Matendo ya Mitume 9:1-43

  • Sauli akiwa njiani kuelekea Damasko (1-9)

  • Anania atumwa kumsaidia Sauli (10-19a)

  • Sauli ahuburi kumhusu Yesu huko Damasko (19b-25)

  • Sauli atembelea Yerusalemu (26-31)

  • Petro amponya Ainea (32-35)

  • Dorkasi mkarimu afufuliwa (36-43)

9  Lakini Sauli aliendelea kuwatisha wanafunzi wa Bwana akitaka kuwaua,+ basi akamwendea kuhani mkuu  na kumwomba barua za kwenda kwenye masinagogi huko Damasko, ili awakamate wanaume na wanawake walioifuata Ile Njia,+ na kuwaleta Yerusalemu wakiwa wamefungwa.  Akiwa safarini karibu kufika Damasko, ghafla nuru kutoka mbinguni ikamulika kumzunguka,+  naye akaanguka chini na kusikia sauti ikimwambia: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?”  Akauliza: “Wewe ni nani Bwana?” Akajibu: “Mimi ni Yesu,+ ambaye unamtesa.+  Hata hivyo, inuka uende jijini, nawe utaambiwa unachopaswa kufanya.”  Wanaume waliokuwa wakisafiri pamoja naye walisimama wakiwa hawana la kusema, kwa kweli waliisikia sauti, lakini hawakumwona mtu yeyote.+  Kisha Sauli akainuka, na ingawa macho yake yalikuwa yamefunguka, hangeweza kuona chochote. Basi wakamshika mkono na kumwongoza mpaka Damasko.  Na kwa siku tatu hakuona chochote,+ na hakula wala kunywa. 10  Huko Damasko kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Anania,+ naye Bwana akamwambia katika maono: “Anania!” Akajibu: “Mimi hapa, Bwana.” 11  Bwana akamwambia: “Ondoka, uende kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, umtafute mwanamume anayeitwa Sauli, kutoka Tarso,+ kwenye nyumba ya Yuda. Kwa maana tazama! anasali, 12  na katika maono amemwona mwanamume anayeitwa Anania akiingia na kuweka mikono juu yake ili aweze kuona tena.”+ 13  Lakini Anania akajibu: “Bwana, nimesikia kutoka kwa watu wengi kuhusu mtu huyu, jinsi alivyowatesa watakatifu wako huko Yerusalemu. 14  Na sasa amepewa mamlaka na wakuu wa makuhani ili awakamate* wote wanaoliitia jina lako.”+ 15  Lakini Bwana akamwambia: “Nenda! kwa sababu mtu huyu ni chombo nilichokichagua+ ili kupeleka jina langu kwa mataifa+ na pia kwa wafalme+ na wana wa Israeli. 16  Kwa maana nitamwonyesha waziwazi mateso mengi yatakayompata kwa sababu ya jina langu.”+ 17  Basi Anania akaenda na kuingia katika ile nyumba, naye akaweka mikono yake juu ya Sauli na kusema: “Sauli, ndugu, Bwana Yesu aliyekutokea barabarani ulipokuwa ukija, amenituma ili uweze kuona tena na ujazwe roho takatifu.”+ 18  Papo hapo, vitu kama magamba vikaanguka kutoka katika macho yake, naye akaanza kuona tena. Kisha akasimama na kubatizwa, 19  naye akala chakula na kupata nguvu. Akakaa kwa siku kadhaa pamoja na wanafunzi huko Damasko,+ 20  na mara moja akaanza kuhubiri katika masinagogi kuhusu Yesu, kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu. 21  Wote waliomsikia wakashangaa na kusema: “Je, huyu si yule mtu aliyewashambulia wale wanaoliitia jina hilo huko Yerusalemu?+ Je, hakuja huku ili awakamate na kuwapeleka* kwa wakuu wa makuhani?”+ 22  Lakini Sauli akazidi kupata nguvu na kuwashangaza Wayahudi walioishi Damasko, akithibitisha kupatana na akili kwamba huyu ndiye Kristo.+ 23  Baada ya siku nyingi kupita, Wayahudi wakapanga njama pamoja ili kumuua.+ 24  Hata hivyo, Sauli akagundua njama yao. Pia walikuwa wakilinda malango usiku na mchana ili wamuue. 25  Basi wanafunzi wake wakamchukua na kumshusha usiku kupitia shimo ukutani, akiwa ndani ya kapu.+ 26  Alipofika Yerusalemu,+ akajaribu kujiunga na wanafunzi, lakini wote walimwogopa kwa sababu hawakuamini kwamba amekuwa mwanafunzi. 27  Ndipo Barnaba+ akamsaidia na kumpeleka kwa mitume, naye akawasimulia kirefu jinsi alivyokuwa amemwona Bwana+ barabarani, na kwamba alikuwa amezungumza naye, na jinsi alivyozungumza kwa ujasiri katika jina la Yesu+ huko Damasko. 28  Basi akakaa pamoja nao, akitembea kwa uhuru* huko Yerusalemu, akizungumza kwa ujasiri katika jina la Bwana. 29  Alikuwa akiongea na kubishana na Wayahudi waliozungumza Kigiriki, lakini hao walikuwa wakijaribu kumuua.+ 30  Akina ndugu walipogundua hilo, wakampeleka Kaisaria na kumtuma aende Tarso.+ 31  Ndipo kutaniko katika eneo lote la Yudea, Galilaya, na Samaria+ likaingia katika kipindi cha amani, huku likijengwa; nalo lilipokuwa likitembea katika kumwogopa Yehova* na katika faraja ya roho takatifu,+ likaendelea kuongezeka. 32  Petro alipokuwa akisafiri katika eneo hilo lote, akashuka pia kwa watakatifu walioishi Lida.+ 33  Huko akampata mwanamume aliyeitwa Ainea, ambaye alikuwa amelala kwenye kitanda chake kwa miaka minane, kwa maana alikuwa amepooza. 34  Petro akamwambia: “Ainea, Yesu Kristo anakuponya.+ Simama, utandike kitanda chako.”+ Naye akasimama mara moja. 35  Wote walioishi huko Lida na katika Nchi Tambarare ya Sharoni walipomwona, wakamgeukia Bwana. 36  Huko Yopa kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Tabitha, jina ambalo linapotafsiriwa linamaanisha “Dorkasi.”* Alikuwa akitenda matendo mema na kutoa zawadi za rehema. 37  Lakini siku hizo akawa mgonjwa, akafa. Basi wakamwosha na kumlaza katika chumba cha juu. 38  Kwa kuwa Lida ilikuwa karibu na Yopa, wanafunzi waliposikia kwamba Petro alikuwa katika jiji hilo wakatuma wanaume wawili wakamsihi: “Tafadhali njoo kwetu haraka iwezekanavyo.” 39  Ndipo Petro akainuka na kwenda pamoja nao. Alipofika, wakampeleka kwenye kile chumba cha juu; nao wajane wote wakaja kwake wakilia na kuonyesha mavazi mengi na majoho* ambayo Dorkasi alikuwa ametengeneza alipokuwa pamoja nao. 40  Petro akaagiza kila mtu aende nje,+ akapiga magoti na kusali. Kisha akaugeukia ule mwili, akasema: “Tabitha, inuka!” Akafungua macho yake, na alipomwona Petro, akaketi.+ 41  Petro akamshika mkono na kumwinua, akawaita watakatifu na wajane, akamkabidhi kwao akiwa hai.+ 42  Jambo hilo likajulikana kotekote huko Yopa, na wengi wakamwamini Bwana.+ 43  Petro akakaa Yopa siku kadhaa pamoja na mtengenezaji wa ngozi aliyeitwa Simoni.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “awafunge; awatie vifungoni.”
Tnn., “kuwaongoza wakiwa wamefungwa.”
Tnn., “akiingia na kutoka.”
Jina la Kigiriki Dorkasi na jina la Kiaramu Tabitha, yote yanamaanisha “Swala.”
Au “mavazi ya nje.”