Kulingana na Marko 8:1-38

  • Yesu alisha wanaume 4,000 (1-9)

  • Waomba ishara (10-13)

  • Chachu ya Mafarisayo na ya Herode (14-21)

  • Mwanamume kipofu aponywa huko Bethsaida (22-26)

  • Petro amtambulisha Kristo (27-30)

  • Kifo cha Yesu chatabiriwa (31-33)

  • Wanafunzi wa kweli (34-38)

8  Siku hizo umati mkubwa ukakusanyika tena, na hawakuwa na chakula. Basi, akawaita wanafunzi na kuwaambia:  “Ninausikitikia umati,+ kwa sababu tayari wamekaa pamoja nami siku tatu nao hawana chakula.+  Nikiwaacha waende nyumbani wakiwa na njaa,* watazimia njiani, na baadhi yao wametoka mbali.”  Lakini wanafunzi wake wakamjibu: “Tutapata wapi mikate ya kuwatosha watu hawa mahali hapa pasipo na watu?”  Ndipo akawauliza: “Mna mikate mingapi?” Wakajibu: “Saba.”+  Naye akauagiza umati uketi chini. Kisha akachukua ile mikate saba, akatoa shukrani, akaimega, na kuanza kuwapa wanafunzi wake waigawe, nao wakaugawia umati.+  Walikuwa pia na samaki wachache wadogo, naye akawabariki, kisha akawaambia wawagawe hao pia.  Basi wakala wakashiba, kisha wakakusanya vipande vilivyobaki wakajaza vikapu saba vikubwa.+  Kulikuwa na wanaume 4,000 hivi. Kisha Yesu akawaaga. 10  Mara moja akapanda mashua pamoja na wanafunzi wake akaenda eneo la Dalmanutha.+ 11  Akiwa huko Mafarisayo wakaja na kuanza kubishana naye, wakimtaka afanye ishara kutoka mbinguni, ili wamjaribu.+ 12  Kwa hiyo akahuzunika sana rohoni na kusema: “Kwa nini kizazi hiki kinatafuta ishara?+ Kwa kweli nasema, kizazi hiki hakitapewa ishara yoyote.”+ 13  Ndipo akawaacha, akapanda mashua tena na kuvuka ng’ambo ya bahari. 14  Hata hivyo, walisahau kuchukua mikate na walikuwa na mkate mmoja tu katika mashua.+ 15  Naye akawaonya waziwazi akisema: “Endeleeni kuwa macho; jihadharini na chachu* ya Mafarisayo na ya Herode.”+ 16  Basi wakaanza kubishana kati yao kwa sababu hawakuwa na mikate. 17  Yesu alipojua hilo, akawaambia: “Kwa nini mnabishana kuhusu kutokuwa na mikate? Je, bado hamjafahamu wala kuelewa? Je, bado mioyo yenu ni mizito isiweze kuelewa? 18  ‘Ingawa mna macho, kwa nini hamwoni; na ingawa mna masikio, kwa nini hamsikii?’ Je, hamkumbuki 19  nilipoimega ile mikate mitano+ kwa ajili ya wale wanaume 5,000, mlikusanya vipande vilivyobaki mkajaza vikapu vingapi?” Wakamwambia: “Kumi na viwili.”+ 20  “Nilipoimega ile mikate saba kwa ajili ya wale wanaume 4,000, mlikusanya vipande vilivyobaki mkajaza vikapu vikubwa vingapi?” Wakamwambia: “Saba.”+ 21  Ndipo akawauliza: “Je, bado hamjaelewa?” 22  Sasa wakafika Bethsaida. Watu wakamletea mwanamume aliye kipofu, wakamsihi amguse.+ 23  Yesu akamshika mkono yule kipofu, akampeleka nje ya kijiji. Kisha akamtemea mate machoni,+ akaweka mikono juu yake na kumuuliza: “Je, unaona kitu chochote?” 24  Yule mtu akatazama juu na kusema: “Ninaona watu, lakini wanaonekana kama miti inayotembea.” 25  Akaweka tena mikono yake juu ya macho ya mtu huyo, naye akaona vizuri. Akawa tena na uwezo wa kuona, naye alikuwa akiona kila kitu waziwazi. 26  Basi akamwacha aende nyumbani, na kumwambia: “Usiingie kijijini.” 27  Yesu na wanafunzi wake wakaelekea kwenye vijiji vya Kaisaria Filipi, na wakiwa njiani, Yesu akaanza kuwauliza wanafunzi wake: “Watu wanasema mimi ni nani?”+ 28  Wakamjibu: “Yohana Mbatizaji,+ lakini wengine Eliya,+ na bado wengine mmoja wa manabii.” 29  Naye akawauliza: “Hata hivyo, ninyi mnasema mimi ni nani?” Petro akajibu: “Wewe ndiye Kristo.”+ 30  Ndipo akawaamuru wasimwambie mtu yeyote kumhusu.+ 31  Pia, akaanza kuwafundisha kwamba Mwana wa binadamu lazima apatwe na mateso mengi na kukataliwa na wazee, wakuu wa makuhani, na waandishi, kisha atauawa,+ na baada ya siku tatu atafufuliwa.+ 32  Kwa kweli, alisema mambo hayo waziwazi. Lakini Petro akampeleka kando na kuanza kumkemea.+ 33  Yesu akageuka na kuwatazama wanafunzi wake, akamkemea Petro, akisema: “Nenda nyuma yangu, Shetani! kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.”+ 34  Sasa akauita umati na wanafunzi wake, akawaambia: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso* na aendelee kunifuata.+ 35  Kwa kuwa yeyote anayetaka kuokoa uhai wake ataupoteza,* lakini yeyote anayeupoteza uhai wake* kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema atauokoa.+ 36  Kwa kweli, mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote kisha apoteze uhai wake?*+ 37  Kwa kweli, mtu anaweza kutoa nini ili abadilishane na uhai wake?*+ 38  Kwa maana yeyote atakayenionea aibu mimi na maneno yangu katika kizazi hiki chenye uzinzi * na chenye dhambi, Mwana wa binadamu atamwonea aibu pia+ atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.”+

Maelezo ya Chini

Au “wakiwa wamefunga.”
Au “hamira.”
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake ataipoteza.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Au “kisicho na uaminifu.”