Kulingana na Mathayo 21:1-46

  • Yesu aingia kwa kishindo (1-11)

  • Yesu asafisha hekalu (12-17)

  • Mtini walaaniwa (18-22)

  • Wataka kujua chanzo cha mamlaka ya Yesu (23-27)

  • Mfano wa wana wawili (28-32)

  • Mfano wa wakulima wauaji (33-46)

    • Jiwe kuu la pembeni lakataliwa (42)

21  Walipokaribia Yerusalemu na kufika Bethfage kwenye Mlima wa Mizeituni, Yesu akawatuma wanafunzi wawili,+  akawaambia: “Nendeni katika kijiji mtakachokiona, na mara moja mtamwona punda amefungwa, na mwanapunda akiwa pamoja naye. Wafungueni na kuniletea.  Mtu yeyote akiwauliza, semeni, ‘Bwana anawahitaji.’ Na mara moja atawaruhusu mwachukue.”  Kwa kweli hilo lilitukia ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii:  “Mwambieni binti ya Sayuni, ‘Tazama! Mfalme wako anakuja kwako,+ naye ni mpole+ na amepanda juu ya punda, naam, juu ya mwanapunda, uzao wa mnyama wa kubeba mizigo.’”+  Kwa hiyo wale wanafunzi wakaenda na kufanya kama Yesu alivyowaagiza.+  Wakamleta huyo punda na mwanapunda wake, kisha wakatandika juu yao mavazi yao ya nje, naye akayakalia.+  Wengi katika umati wakatandaza mavazi yao ya nje barabarani,+ na wengine wakakata matawi ya miti na kuyatandaza barabarani.  Isitoshe umati uliomtangulia na wale waliomfuata waliendelea kupaza sauti: “Tunaomba umwokoe, Mwana wa Daudi!+ Amebarikiwa yule anayekuja katika jina la Yehova!*+ Tunaomba umwokoe, katika vilele vilivyo juu!”+ 10  Alipoingia Yerusalemu, jiji lote likawa na msukosuko, na kuulizana: “Ni nani huyu?” 11  Umati ukaendelea kusema: “Huyu ndiye nabii Yesu,+ kutoka Nazareti ya Galilaya!” 12  Yesu akaingia hekaluni na kuwafukuza wote waliokuwa wakiuza na kununua hekaluni, akazipindua meza za wale waliokuwa wakibadili pesa na viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa.+ 13  Akawaambia: “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala,’+ lakini ninyi mnaifanya kuwa pango la wanyang’anyi.”+ 14  Pia, vipofu na vilema wakamwendea hekaluni, naye akawaponya. 15  Wakuu wa makuhani na waandishi walipoona mambo ya kustaajabisha aliyofanya na pia wavulana waliokuwa wakipaza sauti hekaluni wakisema: “Tunaomba umwokoe, Mwana wa Daudi!”+ wakakasirika+ 16  na kumwambia: “Je, unasikia wanachosema?” Yesu akajibu: “Ndiyo. Je, hamkusoma jambo hili, ‘Kutoka katika vinywa vya watoto wadogo na wanaonyonya, umetoa sifa’?”+ 17  Kisha akawaacha, akatoka nje ya jiji na kwenda Bethania, akalala huko.+ 18  Alipokuwa akirudi jijini asubuhi na mapema, akahisi njaa.+ 19  Akaona mtini kando ya barabara, akaukaribia lakini hakupata chochote ila majani tu,+ akauambia: “Usizae matunda tena kamwe.”+ Mara moja ule mtini ukanyauka. 20  Wanafunzi walipoona hilo, wakashangaa na kusema: “Kwa nini mtini huu umenyauka mara moja?”+ 21  Yesu akawajibu: “Kwa kweli ninawaambia, mkiwa na imani nanyi msiwe na shaka, hamtafanya tu nilichoufanyia mtini huo, bali hata mkiuambia mlima huu, ‘Ng’oka, ukatupwe baharini,’ jambo hilo litatendeka.+ 22  Na mambo yote mnayoomba katika sala, mkiwa na imani, mtapokea.”+ 23  Baada ya kuingia hekaluni, wakuu wa makuhani na wazee wa watu wakaja alipokuwa akifundisha, wakamuuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Na ni nani aliyekupa mamlaka hayo?”+ 24  Yesu akawajibu: “Nami nitawauliza swali. Mkinijibu basi nitawaambia ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani: 25  Ubatizo wa Yohana, ulitoka wapi? Ulitoka mbinguni au kwa wanadamu?”* Lakini wakaanza kujadiliana kati yao wakisema: “Tukisema, ‘Ulitoka mbinguni,’ atatuuliza, ‘Kwa nini hamkumwamini?’+ 26  Lakini tukisema, ‘Ulitoka kwa wanadamu,’ tunaogopa umati, kwa maana wote wanamwona Yohana kuwa nabii.” 27  Basi wakamjibu: “Hatujui.” Naye Yesu akawaambia: “Nami siwaambii ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani. 28  “Mnaonaje? Mtu fulani alikuwa na watoto wawili. Akamwendea wa kwanza, akamwambia, ‘Mwanangu, leo nenda ukafanye kazi katika shamba la mizabibu.’ 29  Akamjibu, ‘Sitaenda,’ lakini baadaye akajuta na akaenda. 30  Akamwendea wa pili na kumwambia jambo hilohilo. Naye akamjibu, ‘Nitaenda Baba,’ lakini hakwenda. 31  Kati ya hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya baba yake?” Wakasema: “Yule wa kwanza.” Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia wakusanya kodi na makahaba wanawatangulia ninyi kuingia katika Ufalme wa Mungu. 32  Kwa maana Yohana alikuja kwenu katika njia ya uadilifu, lakini hamkumwamini. Hata hivyo, wakusanya kodi na makahaba walimwamini,+ nanyi, ijapokuwa mliona hilo, hamkujuta na kumwamini. 33  “Sikilizeni mfano mwingine: Kulikuwa na mtu aliyemiliki shamba, akapanda shamba la mizabibu+ na kulizungushia ua, akachimba shinikizo la divai* ndani yake, akajenga mnara;+ kisha akalikodisha kwa wakulima, naye akasafiri kwenda ng’ambo.+ 34  Majira ya matunda yalipofika, akawatuma watumwa wake kwa wakulima ili wakachukue matunda yake. 35  Hata hivyo, wakulima hao wakawakamata wale watumwa, mmoja wakampiga, mwingine wakamuua, na mwingine wakampiga mawe.+ 36  Akawatuma tena watumwa wengine, wengi zaidi ya wale wa kwanza, lakini wakawatendea vivyo hivyo.+ 37  Mwishowe akamtuma mwana wake kwao, akisema, ‘Watamheshimu mwanangu.’ 38  Wakulima walipomwona yule mwana wakaambiana, ‘Huyu ndiye mrithi.+ Njooni tumuue ili tuuchukue urithi wake!’ 39  Kwa hiyo wakamkamata, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu na kumuua.+ 40  Basi, mwenye shamba la mizabibu atakapokuja, atawatendea nini wakulima hao?” 41  Wakamwambia: “Kwa sababu ni waovu, atawaangamiza kabisa na kulikodisha shamba la mizabibu kwa wakulima wengine, ambao watampa matunda yatakapoiva.” 42  Yesu akawaambia: “Je, hamkusoma kamwe katika Maandiko kwamba ‘Jiwe ambalo wajenzi walilikataa limekuwa jiwe kuu la pembeni.*+ Hili limetoka kwa Yehova,* na ni lenye kustaajabisha machoni petu’?+ 43  Ndiyo sababu ninawaambia, Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu na kupewa taifa linalozaa matunda yake. 44  Pia, mtu atakayeanguka kwenye jiwe hilo atavunjika vipandevipande.+ Na litamponda yeyote litakayemwangukia.”+ 45  Wakuu wa makuhani na Mafarisayo waliposikia mifano ya Yesu, wakajua kwamba alikuwa akizungumza kuwahusu.+ 46  Ingawa walitaka kumkamata, waliogopa umati, kwa sababu walimwona kuwa nabii.+

Maelezo ya Chini

Au “chanzo chake ni wanadamu?”
Au “mahali pa kukamulia zabibu.”
Tnn., “kichwa cha pembeni.”