Matendo ya Mitume 28:1-31

  • Ufuoni huko Malta (1-6)

  • Baba ya Publio aponywa (7-10)

  • Kuelekea Roma (11-16)

  • Paulo azungumza na Wayahudi huko Roma (17-29)

  • Paulo ahubiri kwa ujasiri kwa miaka miwili (30, 31)

28  Tulipofika salama ufuoni, tukajua kwamba kisiwa hicho kiliitwa Malta.+  Na watu hao waliozungumza lugha ya kigeni* walitutendea kwa fadhili zinazopita za kawaida.* Wakawasha moto na kutukaribisha sote kwa fadhili kwa sababu mvua ilikuwa ikinyesha na kulikuwa na baridi.  Lakini Paulo alipokusanya tita la kuni na kuliweka juu ya moto, nyoka* akatoka kwa sababu ya joto na kujifunga kwenye mkono wake.  Watu hao waliozungumza lugha ya kigeni walipomwona nyoka huyo mwenye sumu akining’inia kwenye mkono wake, wakaanza kuambiana: “Hakika mtu huyu ni muuaji, na ingawa alifika salama kutoka baharini, Haki* haikumruhusu aendelee kuishi.”  Hata hivyo, akamkung’uta yule nyoka na kumtupa ndani ya moto, naye hakupatwa na madhara.  Lakini walitarajia kwamba atavimba au aanguke na kufa ghafla. Baada ya kusubiri kwa muda mrefu na kuona hajapatwa na jambo lolote baya, wakabadili maoni yao na kuanza kusema yeye ni mungu.  Sasa karibu na mahali hapo kulikuwa na mashamba ya mkuu wa kisiwa hicho, aliyeitwa Publio, ambaye alitukaribisha na kutuonyesha ukarimu kwa siku tatu.  Ikawa kwamba baba ya Publio alikuwa amelala kitandani akiugua homa na ugonjwa wa kuhara damu. Paulo akaingia alimokuwa na kusali, akaweka mikono juu yake, akamponya.+  Baada ya tukio hilo, wote waliokuwa wagonjwa katika kisiwa hicho wakaanza pia kuja kwake na kuponywa.+ 10  Pia wakatupatia zawadi nyingi, na tulipokuwa tukianza safari, wakapakia melini vitu vyote tulivyohitaji. 11  Miezi mitatu baadaye tukasafiri kwa meli ambayo upande wa mbele ilikuwa na sanamu ya “Wana wa Zeu.” Meli hiyo ilitoka Aleksandria na ilikuwa imekaa kwenye kisiwa hicho wakati wa majira ya baridi kali. 12  Tukatia nanga katika bandari ya Sirakusa tukakaa huko siku tatu; 13  kutoka hapo tukasafiri mpaka Regiamu. Siku moja baadaye, upepo wa kusini ukaanza kuvuma nasi tukaingia Puteoli siku ya pili. 14  Tukawakuta akina ndugu huko, wakatusihi tukae pamoja nao kwa siku saba, kisha tukaelekea Roma. 15  Kutoka huko, akina ndugu waliposikia habari zetu, wakaja mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu ili kutupokea. Paulo alipowaona, akamshukuru Mungu na kujipa moyo.+ 16  Mwishowe, tulipoingia Roma, Paulo aliruhusiwa kukaa peke yake akiwa na mwanajeshi aliyemlinda. 17  Hata hivyo, baada ya siku tatu akawaita wanaume mashuhuri wa Wayahudi. Walipokuwa wamekusanyika, akawaambia: “Wanaume, akina ndugu, ingawa sikuwa nimefanya jambo lolote kinyume cha watu au desturi za mababu zetu,+ nilikabidhiwa nikiwa mfungwa kutoka Yerusalemu na kutiwa mikononi mwa Waroma.+ 18  Na baada ya kufanya uchunguzi,+ walitaka kuniacha huru, kwa maana hawakuwa na sababu yoyote ya kuniua.+ 19  Lakini Wayahudi walipopinga, nililazimika kukata rufaa kwa Kaisari,+ lakini si kwa sababu nilikuwa na shtaka lolote dhidi ya taifa langu. 20  Basi kwa sababu hii niliomba kuwaona na kuzungumza nanyi, kwa maana nimefungwa mnyororo huu kwa sababu ya tumaini la Israeli.”+ 21  Wakamwambia: “Hatujapokea barua zozote kukuhusu kutoka Yudea, wala hakuna ndugu yeyote aliyekuja kutoka huko ambaye ametujulisha au kusema jambo lolote baya juu yako. 22  Lakini tunaona inafaa kusikia kutoka kwako maoni yako, kwa maana kwa kweli kuhusu madhehebu haya,+ tunajua yanasemwa vibaya kila mahali.”+ 23  Basi wakapanga siku ya kukutana pamoja naye, nao wakaja wakiwa wengi hata zaidi mahali alipoishi. Na kuanzia asubuhi mpaka jioni, akawafafanulia jambo hilo na kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu, ili kuwashawishi kumhusu Yesu+ kwa kutumia Sheria ya Musa+ na pia Manabii.+ 24  Baadhi yao wakaanza kuamini mambo aliyosema; lakini wengine hawakuamini. 25  Basi kwa sababu hawakukubaliana miongoni mwao, wakaanza kuondoka, naye Paulo akasema jambo hili moja: “Kwa kufaa roho takatifu ilisema kupitia Isaya nabii kwa mababu zenu, 26  ikisema, ‘Nenda kwa watu hawa uwaambie: “Kwa kweli mtasikia lakini hamtaelewa kamwe, na kwa kweli mtatazama, lakini hamtaona kamwe.+ 27  Kwa maana mioyo ya watu hawa imekuwa migumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia, nao wamefunga macho yao, ili wasione kamwe kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kuelewa kwa mioyo yao, nao wageuke nami niwaponye.”’+ 28  Basi jueni kwamba wokovu huu kutoka kwa Mungu umepelekwa kwa mataifa;+ nao kwa hakika watausikiliza.”+ 29 * —— 30  Kwa hiyo akakaa huko kwa miaka miwili kamili katika nyumba yake ya kukodi,+ naye alikuwa akiwakaribisha kwa fadhili wale wote waliomtembelea, 31  akiwahubiria Ufalme wa Mungu na kuwafundisha kumhusu Bwana Yesu Kristo kwa uhuru mwingi wa kusema,*+ bila kizuizi.

Maelezo ya Chini

Au “wenyeji wa nchi hiyo.”
Au “fadhili za kibinadamu.”
Au “nyoka-kipiri.”
Neno la Kigiriki Diʹke, ambalo huenda linarejelea mungu wa kike wa kulipiza kisasi au wazo la haki ya kudhaniwa.
Au “kwa ujasiri wote.”