Matendo ya Mitume 11:1-30

  • Petro atoa ripoti kwa mitume (1-18)

  • Barnaba na Sauli huko Antiokia ya Siria (19-26)

    • Wanafunzi waanza kuitwa Wakristo (26)

  • Agabo atabiri kuhusu njaa (27-30)

11  Sasa mitume na ndugu waliokuwa Yudea wakasikia kwamba watu wa mataifa pia walikuwa wamelikubali neno la Mungu.  Basi Petro alipopanda kwenda Yerusalemu, wale waliounga mkono kutahiriwa+ wakaanza kumkosoa,*  wakisema: “Uliingia ndani ya nyumba ya watu ambao hawajatahiriwa nawe ukala pamoja nao.”  Ndipo Petro akawafafanulia jambo hilo kwa kina, akisema:  “Nilipokuwa nikisali katika jiji la Yopa, niliona maono katika njozi, kitu fulani* kikishuka kama shuka kubwa la kitani, kikiteremshwa kutoka mbinguni kwa ncha zake nne, nacho kikaja moja kwa moja mpaka mahali nilipokuwa.+  Nilipotazama kwa makini ndani yake, nikaona wanyama wa dunia wenye miguu minne, wanyama wa mwituni, viumbe wanaotambaa, na ndege wa angani.  Pia nikasikia sauti ikiniambia: ‘Petro, simama, chinja ule!’  Lakini nikasema, ‘Hapana Bwana, kwa sababu kitu chochote najisi au kisicho safi hakijawahi kamwe kuingia kinywani mwangu.’  Mara ya pili, ile sauti kutoka mbinguni ikajibu: ‘Wewe acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.’ 10  Hilo likatokea mara ya tatu, na kila kitu kikavutwa juu kurudi mbinguni. 11  Wakati huohuo, wanaume watatu waliotumwa kwangu kutoka Kaisaria walikuwa wamesimama karibu na nyumba tuliyokuwa tukikaa.+ 12  Ndipo roho ikaniambia niende pamoja nao, bila kuwa na shaka hata kidogo. Lakini hawa ndugu sita pia walienda pamoja nami, nasi tukaingia ndani ya nyumba ya mwanamume huyo. 13  “Alitueleza jinsi alivyomwona malaika akiwa amesimama katika nyumba yake na kumwambia, ‘Watume watu waende Yopa wakamwite Simoni anayeitwa Petro,+ 14  naye atakuambia mambo yatayokusaidia wewe na watu wote wa nyumba yako mwokolewe.’ 15  Lakini nilipoanza kuzungumza, roho takatifu ikaja juu yao kama ilivyokuja juu yetu mwanzoni.+ 16  Ndipo nikakumbuka maneno aliyokuwa akisema Bwana: ‘Yohana alibatiza kwa maji,+ lakini ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu.’+ 17  Kwa hiyo, ikiwa Mungu aliwapa zawadi ileile ya bure kama alivyotupatia sisi ambao tumemwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani hata niweze kumzuia* Mungu?”+ 18  Waliposikia mambo hayo, wakaacha kupinga,* nao wakamtukuza Mungu wakisema: “Kwa hiyo basi, Mungu pia ameruhusu watu wa mataifa watubu ili wapate uzima.”+ 19  Sasa wale waliokuwa wametawanyika+ kwa sababu ya dhiki iliyotokea kuhusiana na Stefano, wakaenda mpaka Foinike, Kipro, na Antiokia, lakini walitangaza lile neno kwa Wayahudi tu.+ 20  Hata hivyo, wanaume fulani kati yao kutoka Kipro na Kirene walikuja Antiokia na kuanza kuongea na watu waliozungumza Kigiriki, wakitangaza habari njema ya Bwana Yesu. 21  Isitoshe, mkono wa Yehova* ulikuwa pamoja nao, na idadi kubwa wakawa waamini na kumgeukia Bwana.+ 22  Kutaniko lililokuwa Yerusalemu likasikia kuwahusu, nao wakamtuma Barnaba+ mpaka Antiokia. 23  Alipofika na kuziona fadhili zisizostahiliwa za Mungu, akashangilia na kuanza kuwatia moyo wote waendelee kukaa katika Bwana wakiwa wameazimia moyoni;+ 24  kwa maana alikuwa mtu mwema aliyejaa roho takatifu na imani. Na umati mkubwa ukaongezwa kwa Bwana.+ 25  Basi akaenda Tarso kumtafuta Sauli.+ 26  Baada ya kumpata, akamleta Antiokia. Basi kwa mwaka mzima wakakusanyika pamoja nao katika kutaniko na kufundisha umati mkubwa, na huko Antiokia ndiko kwa mara ya kwanza wanafunzi waliitwa Wakristo+ kupitia mwongozo wa Mungu. 27  Katika siku hizo manabii+ walishuka kutoka Yerusalemu mpaka Antiokia. 28  Mmoja wao aitwaye Agabo+ akasimama na kutabiri kupitia roho kwamba njaa kubwa ilikuwa karibu kutokea juu ya dunia yote inayokaliwa,+ na kwa kweli ilitokea wakati wa Klaudio. 29  Basi wanafunzi wakaamua kila mmoja kulingana na uwezo wake,+ watume msaada*+ kwa akina ndugu walioishi Yudea; 30  nao walifanya hivyo, wakatuma msaada kwa wazee kwa mikono ya Barnaba na Sauli.+

Maelezo ya Chini

Au “kushindana naye.”
Tnn., “chombo cha aina fulani.”
Au “kumpinga.”
Tnn., “wakanyamaza.”
Au “huduma ya msaada.”