Matendo ya Mitume 1:1-26

  • Ujumbe kwa Theofilo (1-5)

  • Mashahidi mpaka sehemu ya mbali ya dunia (6-8)

  • Yesu apaa mbinguni (9-11)

  • Wanafunzi wakusanyika kwa umoja (12-14)

  • Mathia achaguliwa kuchukua mahali pa Yuda (15-26)

1  Lile simulizi la kwanza, ewe Theofilo, niliandika kuhusu mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha+  mpaka siku aliyochukuliwa kwenda juu,+ baada ya kuwapa mitume aliowachagua maagizo kupitia roho takatifu.+  Baada ya kuteseka, alijionyesha kwao akiwa hai kupitia uthibitisho mwingi wenye kusadikisha.+ Walimwona kwa siku 40, naye alizungumza nao kuhusu Ufalme wa Mungu.+  Alipokuwa akikutana nao aliwaagiza hivi: “Msiondoke Yerusalemu,+ bali endeleeni kusubiri kile ambacho Baba ameahidi,+ ambacho mlinisikia nikisema kukihusu;  kwa maana Yohana, kwa kweli, alibatiza kwa maji, lakini ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu+ baada ya siku chache.”  Basi, walipokusanyika, wakamuuliza: “Bwana, je, unaurudisha ufalme kwa Israeli wakati huu?”+  Akawaambia: “Si juu yenu kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.+  Lakini roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu,+ nanyi mtakuwa mashahidi+ wangu katika Yerusalemu,+ katika Yudea yote na Samaria,+ na mpaka sehemu ya mbali zaidi* ya dunia.”+  Baada ya kusema mambo hayo, wakiwa wanatazama, akainuliwa juu na wingu likamfunika nao hawakumwona tena.+ 10  Nao walipokuwa wakitazama angani akiwa anaenda, ghafla wanaume wawili wenye mavazi meupe+ wakasimama kando yao 11  na kusema: “Wanaume wa Galilaya, kwa nini mnasimama mkitazama angani? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda angani atakuja vivyo hivyo kama vile ambavyo mmemwona akienda angani.” 12  Kisha wakarudi Yerusalemu+ kutoka kwenye Mlima wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, umbali wa safari ya siku ya sabato. 13  Walipofika, walienda kwenye chumba cha juu, walipokuwa wakikaa. Walikuwa Petro, Yohana, Yakobo, Andrea, Filipo, Tomasi, Bartholomayo, Mathayo, Yakobo mwana wa Alfayo, Simoni mwenye bidii, na Yuda mwana wa Yakobo.+ 14  Wote hawa walidumu katika sala kwa kusudi moja, wakiwa pamoja na wanawake+ fulani na Maria mama ya Yesu, pamoja na ndugu za Yesu.+ 15  Katika siku hizo Petro akasimama kati ya akina ndugu (kwa ujumla idadi ya* watu ilikuwa karibu 120) na kusema: 16  “Wanaume, akina ndugu, ilikuwa lazima andiko litimizwe, ambalo roho takatifu ilisema kinabii kupitia Daudi kumhusu Yuda,+ aliyewaongoza wale waliomkamata Yesu.+ 17  Kwa maana alihesabiwa miongoni mwetu+ naye alipata fungu katika huduma hii. 18  (Mtu huyo alinunua shamba kwa mshahara wa ukosefu wa uadilifu,+ akaanguka kichwa kwanza, mwili wake ukapasuka* na matumbo yake yote yakamwagika.+ 19  Wakaaji wote wa Yerusalemu wakajua jambo hilo, hivi kwamba shamba hilo likaitwa kwa lugha yao Akeldama, yaani, “Shamba la Damu.”) 20  Kwa maana imeandikwa katika kitabu cha Zaburi, ‘Makao yake yabaki ukiwa, na pasiwe na mkaaji yeyote humo,’+ na, ‘Mtu mwingine na achukue cheo chake cha uangalizi.’+ 21  Kwa hiyo inafaa kwamba mmoja wa wanaume walioandamana nasi wakati wote ambao Bwana Yesu alifanya kazi zake* miongoni mwetu, 22  kuanzia alipobatizwa na Yohana+ mpaka siku alipochukuliwa kutoka kwetu kwenda juu,+ mmoja wa wanaume hao anapaswa kuwa shahidi pamoja nasi kuhusu ufufuo wake.”+ 23  Kwa hiyo wakapendekeza watu wawili, Yosefu aliyeitwa pia Barsaba au Yusto, na Mathia. 24  Ndipo wakasali wakisema: “Wewe, Ee Yehova,* unayejua mioyo ya wote,+ onyesha ni nani kati ya watu hawa wawili ambaye umemchagua 25  achukue mahali pa huduma na utume huu, ambao Yuda aliuacha na kwenda mahali pake mwenyewe.”+ 26  Basi wakawapigia kura,+ na kura ikamwangukia Mathia, naye akahesabiwa* pamoja na wale mitume 11.

Maelezo ya Chini

Au “miisho.”
Au “umati wa.”
Au “akapasuka katikati.”
Au, “alipoingia na kutoka.”
Au “akajumlishwa,” yaani, akaonwa sawa na wale wengine 11.