Kulingana na Marko 3:1-35

  • Mwanamume mwenye mkono uliopooza aponywa (1-6)

  • Umati mkubwa kando ya bahari (7-12)

  • Mitume 12 (13-19)

  • Kukufuru roho takatifu (20-30)

  • Mama na ndugu za Yesu (31-35)

3  Yesu akaingia tena ndani ya sinagogi, na palikuwa na mtu aliyepooza mkono.+  Basi walikuwa wakimwangalia sana waone kama atamponya mtu huyo siku ya Sabato, ili wamshtaki.  Akamwambia yule mtu aliyepooza mkono: “Simama uje hapa katikati.”  Kisha akawauliza: “Je, ni halali kufanya mema au kufanya mabaya siku ya Sabato, kuokoa uhai* au kuua?”+ Lakini wakanyamaza.  Akawatazama kwa hasira na kuhuzunika sana kwa sababu mioyo yao ilikuwa migumu,+ akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha mkono wake, nao ukapona.  Ndipo Mafarisayo wakaenda nje na mara moja wakafanya mkutano pamoja na wafuasi wa chama cha Herode+ ili wamuue Yesu.  Lakini Yesu na wanafunzi wake wakaelekea baharini, na umati mkubwa kutoka Galilaya na Yudea ukamfuata.+  Hata kutoka Yerusalemu, Idumea, ng’ambo ya Yordani, na maeneo ya Tiro na Sidoni, umati mkubwa ukamjia uliposikia kuhusu mambo mengi aliyokuwa akifanya.  Naye akawaambia wanafunzi wake wamletee mashua ndogo ili umati usimsonge. 10  Kwa sababu aliwaponya watu wengi, wote waliokuwa wagonjwa sana walikuwa wakimkaribia ili wamguse.+ 11  Hata roho waovu,+ kila mara walipomwona, walianguka mbele yake na kupaza sauti wakisema: “Wewe ndiye Mwana wa Mungu.”+ 12  Lakini mara nyingi aliwaagiza kwa kusisitiza wasimtangaze.+ 13  Akapanda mlimani na kuwaita wale aliowataka,+ nao wakaja.+ 14  Akaanzisha* kikundi cha wanaume 12, ambao pia aliwaita mitume, nao wangefuatana naye, na angewatuma kuhubiri 15  na wangekuwa na mamlaka ya kufukuza roho waovu.+ 16  Kile kikundi cha wanaume 12+ alichoanzisha* kilikuwa na Simoni, ambaye pia alimwita Petro,+ 17  Yakobo na Yohana wana wa Zebedayo (ambao pia aliwaita Boanerge, jina linalomaanisha “Wana wa Ngurumo”),+ 18  Andrea, Filipo, Bartholomayo, Mathayo, Tomasi, Yakobo mwana wa Alfayo, Thadayo, Simoni Mkananayo,* 19  na Yuda Iskariote, ambaye baadaye alimsaliti. Kisha Yesu akaingia ndani ya nyumba, 20  na umati ukakusanyika tena, hivi kwamba hata hawakupata nafasi ya kula. 21  Lakini watu wake wa ukoo waliposikia hilo, wakaenda kumkamata, kwa maana walikuwa wakisema: “Amerukwa na akili.”+ 22  Pia, waandishi walioshuka kutoka Yerusalemu walikuwa wakisema: “Ana Beelzebuli,* naye anawafukuza roho waovu kwa nguvu za mtawala wa roho waovu.”+ 23  Kisha akawaita na kuzungumza nao kwa mifano: “Shetani anawezaje kumfukuza Shetani? 24  Ufalme ukigawanyika dhidi yake wenyewe, hauwezi kusimama;+ 25  na nyumba ikigawanyika dhidi yake yenyewe, haiwezi kusimama. 26  Pia, ikiwa Shetani anajipinga mwenyewe na amegawanyika, hawezi kusimama, bali ataangamia. 27  Kwa kweli, hakuna yeyote anayeweza kuingia ndani ya nyumba ya mtu mwenye nguvu na kuiba mali zake isipokuwa kwanza amfunge mtu huyo. Hapo ndipo atakapoweza kuipora nyumba yake. 28  Kwa kweli ninawaambia kwamba wanadamu watasamehewa mambo yote, hata ziwe dhambi gani au maneno ya kukufuru wanayosema. 29  Lakini yeyote anayekufuru roho takatifu hatasamehewa milele,+ bali atakuwa na hatia ya dhambi ya milele.”+ 30  Alisema hivyo kwa sababu walikuwa wakisema: “Ana roho mwovu.”+ 31  Mama yake na ndugu zake+ wakaja na kusimama nje, wakamtuma mtu akamwite.+ 32  Kwa kuwa umati ulikuwa umeketi kumzunguka, wakamwambia: “Tazama! Mama yako na ndugu zako wako nje wanakuita.”+ 33  Lakini akawauliza: “Mama yangu na ndugu zangu ni nani?” 34  Akawatazama watu walioketi kumzunguka, akasema: “Tazama, mama yangu na ndugu zangu!+ 35  Yeyote anayefanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, dada yangu, na mama yangu.”+

Maelezo ya Chini

Au “nafsi.”
Au “Akachagua.”
Au “alichochagua.”
Au “mwenye bidii.”
Jina lingine la Shetani.