Kulingana na Mathayo 8:1-34

  • Mtu mwenye ukoma aponywa (1-4)

  • Ofisa wa jeshi mwenye imani (5-13)

  • Yesu aponya wengi Kapernaumu (14-17)

  • Jinsi ya kumfuata Yesu (18-22)

  • Yesu atuliza dhoruba (23-27)

  • Yesu awaruhusu roho waovu waingie katika nguruwe (28-34)

8  Yesu aliposhuka kutoka mlimani, umati mkubwa ukamfuata.  Na tazama! mtu fulani mwenye ukoma akaja na kumsujudia* akimwambia: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.”+  Basi akaunyoosha mkono wake, akamgusa na kusema: “Ninataka! Takasika.”+ Mara moja ukoma wake ukatakasika.+  Kisha Yesu akamwambia: “Usimwambie mtu yeyote,+ bali nenda, ukajionyeshe kwa kuhani,+ na utoe zawadi ambayo Musa aliagiza,+ ili kuwa ushahidi kwao.”  Alipoingia Kapernaumu, ofisa mmoja wa jeshi alimjia, akamsihi+  na kusema: “Bwana, mtumishi wangu amelala nyumbani na ana ugonjwa wa kupooza, naye anateseka sana.”  Akamwambia: “Nikifika huko, nitamponya.”  Ofisa huyo akamjibu: “Bwana, sistahili uingie ndani ya nyumba yangu, lakini sema tu neno na mtumishi wangu atapona.  Kwa maana mimi pia niko chini ya mamlaka, na nina wanajeshi walio chini yangu, nami humwambia mmoja, ‘Nenda!’ naye huenda, na mwingine, ‘Njoo!’ naye huja, na mtumwa wangu, ‘Fanya hili!’ naye hulifanya.” 10  Yesu aliposikia hayo, akashangaa na kuwaambia wale waliomfuata: “Ninawaambia ukweli, sijaona mtu yeyote katika Israeli mwenye imani kubwa kama hii.+ 11  Lakini ninawaambia kwamba wengi watakuja kutoka mashariki na magharibi na kuketi mezani pamoja na Abrahamu, Isaka, na Yakobo katika Ufalme wa mbinguni;+ 12  lakini wana wa Ufalme watatupwa nje gizani. Huko ndiko watalia na kusaga meno yao.”+ 13  Kisha Yesu akamwambia yule ofisa wa jeshi: “Nenda. Na iwe kama ulivyoamini.”+ Na yule mtumishi akapona saa ileile.+ 14  Yesu alipoingia nyumbani kwa Petro, alimwona mama mkwe wa Petro+ akiwa amelala akiugua homa.+ 15  Basi Yesu akamgusa mkono,+ naye akapona homa, akasimama na kuanza kumhudumia. 16  Lakini ilipofika jioni, watu walimletea watu wengi wenye roho waovu; akawafukuza hao roho kwa kusema neno moja, naye akawaponya wote waliokuwa wakiteseka, 17  ili yatimie maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii Isaya: “Yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu na kuyabeba maradhi yetu.”+ 18  Yesu alipoona umati umemzunguka, akaagiza wavuke kwenda ng’ambo ya bahari.+ 19  Mwandishi fulani akaja na kumwambia: “Mwalimu, nitakufuata popote utakapoenda.”+ 20  Lakini Yesu akamwambia: “Mbweha wana mapango na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali pa kulaza kichwa chake.”+ 21  Kisha mwanafunzi mwingine akamwambia: “Bwana, niruhusu kwanza niende nikamzike baba yangu.”+ 22  Yesu akamwambia: “Endelea kunifuata, waache wafu wawazike wafu wao.”+ 23  Alipopanda kwenye mashua, wanafunzi wake wakamfuata.+ 24  Na tazama! dhoruba kubwa ikatokea baharini, hata mawimbi yakaanza kuifunika mashua; lakini Yesu alikuwa amelala usingizi.+ 25  Wakaja na kumwamsha wakisema: “Bwana, tuokoe, tuko karibu kuangamia!” 26  Lakini akawauliza: “Kwa nini mnaogopa sana, ninyi wenye imani ndogo?”+ Kisha akasimama na kuukemea upepo na bahari, kukawa shwari kabisa.+ 27  Basi wanafunzi wakashangaa na kusema: “Huyu ni mtu wa aina gani? Hata upepo na bahari vinamtii.” 28  Alipofika upande ule mwingine na kuingia katika eneo la Wagadarene, alikutana na wanaume wawili waliokuwa na roho waovu wakitoka makaburini.*+ Walikuwa wakali sana, hivi kwamba hakuna mtu aliyekuwa na ujasiri wa kupita katika barabara hiyo. 29  Na tazama! wakapiga mayowe wakisema: “Kwa nini unatusumbua, Mwana wa Mungu?+ Je, umekuja kututesa+ kabla ya wakati uliowekwa?”+ 30  Lakini kule mbali nao kulikuwa na kundi la nguruwe wengi wakila.+ 31  Kwa hiyo wale roho waovu wakaanza kumsihi: “Ukitufukuza, turuhusu tuingie katika lile kundi la nguruwe.”+ 32  Basi akawaambia: “Nendeni!” Ndipo wakatoka na kuingia ndani ya wale nguruwe, na tazama! kundi zima likatimua mbio, likaruka poromoko* likazama baharini na kufa maji. 33  Lakini wachungaji wakakimbia, na walipoingia jijini, wakasimulia mambo yote, kutia ndani habari kuhusu wale watu waliokuwa na roho waovu. 34  Na tazama! watu wote katika jiji hilo wakaenda kukutana na Yesu, na walipomwona, wakamsihi aondoke katika eneo lao.+

Maelezo ya Chini

Au “kumwinamia.”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “ukingo wenye mteremko mkali.”