Matendo ya Mitume 12:1-25

  • Yakobo auawa; Petro afungwa gerezani (1-5)

  • Petro awekwa huru kimuujiza (6-19)

  • Malaika ampiga Herode (20-25)

12  Karibu na wakati huo, Mfalme Herode akaanza kuwatesa baadhi ya watu katika kutaniko.+  Alimuua kwa upanga+ Yakobo ndugu ya Yohana.+  Alipoona Wayahudi wamefurahishwa na jambo hilo, akamkamata Petro pia. (Ulikuwa wakati wa Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu.)+  Akamkamata na kumtia gerezani,+ chini ya ulinzi wa zamu nne za wanajeshi wanne kwa kila zamu, naye alikusudia kumtoa* mbele ya watu baada ya Pasaka.  Kwa hiyo, Petro alikuwa gerezani lakini kutaniko lilikuwa likisali kwa Mungu kwa bidii sana kwa ajili yake.+  Herode alipokuwa karibu kumtoa, usiku huo Petro alikuwa amelala akiwa amefungwa kwa minyororo miwili katikati ya wanajeshi wawili, na walinzi walikuwa mbele ya mlango wakilinda gereza.  Lakini tazama! malaika wa Yehova* alikuwa amesimama hapo,+ na nuru ikang’aa katika chumba cha gereza. Akamgonga Petro ubavuni, akamwamsha akisema: “Simama upesi!” Na minyororo ikaanguka kutoka kwenye mikono yake.+  Malaika akamwambia: “Vaa nguo* na uvae viatu vyako.” Akafanya hivyo. Mwishowe akamwambia: “Vaa vazi lako la nje, uendelee kunifuata.”  Naye akatoka na kuendelea kumfuata, lakini hakujua kwamba mambo yaliyokuwa yakitendeka kupitia yule malaika yalikuwa halisi. Kwa kweli, alidhani anaona maono. 10  Wakampita mlinzi wa kwanza na wa pili, wakafika kwenye lango la chuma linaloelekea jijini, nalo likafunguka lenyewe mbele yao. Walipotoka nje wakapita kwenye barabara fulani, na mara moja yule malaika akamwacha. 11  Petro alipotambua kilichokuwa kikitendeka, akasema: “Sasa ninajua kwa hakika kwamba Yehova* alimtuma malaika wake na kunikomboa kutoka mkononi mwa Herode na mambo yote ambayo Wayahudi walitarajia.”+ 12  Baada ya kutambua hivyo, akaenda kwenye nyumba ya Maria mama ya Yohana aliyeitwa Marko,+ ambamo watu wengi walikuwa wamekusanyika wakisali. 13  Alipopiga hodi kwenye mlango wa lango kuu, kijakazi anayeitwa Roda akaenda kuangalia. 14  Alipotambua sauti ya Petro, akashangilia sana hivi kwamba badala ya kufungua lango, akarudi ndani mbio na kuwaeleza kwamba Petro amesimama langoni. 15  Wakamwambia: “Umerukwa na akili.” Lakini akaendelea kusisitiza kwamba ni kweli. Wakaanza kusema: “Ni malaika wake.” 16  Lakini Petro akaendelea kubisha. Walipofungua mlango, wakamwona nao wakashangaa. 17  Lakini akawapungia mkono wanyamaze na kuwaambia kirefu jinsi Yehova* alivyomtoa gerezani, naye akasema: “Waambieni Yakobo+ na akina ndugu mambo haya.” Ndipo akatoka, akasafiri kwenda mahali pengine. 18  Basi kulipokucha, kukawa na mvurugo miongoni mwa wanajeshi kuhusu kilichompata Petro. 19  Herode akamtafuta kwa bidii, na aliposhindwa kumpata, akawahoji walinzi na kuamuru wapelekwe kuadhibiwa;+ basi akatoka Yudea na kushuka kwenda Kaisaria, akakaa huko kwa muda. 20  Sasa alikuwa amewakasirikia* watu wa Tiro na Sidoni. Basi wakaja kwake wakiwa na kusudi moja, na baada ya kumshawishi Blasto, mwanamume aliyesimamia nyumba ya mfalme,* wakatoa ombi la amani, kwa sababu nchi yao ilipata chakula kutoka kwa nchi ya mfalme. 21  Siku moja iliyochaguliwa, Herode alivaa mavazi ya kifalme akaketi kwenye kiti cha hukumu na kuanza kuwahutubia watu wote. 22  Ndipo watu waliokusanyika wakaanza kusema kwa sauti kubwa: “Hii ni sauti ya mungu, si ya mwanadamu!” 23  Papo hapo, malaika wa Yehova* akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu, naye akaliwa na wadudu akafa. 24  Lakini neno la Yehova* likazidi kukua na kuenea.+ 25  Nao Barnaba+ na Sauli, baada ya kutimiza kikamili kazi ya kutoa msaada huko Yerusalemu,+ wakarudi na kumchukua Yohana,+ ambaye pia aliitwa Marko, aende pamoja nao.

Maelezo ya Chini

Au “kumtoa ili ahukumiwe.”
Au “Jifunge.”
Au “alitaka kupigana na.”
Tnn., “chumba cha kulala cha mfalme.”