Mwanzo 18:1-33

  • Malaika watatu wamtembelea Abrahamu (1-8)

  • Sara aahidiwa kuzaa mwana; Sara acheka (9-15)

  • Abrahamu amsihi Mungu asiangamize Sodoma (16-33)

18  Baadaye, Yehova*+ akamtokea kati ya miti mikubwa ya Mamre+ alipokuwa ameketi kwenye mlango wa hema mchana wakati wa joto kali.  Akainua macho yake na kuwaona wanaume watatu wakiwa wamesimama umbali fulani kutoka kwake.+ Alipowaona, alikimbia kutoka kwenye mlango wa hema na kwenda kuwapokea, naye akainama mpaka chini.  Kisha akasema: “Yehova, ikiwa nimepata kibali machoni pako, tafadhali usinipite mimi mtumishi wako.  Tafadhali, acheni maji kidogo yaletwe ili mwoshwe miguu yenu;+ kisha mpumzike chini ya mti.  Kwa sababu mmekuja hapa kwangu mimi mtumishi wenu, acheni nilete kipande cha mkate ili mjiburudishe.* Kisha mnaweza kuendelea na safari yenu.” Ndipo wakasema: “Ni sawa. Unaweza kufanya kama ulivyosema.”  Kwa hiyo Abrahamu akaenda haraka hemani na kumwambia Sara: “Fanya haraka! Chukua vipimo vitatu* vya unga laini, ukande unga huo, na kuoka mikate.”  Kisha Abrahamu akakimbia kwenda kwenye mifugo, akachagua ng’ombe dume mchanga, mzuri na laini. Akampa mtumishi wake, naye akafanya haraka kumtayarisha.  Halafu akachukua siagi na maziwa na huyo ng’ombe dume mchanga ambaye alikuwa amemtayarisha, akaviweka vyakula hivyo mbele yao. Kisha akasimama kando yao chini ya mti walipokuwa wakila.+  Wakamuuliza: “Yuko wapi Sara mke wako?”+ Akajibu: “Yumo humu hemani.” 10  Kwa hiyo mmoja wao akasema: “Kwa hakika nitarudi kwako mwaka ujao wakati huuhuu, na tazama! mke wako Sara atakuwa na mwana.”+ Sasa Sara alikuwa akisikiliza kwenye mlango wa hema uliokuwa nyuma ya mtu huyo. 11  Abrahamu na Sara walikuwa wazee, umri wao ulikuwa umesonga.+ Sara alikuwa amepita umri wa kuzaa watoto.*+ 12  Kwa hiyo Sara akaanza kucheka kimoyomoyo na kusema: “Nikiwa mkongwe hivi na bwana wangu akiwa amezeeka, ninaweza kweli kupata shangwe hii?”+ 13  Kisha Yehova akamwambia Abrahamu: “Kwa nini Sara amecheka na kusema, ‘Je, kweli nitazaa mtoto nikiwa nimezeeka?’ 14  Je, kuna jambo lolote lisilowezekana kwa Yehova?+ Nitarudi kwako mwaka ujao wakati huuhuu, na Sara atakuwa na mwana.” 15  Lakini Sara akakana akisema, “Mimi sikucheka!” kwa maana aliogopa. Ndipo Mungu akamwambia: “Hakika! Ulicheka.” 16  Wanaume hao waliposimama ili kuondoka Abrahamu aliwasindikiza, wakatazama chini kuelekea Sodoma.+ 17  Yehova akasema: “Kwa nini nimfiche Abrahamu jambo ninalokusudia kufanya?+ 18  Kwa hakika Abrahamu atakuwa taifa kubwa na lenye nguvu, na mataifa yote ya dunia yatabarikiwa* kupitia yeye.+ 19  Kwa maana sasa nimemjua ili awaamuru watoto wake na nyumba yake baada yake kushika njia ya Yehova kwa kutenda yaliyo sawa na ya haki,+ ili Yehova atimize mambo aliyoahidi kumhusu Abrahamu.” 20  Kisha Yehova akasema: “Kilio dhidi ya Sodoma na Gomora kwa kweli ni kikubwa,+ na dhambi yao ni nzito sana.+ 21  Nitashuka chini ili nione kama mambo wanayotenda yanalingana na kilio kilichonifikia. Na kama sivyo, nitajua.”+ 22  Kisha wanaume hao wakatoka huko na kuelekea Sodoma, lakini Yehova+ akabaki na Abrahamu. 23  Kisha Abrahamu akamkaribia na kumuuliza: “Je, kweli utamfagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu?+ 24  Tuseme kuna watu 50 waadilifu katika jiji hilo. Je, kweli utawafagilia mbali na hutalisamehe jiji hilo kwa ajili ya waadilifu hao 50 waliomo? 25  Ni jambo usiloweza kuwazia kumuua mwadilifu pamoja na mwovu hivi kwamba mtu mwadilifu apatwe na jambo lilelile linalompata mwovu!+ Ni jambo usiloweza kuwazia.+ Je, Mwamuzi wa dunia yote hatatenda jambo la haki?”+ 26  Kisha Yehova akasema: “Nikipata watu 50 waadilifu katika jiji la Sodoma, nitalisamehe jiji lote kwa ajili yao.” 27  Lakini Abrahamu akasema tena: “Tafadhali, nimethubutu kuzungumza nawe, Yehova, ijapokuwa mimi ni mavumbi na majivu. 28  Tuseme waadilifu hao 50 wapungue watano. Je, utaliangamiza jiji lote kwa sababu ya hao watano?” Akajibu: “Sitaliangamiza nikipata waadilifu 45 humo.”+ 29  Lakini kwa mara nyingine tena akamwambia: “Tuseme 40 wapatikane humo.” Akamjibu: “Sitaliangamiza kwa ajili ya hao 40.” 30  Lakini akaendelea kusema: “Tafadhali Yehova, usiwake hasira,+ niruhusu niendelee kuongea: Tuseme ni 30 tu wanaopatikana humo.” Akamjibu: “Sitaliangamiza nikipata 30 humo.” 31  Lakini akaendelea kusema: “Tafadhali, nimethubutu kuzungumza nawe, Yehova: Tuseme ni 20 tu wanaopatikana humo.” Mungu akamjibu: “Sitaliangamiza kwa ajili ya hao 20.” 32  Mwishowe akasema: “Tafadhali Yehova, usiwake hasira, lakini niruhusu niongee kwa mara ya mwisho: Tuseme ni kumi tu wanaopatikana humo.” Akamjibu: “Sitaliangamiza kwa ajili ya hao kumi.” 33  Yehova alipomaliza kuzungumza na Abrahamu, alienda zake+ na Abrahamu akarudi nyumbani kwake.

Maelezo ya Chini

Yaani, malaika aliyemwakilisha Yehova.
Tnn., “mtie nguvu mioyo yenu.”
Tnn., “vipimo vitatu vya sea.” Sea moja ilikuwa sawa na lita 7.33 (vibaba 6.66). Angalia Nyongeza B14.
Yaani, “Alikuwa ameacha kupata hedhi.”
Au “yatajipatia baraka.”