Matendo ya Mitume 22:1-30

  • Paulo ajitetea mbele ya umati (1-21)

  • Paulo atumia uraia wake wa Roma (22-29)

  • Baraza la Sanhedrini lakutana (30)

22  “Wanaume, akina ndugu na akina baba, nisikilizeni ninapojitetea mbele yenu sasa.”+  Basi, waliposikia anazungumza nao kwa lugha ya Kiebrania, wakazidi kukaa kimya, naye akasema:  “Mimi ni Myahudi,+ aliyezaliwa huko Tarso ya Kilikia,+ nilielimishwa katika jiji hili miguuni pa Gamalieli,+ na kufundishwa kwa usahihi kabisa Sheria ya mababu,+ nikiwa na bidii kwa ajili ya Mungu kama nyote mlivyo leo.+  Niliitesa Njia hii kufikia kifo, nikiwafunga na kuwatia magerezani wanaume na wanawake pia,+  kama vile kuhani mkuu na kusanyiko lote la wazee wanavyoweza kutoa ushahidi. Nilipata pia barua kutoka kwao ili nizipeleke kwa akina ndugu huko Damasko, nami nilikuwa ninaenda kuwakamata wale waliokuwa huko na kuwaleta Yerusalemu wakiwa wamefungwa ili waadhibiwe.  “Lakini nilipokuwa safarini nikikaribia kufika Damasko, karibu katikati ya mchana, ghafla nuru kubwa kutoka mbinguni ikamulika kunizunguka,+  nami nikaanguka chini na kusikia sauti ikiniuliza: ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?’  Nikajibu: ‘Wewe ni nani Bwana?’ Naye akaniambia: ‘Mimi ni Yesu Mnazareti, ambaye unamtesa.’  Basi watu waliokuwa pamoja nami, waliiona ile nuru lakini hawakuisikia sauti ya yule aliyezungumza nami. 10  Ndipo nikamuuliza: ‘Nifanye nini Bwana?’ Bwana akaniambia: ‘Simama, uende Damasko, na huko utaambiwa kila kitu ambacho umepangiwa kufanya.’+ 11  Lakini kwa kuwa sikuweza kuona chochote kwa sababu ya utukufu wa nuru hiyo, wale waliokuwa pamoja nami wakanishika mkono na kuniongoza mpaka Damasko. 12  “Kisha mwanamume anayeitwa Anania, aliyemwogopa Mungu kulingana na Sheria, na kushuhudiwa vema na Wayahudi wote walioishi huko, 13  akaja nilipokuwa. Akasimama kando yangu, akaniambia, ‘Sauli ndugu, anza kuona tena!’ Papo hapo nikatazama juu nikamwona.+ 14  Akasema: ‘Mungu wa mababu zetu amekuchagua ujue mapenzi yake na umwone yule aliye mwadilifu+ na kuisikia sauti ya kinywa chake, 15  kwa sababu utakuwa shahidi wake kwa watu wote kuhusu mambo ambayo umeona na kusikia.+ 16  Na sasa kwa nini unakawia? Simama, ubatizwe na uoshe dhambi zako+ kwa kuliitia jina lake.’+ 17  “Lakini niliporudi Yerusalemu,+ nikiwa ninasali hekaluni, nikapata njozi 18  na kumwona Bwana akiniambia: ‘Fanya upesi uondoke Yerusalemu haraka, kwa sababu hawatakubali ushahidi wako kunihusu.’+ 19  Nami nikasema: ‘Bwana, wao wenyewe wanajua vema kwamba nilikuwa nikiwatia gerezani na kuwapiga viboko katika sinagogi moja baada ya lingine wale waliokuamini;+ 20  na damu ya Stefano shahidi wako ilipokuwa ikimwagwa, nilikuwa nimesimama kando na kukubaliana na jambo hilo nikiyalinda mavazi ya nje ya wale waliokuwa wakimuua.’+ 21  Na bado akaniambia: ‘Nenda kwa sababu nitakutuma kwa mataifa yaliyo mbali.’”+ 22  Basi wakaendelea kumsikiliza mpaka aliposema maneno hayo. Kisha wakasema kwa sauti kubwa: “Mwondoeni duniani mtu kama huyu, hafai kuishi!” 23  Kwa sababu walikuwa wakipiga kelele na kutupa mavazi yao ya nje huku na huku na kurusha mavumbi hewani,+ 24  yule kamanda wa jeshi akaagiza Paulo aingizwe katika makao ya wanajeshi na kuamuru ahojiwe huku akipigwa mijeledi, ili ajue kwa nini hasa walikuwa wakimpigia Paulo kelele hivyo. 25  Lakini walipokuwa wamemnyoosha ili kumpiga mijeledi, Paulo akamuuliza ofisa wa jeshi aliyekuwa amesimama hapo: “Je, ni halali kwenu kumpiga mijeledi Mroma* ambaye hajahukumiwa?”*+ 26  Yule ofisa wa jeshi aliposikia hivyo, akaenda kwa kamanda wa jeshi na kumwambia: “Unakusudia kufanya nini? Kwa maana mtu huyu ni Mroma.” 27  Basi kamanda wa jeshi akakaribia na kumuuliza: “Niambie, wewe ni Mroma?” Akajibu: “Ndiyo.” 28  Kamanda wa jeshi akasema: “Mimi nilinunua haki hizo za kuwa raia kwa pesa nyingi.” Paulo akasema: “Lakini mimi nina haki hizo kwa kuzaliwa.”+ 29  Kwa hiyo, mara moja watu waliokuwa karibu kumhoji kwa kumtesa wakamwacha; na kamanda wa jeshi akaogopa alipotambua kwamba Paulo ni Mroma na kwamba alikuwa amemfunga kwa minyororo.+ 30  Basi siku iliyofuata, kwa kuwa alitaka kujua hasa sababu iliyowafanya Wayahudi wamshtaki, akamfungua na kuwaamuru wakuu wa makuhani na Sanhedrini yote wakusanyike. Kisha akamleta Paulo chini na kumsimamisha kati yao.+

Maelezo ya Chini

Au “raia Mroma.”
Au “bila uamuzi wa mahakama.”