Mwanzo 17:1-27

  • Abrahamu atakuwa baba wa mataifa mengi (1-8)

    • Abramu apewa jina jipya, Abrahamu (5)

  • Agano la kutahiri (9-14)

  • Sarai apewa jina jipya, Sara (15-17)

  • Aahidiwa kumzaa mwana aitwaye Isaka (18-27)

17  Abramu alipokuwa na umri wa miaka 99, Yehova alimtokea na kumwambia: “Mimi ni Mungu Mweza-Yote. Tembea mbele zangu na ujithibitishe mwenyewe kuwa bila kosa.*  Nitaimarisha agano langu kati yangu na wewe,+ nami nitawafanya wazao wako wawe wengi, wengi sana.”+  Ndipo Abramu akaanguka kifudifudi, na Mungu akaendelea kuongea naye, na kumwambia:  “Mimi nami, tazama! agano langu liko pamoja nawe,+ nawe hakika utakuwa baba wa mataifa mengi.+  Jina lako halitakuwa tena Abramu;* jina lako litakuwa Abrahamu,* kwa sababu nitakufanya kuwa baba wa mataifa mengi.  Nitakufanya uwe na wazao wengi, wengi sana, nami nitakufanya uwe mataifa, na wafalme watatoka kwako.+  “Nami nitalishika agano langu nililofanya pamoja nawe+ na uzao wako* baada yako katika vizazi vyao vyote; hili ni agano la milele, ili niwe Mungu wako na Mungu wa uzao wako* baada yako.  Nami nitakupa wewe na uzao wako* baada yako nchi ambamo uliishi ukiwa mgeni+—nchi yote ya Kanaani—iwe miliki ya kudumu, nami nitakuwa Mungu wao.”+  Mungu akaendelea kumwambia Abrahamu: “Wewe nawe, unapaswa kushika agano langu, wewe na uzao wako* baada yako katika vizazi vyao vyote. 10  Hili ndilo agano langu nililofanya pamoja nawe, ambalo wewe na uzao wako* baada yako mtalishika: Kila mwanamume miongoni mwenu ni lazima atahiriwe.+ 11  Ni lazima mtahiri nyama ya magovi yenu, na jambo hilo litakuwa ishara ya agano kati yangu nanyi.+ 12  Katika vizazi vyenu vyote, kila mwanamume miongoni mwenu mwenye umri wa siku nane ni lazima atahiriwe,+ yeyote anayezaliwa nyumbani mwenu na yeyote ambaye si mmoja wa uzao wenu* na yeyote aliyenunuliwa kwa pesa kutoka kwa mgeni. 13  Kila mwanamume aliyezaliwa nyumbani mwenu na kila mwanamume aliyenunuliwa kwa pesa zenu ni lazima atahiriwe,+ na agano langu katika miili yenu litakuwa agano la kudumu. 14  Ikiwa mwanamume yeyote ambaye hajatahiriwa hatatahiri nyama ya govi lake, ni lazima auawe. Amevunja agano langu.” 15  Kisha Mungu akamwambia Abrahamu: “Kuhusu mke wako Sarai,*+ usimwite tena Sarai, kwa sababu jina lake litakuwa Sara.* 16  Nitambariki na pia nitakupa mwana kupitia yeye;+ nitambariki Sara, naye atakuwa mataifa; wafalme wa mataifa watatoka kwake.” 17  Ndipo Abrahamu akaanguka kifudifudi, akaanza kucheka na kusema moyoni mwake:+ “Je, mwanamume mwenye umri wa miaka 100 atazaa mtoto, na je, Sara, mwanamke mwenye umri wa miaka 90, atazaa?”+ 18  Kwa hiyo Abrahamu akamwambia Mungu wa kweli: “Afadhali umbariki Ishmaeli ili aendelee kuishi!”+ 19  Ndipo Mungu akasema: “Mke wako Sara hakika atakuzalia mwana, nawe unapaswa kumpa jina Isaka.*+ Nami nitaimarisha agano langu pamoja naye liwe agano la milele kwa uzao wake* baada yake.+ 20  Lakini kuhusu Ishmaeli, nimesikia ombi lako. Tazama! Nitambariki, nami nitamfanya awe na wazao wengi, nao wataongezeka na kuwa wengi, wengi sana. Atazaa wakuu 12, nami nitamfanya awe taifa kubwa.+ 21  Hata hivyo, nitaimarisha agano langu pamoja na Isaka,+ ambaye Sara atakuzalia wakati huuhuu mwaka ujao.”+ 22  Mungu alipomaliza kuzungumza na Abrahamu, alipanda na kumwacha Abrahamu. 23  Kisha Abrahamu akamchukua Ishmaeli mwana wake na wanaume wote waliozaliwa nyumbani mwake na kila mwanamume aliyekuwa amemnunua kwa pesa, kila mwanamume katika nyumba ya Abrahamu, naye akawatahiri nyama ya magovi yao siku hiyohiyo, kama Mungu alivyokuwa amemwambia.+ 24  Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 99 alipotahiriwa nyama ya govi lake.+ 25  Na Ishmaeli mwanawe alikuwa na umri wa miaka 13 alipotahiriwa nyama ya govi lake.+ 26  Siku hiyohiyo, Abrahamu alitahiriwa na pia Ishmaeli mwanawe. 27  Wanaume wote wa nyumba yake, yeyote aliyezaliwa nyumbani mwake na yeyote aliyenunuliwa kwa pesa kutoka kwa mgeni, walitahiriwa pia pamoja naye.

Maelezo ya Chini

Au “bila lawama.”
Maana yake “Baba Yuko Juu (Amekwezwa).”
Maana yake “Baba wa Umati (Halaiki); Baba wa Wengi.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu yenu.”
Huenda jina hili linamaanisha “Mgomvi.”
Maana yake “Binti ya Mfalme.”
Tnn., “mbegu yake.”
Maana yake “Kicheko.”