Kulingana na Marko 15:1-47

  • Yesu mbele ya Pilato (1-15)

  • Adhihakiwa hadharani (16-20)

  • Atundikwa kwenye mti huko Golgotha (21-32)

  • Yesu afa (33-41)

  • Yesu azikwa (42-47)

15  Mara tu kulipopambazuka wakuu wa makuhani, wazee, na waandishi, yaani, Sanhedrini yote, wakashauriana pamoja na kumfunga Yesu, kisha wakampeleka na kumkabidhi kwa Pilato.+  Basi Pilato akamuuliza: “Je, wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?”+ Akamjibu: “Wewe mwenyewe umesema.”+  Lakini wakuu wa makuhani walikuwa wakimshtaki kwa mambo mengi.  Pilato akaanza kumuuliza tena: “Je, huna jibu lolote?+ Ona ni mashtaka mangapi wanayoleta dhidi yako.”+  Lakini Yesu hakujibu tena, hivi kwamba Pilato akashangaa.+  Basi, kila sherehe ya Pasaka, alikuwa na desturi ya kuwafungulia mfungwa ambaye waliomba.+  Wakati huo mtu aliyeitwa Baraba alikuwa amefungwa pamoja na wachochezi ambao katika uchochezi wao walikuwa wameua.  Basi umati ukaja na kuanza kumwomba Pilato awafanyie kama ilivyokuwa desturi yake.  Akawauliza: “Je, mnataka niwafungulie Mfalme wa Wayahudi?”+ 10  Kwa maana Pilato alijua kwamba wakuu wa makuhani walikuwa wamemkabidhi Yesu kwake kwa sababu ya wivu.+ 11  Lakini wakuu wa makuhani wakauchochea umati umwombe awafungulie Baraba badala yake.+ 12  Pilato akawauliza tena: “Basi, nifanye nini na mtu huyu mnayemwita Mfalme wa Wayahudi?”+ 13  Kwa mara nyingine tena wakapaza sauti: “Atundikwe mtini!”*+ 14  Lakini Pilato akawaambia: “Kwa nini? Amefanya kosa gani?” Hata hivyo, wakaendelea kupaza sauti hata zaidi: “Atundikwe mtini!”*+ 15  Basi Pilato akitaka kuuridhisha umati, akawafungulia Baraba; akaagiza Yesu apigwe mijeledi,+ kisha akamtoa ili auawe kwenye mti.+ 16  Sasa wanajeshi wakampeleka kwenye ua, katika makao ya gavana, nao wakakusanya kikosi chote cha wanajeshi.+ 17  Wakamvika Yesu vazi la zambarau, wakasokota taji la miiba na kumvisha; 18  nao wakaanza kumwambia kwa sauti kubwa: “Salamu,* ewe Mfalme wa Wayahudi!”+ 19  Pia, walikuwa wakimpiga kichwani kwa utete na kumtemea mate, nao wakapiga magoti na kumsujudia.* 20  Mwishowe, baada ya kumdhihaki, wakamvua lile vazi la zambarau na kumvisha mavazi yake ya nje. Kisha wakampeleka ili kumtundika mtini.+ 21  Pia, wakamlazimisha mpita njia afanye utumishi, mtu fulani aitwaye Simoni wa Kirene, baba ya Aleksanda na Rufo, aliyekuwa akitoka mashambani, aubebe mti wa mateso* wa Yesu.+ 22  Basi wakampeleka mahali panapoitwa Golgotha, neno ambalo linapotafsiriwa linamaanisha, “Mahali pa Fuvu la Kichwa.”+ 23  Hapa wakajaribu kumpa divai iliyotiwa kileo cha manemane,+ lakini hakuinywa. 24  Nao wakamtundika kwenye mti na wakagawana mavazi yake kwa kuyapigia kura ili kuamua ni nini ambacho kila mtu angechukua.+ 25  Ilikuwa saa tatu,* nao wakamtundika kwenye mti. 26  Na maandishi ya mashtaka dhidi yake yalikuwa yameandikwa: “Mfalme wa Wayahudi.”+ 27  Pia, wakawatundika wezi wawili kwenye mti kando yake, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.+ 28 * —— 29  Wale waliokuwa wakipita hapo wakamtukana huku wakitikisa vichwa vyao+ wakisema: “Aha! Wewe uliyetaka kuliangusha chini hekalu na kulijenga kwa siku tatu,+ 30  jiokoe mwenyewe kwa kushuka kutoka kwenye mti wa mateso.”* 31  Vivyo hivyo, wakuu wa makuhani na waandishi walikuwa wakimdhihaki kati yao wakisema: “Aliwaokoa wengine lakini hawezi kujiokoa mwenyewe!+ 32  Acheni Kristo, Mfalme wa Israeli, ashuke sasa kutoka kwenye mti wa mateso,* ili tuone na kuamini.”+ Hata wale waliotundikwa mtini kando yake walikuwa wakimshutumu.+ 33  Ilipofika saa sita* kukawa na giza katika nchi yote mpaka saa tisa.*+ 34  Na saa tisa Yesu akapaza sauti: “Eli, Eli, lama sabakthani?” maneno hayo yanapotafsiriwa yanamaanisha, “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?”+ 35  Na baadhi ya wale waliokuwa wamesimama karibu walipomsikia wakaanza kusema: “Sikia! Anamwita Eliya.” 36  Kisha mtu fulani akakimbia, akalowesha sifongo katika divai kali, akaiweka kwenye utete, akampa anywe,+ akisema: “Mwacheni! Acheni tuone kama Eliya atakuja kumshusha.” 37  Lakini Yesu akalia kwa sauti kubwa, akakata pumzi.*+ 38  Na pazia la patakatifu+ likapasuka vipande viwili kuanzia juu mpaka chini.+ 39  Sasa ofisa wa jeshi aliyekuwa amesimama kando yake akimtazama, alipoona amekufa katika hali hizo, akasema: “Hakika mtu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”+ 40  Kulikuwa pia na wanawake wakitazama kwa mbali, miongoni mwao kulikuwa na Maria Magdalene, Salome, na Maria mama ya Yakobo Mdogo na Yose,+ 41  walikuwa wakifuatana na Yesu na kumhudumia+ alipokuwa Galilaya, pia wanawake wengine wengi waliokuwa wamekuja Yerusalemu pamoja naye. 42  Sasa kwa kuwa ilikuwa jioni, siku ya Matayarisho, yaani, siku moja kabla ya Sabato, 43  akaja Yosefu wa Arimathea, mshiriki wa Baraza aliyeheshimiwa, ambaye pia alikuwa akiungojea Ufalme wa Mungu. Akajipa moyo na kwenda kwa Pilato, akaomba apewe mwili wa Yesu.+ 44  Lakini Pilato akataka kujua kama tayari alikuwa amekufa, akamwita yule ofisa wa jeshi, akamuuliza ikiwa Yesu alikuwa amekufa. 45  Baada ya kuhakikisha kutoka kwa huyo ofisa wa jeshi, akamruhusu Yosefu auchukue mwili huo. 46  Baada ya kununua kitani bora, akamshusha na kumfunga kwa kile kitani bora na kumlaza katika kaburi*+ lililokuwa limechimbwa katika mwamba; kisha akaviringisha jiwe kwenye mwingilio wa lile kaburi.+ 47  Lakini Maria Magdalene na Maria mama ya Yose wakaendelea kutazama mahali alipokuwa amelazwa.+

Maelezo ya Chini

Au “Auawe kwenye mti!”
Au “Auawe kwenye mti!”
Au “Usifiwe.”
Au “kumwinamia.”
Angalia Kamusi.
Yaani, karibu saa tatu asubuhi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Au “akapumua mara ya mwisho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”