Kulingana na Marko 5:1-43

  • Yesu awaruhusu roho waovu waingie ndani ya nguruwe (1-20)

  • Binti ya Yairo; mwanamke agusa vazi la nje la Yesu (21-43)

5  Basi, wakafika ng’ambo ya bahari na kuingia katika eneo la Wagerasene.+  Mara tu Yesu alipotoka kwenye mashua akakutana na mtu mwenye roho mwovu akitoka makaburini.*  Alikuwa akikaa makaburini, na kufikia wakati huo hakuna mtu yeyote aliyeweza kumfunga kabisa hata kwa mnyororo.  Alikuwa amefungwa mara nyingi kwa pingu na minyororo, lakini aliikata minyororo na kuzivunja pingu; na hakuna mtu aliyeweza kumzuia.  Sikuzote, usiku na mchana alikuwa akipaza sauti makaburini na milimani na kujikatakata kwa mawe.  Lakini alipomwona Yesu kwa mbali, alimkimbilia na kumwinamia.+  Kisha akapaza sauti na kusema: “Kwa nini unanisumbua, Yesu, Mwana wa Mungu Aliye Juu Zaidi? Ninakuapisha kwa Mungu usinitese.”+  Kwa maana Yesu alikuwa akimwambia: “Mtoke mtu huyu, wewe roho mwovu.”+  Lakini Yesu akamuuliza: “Unaitwa nani?” Naye akamwambia: “Jina langu ni Kikosi, kwa sababu tuko wengi.” 10  Naye akamsihi sana Yesu asiwafukuze roho hao kutoka katika nchi hiyo.+ 11  Sasa kulikuwa na nguruwe wengi+ wakila hapo mlimani.+ 12  Basi hao roho waovu wakamsihi: “Turuhusu tuingie ndani ya wale nguruwe.” 13  Naye akawaruhusu. Ndipo wale roho waovu wakatoka na kuingia ndani ya wale nguruwe, kisha lile kundi likatimua mbio, likaruka poromoko* na kuzama baharini. Walikuwa karibu 2,000, nao wakafa maji baharini. 14  Lakini wachungaji wa nguruwe hao wakakimbia wakapeleka habari jijini na mashambani, watu wakaja kuona kilichotukia.+ 15  Basi wakamjia Yesu, wakamwona yule mtu aliyekuwa na roho waovu, ambaye mwanzoni alikuwa na kile kikosi, akiwa ameketi, amevaa nguo, na akiwa na akili timamu, nao wakaogopa. 16  Pia, wale walioona tukio hilo wakawasimulia mambo yaliyompata mtu huyo aliyekuwa na roho waovu na kuhusu wale nguruwe. 17  Basi wakaanza kumsihi Yesu aondoke katika eneo lao.+ 18  Alipokuwa akipanda mashua, yule mtu aliyekuwa na roho waovu akaanza kumsihi aende pamoja naye.+ 19  Hata hivyo, hakumruhusu, bali alimwambia: “Nenda nyumbani kwa watu wako wa ukoo, ukawaambie mambo yote ambayo Yehova* amekufanyia na jinsi alivyokuonyesha rehema.” 20  Mtu huyo akaenda zake akaanza kutangaza katika Dekapoli* mambo yote ambayo Yesu alimfanyia, na watu wote wakashangaa. 21  Baada ya Yesu kuvuka tena ng’ambo ya bahari kwa mashua, umati mkubwa ukakusanyika karibu naye alipokuwa kando ya bahari.+ 22  Sasa mmoja wa maofisa wasimamizi wa sinagogi, aliyeitwa Yairo akaja, na alipomwona Yesu, akaanguka miguuni pake.*+ 23  Akamsihi mara nyingi, akisema: “Binti yangu mdogo ni mgonjwa sana.* Tafadhali njoo uweke mikono yako juu yake+ ili apone na kuishi.” 24  Ndipo Yesu akaenda pamoja naye, na umati mkubwa ulikuwa ukimfuata na kumsonga. 25  Sasa kuna mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu+ kwa miaka 12.+ 26  Alikuwa ameteseka sana* mikononi mwa madaktari wengi na alikuwa ametumia mali yake yote, na hakuwa amepona, badala yake hali yake ilizidi kuwa mbaya. 27  Aliposikia kumhusu Yesu, akapenya katika umati nyuma ya Yesu na kuligusa vazi lake la nje,+ 28  kwa maana alikuwa akisema: “Nikiyagusa tu mavazi yake ya nje, nitapona.”+ 29  Papo hapo mtiririko wake wa damu ukakoma, naye akahisi mwilini mwake kwamba alikuwa amepona ule ugonjwa mbaya. 30  Mara moja Yesu akahisi ndani yake kwamba nguvu+ zimemtoka, akaugeukia umati na kuuliza: “Ni nani aliyegusa mavazi yangu ya nje?”+ 31  Lakini wanafunzi wake wakamwambia: “Unaona jinsi umati unavyokusonga, na unauliza, ‘Ni nani aliyenigusa?’” 32  Hata hivyo, alikuwa akitazama ili aone mtu aliyekuwa amefanya hivyo. 33  Yule mwanamke akijua lililompata, akaja akitetemeka kwa hofu akaanguka chini mbele yake, akamwambia ukweli wote. 34  Yesu akamwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani,+ umepona ugonjwa wako mbaya.”+ 35  Alipokuwa bado anazungumza, watu fulani kutoka nyumbani kwa yule ofisa msimamizi wa sinagogi wakaja na kusema: “Binti yako amekufa! Kwa nini uendelee kumsumbua Mwalimu?”+ 36  Lakini Yesu akasikia maneno yao naye akamwambia yule ofisa msimamizi wa sinagogi: “Usiogope, uwe tu na imani.”*+ 37  Hakumruhusu mtu yeyote amfuate isipokuwa Petro, Yakobo, na Yohana ndugu ya Yakobo.+ 38  Wakafika kwenye nyumba ya yule ofisa msimamizi wa sinagogi, Yesu akaona mvurugo wa watu waliokuwa wakilia na kuomboleza kwa sauti kubwa.+ 39  Baada ya kuingia, akawaambia: “Kwa nini mnaomboleza na kuleta mvurugo? Mtoto hajafa bali amelala usingizi.”+ 40  Ndipo wakaanza kumcheka kwa dharau. Lakini baada ya kuwatoa wote nje, akamchukua baba na mama ya yule mtoto pamoja na wanafunzi wake, akaingia mahali alipokuwa huyo mtoto. 41  Kisha akaushika mkono wa msichana huyo na kumwambia: “Talitha kumi,” maneno ambayo yanapotafsiriwa, yanamaanisha: “Msichana mdogo, ninakuambia, ‘inuka!’”+ 42  Mara moja yule msichana akasimama akaanza kutembea. (Alikuwa na umri wa miaka 12.) Ndipo wakawa na shangwe kubwa sana. 43  Lakini akawaagiza tena na tena* wasimwambie mtu yeyote kuhusu jambo hilo,+ naye akawaambia wampe mtoto huyo chakula.

Maelezo ya Chini

Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “ukingo wenye mteremko mkali.”
Au “Eneo lenye Majiji Kumi.”
Au “akapiga magoti mbele yake.”
Au “anakaribia kufa.”
Au “alikuwa ameumizwa sana.”
Au “onyesha tu imani.”
Au “akawaamuru kwa uthabiti.”