Kulingana na Marko 2:1-28

  • Yesu amponya mtu aliyepooza (1-12)

  • Yesu amwita Lawi (13-17)

  • Swali kuhusu kufunga (18-22)

  • Yesu, ‘Bwana wa Sabato’ (23-28)

2  Hata hivyo, baada ya siku kadhaa Yesu akarudi tena Kapernaumu na watu wakasikia kwamba yuko nyumbani.+  Basi watu wengi sana wakaja hivi kwamba hapakuwa na nafasi tena, hata mlangoni, naye akaanza kuwahubiria.+  Wakamletea mtu aliyepooza, akiwa amebebwa na watu wanne.+  Lakini kwa sababu ya umati, hawakuweza kumleta moja kwa moja kwa Yesu, basi baada ya kutoboa sehemu ya paa lililokuwa juu ya Yesu, wakamteremsha yule mtu aliyepooza, akiwa amelala juu ya kitanda.*  Yesu alipoona imani yao,+ akamwambia yule mtu aliyepooza: “Mwanangu, umesamehewa dhambi zako.”+  Sasa baadhi ya waandishi waliokuwa wameketi hapo wakaanza kuwaza mioyoni mwao:+  “Kwa nini mtu huyu anasema hivyo? Anakufuru. Ni nani anayeweza kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”+  Lakini mara moja Yesu akatambua rohoni mwake kwamba walikuwa wakiwaza hivyo, basi akawaambia: “Kwa nini mnawaza mambo hayo katika mioyo yenu?+  Ni jambo gani rahisi zaidi, kumwambia mtu huyu aliyepooza, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama, uchukue kitanda chako utembee’? 10  Lakini ili mjue kwamba Mwana wa binadamu+ ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani—”+ akamwambia yule mtu aliyepooza: 11  “Ninakuambia, Simama, chukua kitanda chako, uende nyumbani.” 12  Ndipo akasimama, na mara moja akachukua kitanda chake akatembea mbele yao wote na kwenda nje. Basi, wote wakashangaa, na kumtukuza Mungu wakisema: “Hatujawahi kamwe kuona jambo kama hilo.”+ 13  Akaenda tena kando ya bahari; na umati ukamjia, naye akaanza kuwafundisha. 14  Alipokuwa akipita, akamwona Lawi mwana wa Alfayo akiwa ameketi kwenye ofisi ya kodi, akamwambia: “Njoo uwe mfuasi wangu.” Mara moja akasimama na kumfuata.+ 15  Baadaye alipokuwa akila* katika nyumba ya Lawi, wakusanya kodi wengi na watenda dhambi walikuwa wakila* pamoja na Yesu na wanafunzi wake, kwa maana wengi wao walikuwa wakimfuata.+ 16  Lakini waandishi wa Mafarisayo, walipoona akila na watenda dhambi na wakusanya kodi, wakaanza kuwauliza wanafunzi wake: “Je, yeye hula pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi?” 17  Aliposikia hilo, Yesu akawaambia: “Watu wenye nguvu hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji. Sikuja kuwaita waadilifu, bali watenda dhambi.”+ 18  Wanafunzi wa Yohana na Mafarisayo walikuwa na zoea la kufunga. Basi wakaja na kumuuliza Yesu: “Kwa nini wanafunzi wa Yohana na wanafunzi wa Mafarisayo hufunga, lakini wanafunzi wako hawafungi?”+ 19  Yesu akawajibu: “Rafiki za bwana harusi+ hawahitaji kufunga wanapokuwa naye, sivyo? Bwana harusi akiwa pamoja nao hawawezi kufunga. 20  Lakini siku zitakuja ambapo bwana harusi ataondolewa kwao,+ ndipo watakapofunga siku hiyo. 21  Hakuna mtu anayeshona kiraka cha kitambaa kipya juu ya vazi la nje la zamani. Akifanya hivyo, kitambaa kipya kitatoka kwenye vazi la zamani, nalo litararuka vibaya zaidi.+ 22  Pia, hakuna mtu anayeweka divai mpya katika viriba vya divai vilivyochakaa. Akifanya hivyo, divai itapasua ngozi ya viriba naye atapoteza divai pamoja na ngozi. Lakini divai mpya huwekwa katika viriba vipya vya divai.” 23  Alipokuwa akipita kwenye mashamba ya nafaka siku ya Sabato, wanafunzi wake wakaanza kukata masuke ya nafaka huku wakitembea.+ 24  Hivyo, Mafarisayo wakamwambia: “Tazama sasa! Kwa nini wanafanya jambo lisilo halali siku ya Sabato?” 25  Lakini akawaambia: “Je, hamjasoma alilofanya Daudi, wakati alipokuwa na uhitaji na yeye na wanaume waliokuwa pamoja naye walipohisi njaa?+ 26  Jinsi katika simulizi kuhusu mkuu wa makuhani Abiathari,+ Daudi alivyoingia katika nyumba ya Mungu na kula mikate ya toleo,* ambayo si halali kwa mtu yeyote kula isipokuwa makuhani,+ naye akawapa pia watu waliokuwa pamoja naye?” 27  Kisha akawaambia: “Sabato iliwekwa kwa ajili ya mwanadamu,+ bali si mwanadamu kwa ajili ya Sabato. 28  Basi, Mwana wa binadamu pia ndiye Bwana wa Sabato.”+

Maelezo ya Chini

Au “machela.”
Au “walikuwa wameketi mezani.”
Au “alipokuwa ameketi mezani.”
Au “mikate iliyowekwa mbele za Mungu.”