Mwanzo 13:1-18

  • Abramu arudi Kanaani (1-4)

  • Abramu na Loti watengana (5-13)

  • Mungu arudia ahadi aliyompa Abramu (14-18)

13  Kisha Abramu akapanda kutoka Misri kwenda Negebu,+ yeye pamoja na mke wake na vitu vyote alivyokuwa navyo, pamoja na Loti.  Abramu alikuwa na utajiri mwingi wa mifugo, fedha, na dhahabu.+  Alipiga kambi sehemu moja baada ya nyingine aliposafiri kutoka Negebu kwenda Betheli, mpaka alipofika mahali alipokuwa amepiga hema lake kati ya Betheli na Ai,+  mahali alipokuwa amejenga madhabahu mwanzoni. Huko, Abramu akaliitia jina la Yehova.  Sasa Loti, aliyekuwa akisafiri pamoja na Abramu, alikuwa pia na kondoo, ng’ombe, na mahema.  Basi wote hawangeweza kukaa pamoja kwa sababu nchi haikuwatosha; mali zao zilikuwa zimeongezeka sana hivi kwamba hawangeweza tena kukaa pamoja.  Kwa sababu hiyo, ugomvi ukatokea kati ya wachungaji wa mifugo ya Abramu na wachungaji wa mifugo ya Loti. (Wakati huo Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi hiyo.)+  Basi Abramu akamwambia Loti:+ “Tafadhali, pasiwe na ugomvi wowote kati yangu mimi na wewe na kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako, kwa maana sisi ni ndugu.  Je, nchi yote haiko mbele yako? Tafadhali, jitenge nami. Ukienda kushoto, nitakwenda kulia; lakini ukienda kulia, basi mimi nitakwenda kushoto.” 10  Kwa hiyo Loti akainua macho yake na kuona kwamba wilaya yote ya Yordani+ ilikuwa na maji ya kutosha (kabla Yehova hajaharibu Sodoma na Gomora), kama bustani ya Yehova,+ kama nchi ya Misri, mpaka Soari.+ 11  Basi Loti akajichagulia wilaya yote ya Yordani, naye Loti akahamisha kambi yake kuelekea upande wa mashariki. Kwa hiyo wakatengana. 12  Abramu aliishi katika nchi ya Kanaani, lakini Loti aliishi katika majiji ya wilaya hiyo.+ Hatimaye akapiga hema lake karibu na Sodoma. 13  Sasa watu wa Sodoma walikuwa waovu, nao walitenda dhambi nzito machoni pa Yehova.+ 14  Yehova akamwambia hivi Abramu baada ya Loti kujitenga naye: “Tafadhali, inua macho yako, na kutoka mahali ulipo tazama kaskazini na kusini, mashariki na magharibi, 15  kwa sababu nchi yote unayoona, nitakupa wewe na uzao wako* iwe miliki yenu ya kudumu.+ 16  Nami nitaufanya uzao wako uwe* kama chembe za mavumbi ya ardhi, hivi kwamba ikiwa kuna yeyote anayeweza kuhesabu chembe za mavumbi ya ardhi, basi uzao wako utaweza* kuhesabiwa.+ 17  Ondoka, safiri kwa mapana na marefu katika nchi hii, kwa maana nitakupa wewe nchi hii.” 18  Basi Abramu akaendelea kuishi katika mahema. Baadaye akaja na kuishi kati ya miti mikubwa ya Mamre,+ ambayo iko Hebroni,+ na huko akamjengea Yehova madhabahu.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “nitaifanya mbegu yako iwe.”
Tnn., “mbegu yako itaweza.”