Mhubiri 10:1-20
10 Kama nzi waliokufa wanavyofanya mafuta ya mtengenezaji wa marashi yanuke na kutoa povu, ndivyo ujinga kidogo unavyozidi hekima na utukufu.+
2 Moyo wa mwenye hekima humwongoza katika njia inayofaa,* lakini moyo wa mpumbavu humwongoza katika njia isiyofaa.*+
3 Katika njia yoyote ambayo mjinga anatembea, hana busara,*+ naye huacha kila mtu ajue kwamba yeye ni mjinga.+
4 Hasira* ya mtawala ikiwaka dhidi yako, usiondoke mahali pako,+ kwa maana utulivu huzuia dhambi kubwa.+
5 Kuna jambo linalohuzunisha ambalo nimeona chini ya jua, aina ya kosa linalofanywa na watawala:+
6 Ujinga huwekwa katika vyeo vingi vya juu, lakini matajiri* hubaki kwenye vyeo vya chini.
7 Nimeona watumishi wakiwa wamepanda farasi lakini wakuu wakitembea kwa miguu kama watumishi tu.+
8 Anayechimba shimo huenda akaanguka ndani yake;+ na anayebomoa ukuta wa mawe huenda akaumwa na nyoka.
9 Anayechimbua mawe huenda yakamuumiza, na yule anayepasua magogo huenda yakamuumiza.*
10 Ikiwa kifaa cha chuma hakina makali na mtu hakinoi, atahitaji kutumia nguvu nyingi. Lakini hekima husaidia kuleta mafanikio.
11 Nyoka akiuma kabla hajachezeshwa, mtu anayemchezesha kwa ustadi* hapati faida yoyote.
12 Maneno yanayotoka kwenye kinywa cha mwenye hekima huleta kibali,+ lakini midomo ya mpumbavu ndiyo inayomwangamiza.+
13 Maneno ya kwanza yanayotoka katika kinywa chake ni ujinga,+ na maneno yake ya mwisho ni wazimu unaoleta msiba.
14 Lakini mjinga huendelea kuongea.+
Mwanadamu hajui yatakayotukia; ni nani anayeweza kumwambia yatakayotukia baada yake?+
15 Kazi ngumu ya mpumbavu humchosha kabisa, kwa sababu hata hajui jinsi atakavyofika jijini.
16 Ole kwa nchi ambayo mfalme wake ni mvulana+ na wakuu wake huanza karamu asubuhi!
17 Yenye furaha ni nchi ambayo mfalme wake ni mwana wa watu mashuhuri na wakuu wake hula wakati unaofaa ili wapate nguvu, si walewe!+
18 Kwa sababu ya uvivu unaopita kiasi paa hubonyea, na kwa sababu ya mikono milegevu nyumba huvuja.+
19 Mkate umekusudiwa* kuleta kicheko, na divai hufanya maisha yafurahishe;+ lakini pesa ni jawabu la mahitaji yote.+
20 Usimtukane* mfalme hata katika mawazo yako,*+ na usiwatukane matajiri katika chumba chako cha kulala; kwa sababu huenda ndege* akapeleka habari zako,* au huenda kiumbe mwenye mabawa akarudia lililosemwa.
Maelezo ya Chini
^ Tnn., “uko kwenye mkono wake wa kulia.”
^ Tnn., “uko kwenye mkono wake wa kushoto.”
^ Tnn., “moyo wake umepungukiwa.”
^ Tnn., “Roho, Pumzi.”
^ Au “wanaostahili.”
^ Au labda, “anapaswa kujihadhari nayo.”
^ Tnn., “stadi wa ulimi.”
^ Au “Chakula kimekusudiwa.”
^ Au “Usimlaani.”
^ Au labda, “kitandani mwako.”
^ Tnn., “kiumbe anayeruka angani.”
^ Tnn., “sauti yako.”