Kulingana na Mathayo 17:1-27

  • Yesu ageuka sura (1-13)

  • Imani kama mbegu ya haradali (14-21)

  • Kifo cha Yesu chatabiriwa tena (22, 23)

  • Walipa kodi kwa sarafu iliyotolewa kinywani mwa samaki (24-27)

17  Siku sita baadaye, Yesu alienda pamoja na Petro, Yakobo na Yohana ndugu yake kwenye mlima mrefu wakiwa peke yao.+  Sura yake ikageuka mbele yao; uso wake ukang’aa kama jua, na mavazi yake ya nje yakang’aa* kama nuru.+  Tazama! wakaona Musa na Eliya wakizungumza na Yesu.  Ndipo Petro akamwambia Yesu: “Bwana, ni vizuri sisi tuwe hapa. Ukitaka, nitasimamisha mahema matatu hapa, moja lako, moja la Musa, na moja la Eliya.”  Alipokuwa bado akizungumza, tazama! wingu jangavu likawafunika, na tazama! sauti kutoka katika lile wingu ikasema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.+ Msikilizeni.”+  Wanafunzi waliposikia hilo wakaanguka kifudifudi, wakaogopa sana.  Ndipo Yesu akawakaribia, akawagusa na kuwaambia: “Simameni. Msiogope.”  Walipotazama juu, hawakumwona mtu yeyote ila Yesu tu.  Walipokuwa wakishuka kutoka mlimani, Yesu akawaamuru: “Msimwambie mtu yeyote maono hayo mpaka Mwana wa binadamu atakapofufuliwa kutoka kwa wafu.”+ 10  Hata hivyo, wanafunzi wakamuuliza: “Kwa nini basi waandishi husema kwamba lazima Eliya aje kwanza?”+ 11  Akawajibu: “Kwa kweli Eliya anakuja naye atarudisha mambo yote.+ 12  Hata hivyo, ninawaambia kwamba tayari Eliya amekuja lakini hawakumtambua bali walimtendea kama walivyotaka.+ Vivyo hivyo, Mwana wa binadamu atateseka mikononi mwao.”+ 13  Ndipo wanafunzi wakatambua kwamba alikuwa akiwaeleza kumhusu Yohana Mbatizaji. 14  Walipofika karibu na umati,+ mtu fulani akamkaribia Yesu, akapiga magoti, na kusema: 15  “Bwana, mhurumie* mwanangu, kwa sababu ana kifafa na ni mgonjwa sana. Yeye huanguka ndani ya moto na ndani ya maji mara nyingi.+ 16  Nilimleta kwa wanafunzi wako, lakini walishindwa kumponya.” 17  Yesu akajibu: “Enyi kizazi kisicho na imani na kilichopotoka,+ nitaendelea kuwa pamoja nanyi mpaka lini? Nitawavumilia mpaka lini? Mleteni hapa.” 18  Kisha Yesu akamkemea yule roho mwovu, naye akamtoka, na yule mvulana akapona kuanzia saa hiyo.+ 19  Ndipo wanafunzi wakamjia Yesu faraghani na kumuuliza: “Kwa nini tulishindwa kumfukuza?” 20  Akawaambia: “Ni kwa sababu ya imani yenu ndogo. Kwa kweli ninawaambia, mkiwa na imani inayolingana na mbegu ya haradali, mtauambia mlima huu, ‘Ondoka hapa uende pale,’ nao utaondoka, na hakuna jambo litakalowashinda.”+ 21 * —— 22  Walipokuwa wamekusanyika huko Galilaya, Yesu akawaambia: “Mwana wa binadamu atasalitiwa mikononi mwa watu,+ 23  nao watamuua, na siku ya tatu atafufuliwa.”+ Kwa hiyo wakahuzunika sana. 24  Baada ya kufika Kapernaumu watu wanaokusanya kodi ya drakma* mbili wakaja na kumuuliza Petro: “Je, mwalimu wenu hulipa kodi ya drakma mbili?”+ 25  Akajibu: “Ndiyo.” Hata hivyo, mara tu alipoingia ndani ya nyumba Yesu akamuuliza: “Unaonaje Simoni? Wafalme wa dunia hupokea ushuru au kodi* kutoka kwa nani? Kutoka kwa wana wao au kutoka kwa wageni?” 26  Alipojibu: “Kutoka kwa wageni,” Yesu akamwambia: “Basi, kwa kweli wana hawalipi kodi. 27  Lakini ili tusiwakwaze,+ nenda baharini utupe ndoano na uchukue samaki wa kwanza atakayetokea, na utakapofungua kinywa chake, utapata sarafu ya fedha.* Ichukue nawe uwape kwa ajili yangu na kwa ajili yako.”

Maelezo ya Chini

Au “yakawa meupe.”
Au “mwonyeshe rehema.”
Au “kodi ya kichwa.”
Tnn., “sarafu ya stateri,” inadhaniwa kuwa ndiyo tetradrakma. Angalia Nyongeza B14.