” 50  Akatupa vazi lake la nje, akasimama haraka na kumwendea Yesu. 51  Kisha Yesu akamwuliza: “Unataka nikufanyie nini?” Yule kipofu akamwambia: “Raboni,* naomba niweze kuona tena.” 52  Yesu akamwambia: “Nenda, imani yako imekuponya.”+ Na mara moja akaanza kuona,+ naye akaanza kumfuata barabarani.

Maelezo ya Chini

Au “karibu na mipaka.”
Au labda, “wakaambiana.”
Angalia Kamusi.
Au “wanaoonwa kuwa watawala wa.”
Au “nafsi yake iwe.”
Au “nionyeshe rehema!”
Au “nionyeshe rehema!”
Maana yake “Mwalimu.”