Matendo ya Mitume 26:1-32

  • Paulo ajitetea mbele ya Agripa (1-11)

  • Paulo aeleza jinsi alivyogeuka (12-23)

  • Maoni ya Festo na Agripa (24-32)

26  Agripa+ akamwambia Paulo: “Unaruhusiwa kujitetea.” Ndipo Paulo akanyoosha mkono wake na kuanza kujitetea:  “Kuhusu mambo yote ninayoshtakiwa na Wayahudi,+ Mfalme Agripa, ninafurahi kwamba ninajitetea mbele yako leo,  hasa kwa sababu wewe una ujuzi mwingi kuhusu desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kwa hiyo, ninakuomba unisikilize kwa subira.  “Kwa kweli, maisha niliyoishi tangu ujana miongoni mwa watu wangu* na huko Yerusalemu yanajulikana vizuri na Wayahudi wote+  ambao mwanzoni walinifahamu, nao wakipenda wanaweza kutoa ushahidi kwamba niliishi nikiwa Farisayo+ kulingana na madhehebu yetu yenye msimamo mkali zaidi katika ibada yetu.+  Lakini sasa, kwa sababu ya tumaini la ahadi iliyotolewa na Mungu kwa mababu zetu,+ nimeitwa kwenye hukumu;  makabila yetu 12 yanatumaini kuona ahadi hiyo ikitimizwa kwa kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa bidii usiku na mchana. Wayahudi wananishtaki kwa sababu ya tumaini hili,+ ewe Mfalme.  “Kwa nini mnafikiri* kwamba ni jambo lisilowezekana kwa Mungu kuwafufua wafu?  Mimi niliamini kwamba ninapaswa kufanya matendo mengi ili kulipinga jina la Yesu Mnazareti. 10  Hivyo ndivyo nilivyofanya huko Yerusalemu, niliwafunga gerezani watakatifu wengi,+ kwa maana nilikuwa nimepewa mamlaka na wakuu wa makuhani;+ na walipopaswa kuuawa, nilipiga kura yangu dhidi yao. 11  Niliwaadhibu mara nyingi katika masinagogi yote, nikijaribu kuwalazimisha wakane imani yao; na kwa sababu nilikuwa nimewakasirikia sana, nilifikia hatua ya kuwatesa hata katika majiji yaliyo mbali. 12  “Nilipokuwa nikifanya hivyo nikiwa safarini kwenda Damasko pia nikiwa na mamlaka na maagizo kutoka kwa wakuu wa makuhani, 13  katikati ya mchana niliona barabarani, ewe Mfalme, nuru kutoka mbinguni inayozidi mwangaza wa jua ikimulika kunizunguka mimi na wale waliokuwa wakisafiri pamoja nami.+ 14  Sisi sote tulipoanguka chini, nikasikia sauti ikiniambia katika lugha ya Kiebrania: ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa? Kuendelea kuipiga teke michokoo* kunafanya iwe vigumu kwako.’⁠ 15  Lakini nikauliza: ‘Wewe ni nani Bwana?’ Naye Bwana akajibu: ‘Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa. 16  Hata hivyo, inuka usimame kwa miguu yako. Kwa sababu nimekutokea ili nikuchague uwe mtumishi na shahidi wa mambo ambayo umeona na pia mambo nitakayokuonyesha kunihusu.+ 17  Nami nitakuokoa kutoka kwa watu hawa na kutoka kwa mataifa ambayo ninakutuma kwao+ 18  ili kuwafungua macho,+ kuwageuza watoke gizani+ waingie kwenye nuru+ na watoke kwenye mamlaka ya Shetani+ wamgeukie Mungu, ili wasamehewe dhambi zao+ na kupata urithi miongoni mwa wale waliotakaswa kwa kuniamini mimi.’ 19  “Kwa hiyo, Mfalme Agripa, mimi sikukosa kutii maono hayo kutoka mbinguni, 20  lakini kwanza kwa wale walio huko Damasko+ kisha kwa wale walio Yerusalemu,+ na katika nchi yote ya Yudea, na pia kwa mataifa, nilikuwa nikipeleka ujumbe kwamba wanapaswa kutubu na kumgeukia Mungu kwa kufanya matendo yanayoonyesha toba.+ 21  Hiyo ndiyo sababu Wayahudi walinikamata hekaluni na kujaribu kuniua.+ 22  Hata hivyo, kwa sababu nimepata msaada kutoka kwa Mungu, mpaka leo hii ninaendelea kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia, bila kusema lolote zaidi ya yale ambayo Manabii na pia Musa walisema yatatukia+ 23  kwamba Kristo atateseka+ na akiwa wa kwanza kufufuliwa kutoka kwa wafu,+ atawatangazia nuru watu hawa na pia mataifa.”+ 24  Paulo alipokuwa akijitetea kwa kusema mambo hayo, Festo akasema kwa sauti kubwa: “Unarukwa na akili, Paulo! Kusoma kwingi kunafanya urukwe na akili!” 25  Lakini Paulo akasema: “Mimi sirukwi na akili, ewe Mtukufu Festo, bali ninasema maneno ya kweli na ya akili timamu. 26  Kwa kweli, mfalme ninayezungumza naye kwa uhuru anajua vizuri mambo haya; nina hakika kwamba hakuna hata moja kati ya mambo haya ambalo hajui, kwa maana hakuna jambo lolote lililofanywa kisiri.+ 27  Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii? Ninajua unawaamini.” 28  Lakini Agripa akamwambia Paulo: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” 29  Ndipo Paulo akasema: “Ninamwomba Mungu kwamba iwe ni kwa muda mfupi au muda mrefu, si wewe tu bali pia wote wanaonisikia leo wawe kama mimi nilivyo, ila tu bila vifungo hivi vya gereza.” 30  Ndipo mfalme akasimama, vilevile gavana na Bernike na watu walioketi pamoja nao. 31  Lakini walipokuwa wakiondoka wakaanza kuambiana: “Mtu huyu hafanyi lolote linalostahili kifo au vifungo vya gereza.”+ 32  Kisha Agripa akamwambia Festo: “Mtu huyu angefunguliwa kama hangekuwa amekata rufaa kwa Kaisari.”+

Maelezo ya Chini

Au “taifa langu.”
Tnn., “mnahukumu.”
Mchokoo ni fimbo yenye ncha iliyochongoka inayotumiwa kumwelekeza mnyama.