Mwanzo 21:1-34

  • Isaka azaliwa (1-7)

  • Ishmaeli amdhihaki Isaka (8, 9)

  • Hagari na Ishmaeli wafukuzwa (10-21)

  • Agano kati ya Abrahamu na Abimeleki (22-34)

21  Yehova akamkumbuka Sara kama alivyokuwa amesema, na Yehova akamtendea Sara jambo alilokuwa amemwahidi.+  Basi Sara akapata mimba+ Abrahamu akiwa mzee, akamzalia mwana wakati uleule ambao Mungu alikuwa amemwahidi Abrahamu.+  Abrahamu akamwita Isaka, mwana huyo ambaye Sara alikuwa amemzalia.+  Na Abrahamu akamtahiri Isaka mwanawe akiwa na umri wa siku nane, kama Mungu alivyokuwa amemwamuru.+  Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 100 Isaka mwanawe alipozaliwa.  Kisha Sara akasema: “Mungu ameniletea kicheko; kila mtu atakayesikia jambo hili atacheka pamoja nami.”*  Naye akaendelea kusema: “Ni nani angeweza kumwambia Abrahamu, ‘Kwa hakika Sara atanyonyesha watoto’? Hata hivyo, nimemzalia mwana katika uzee wake.”  Basi mtoto huyo akakua na kuachishwa kunyonya, Abrahamu akafanya karamu kubwa siku ambayo Isaka aliachishwa kunyonya.  Lakini Sara alikuwa akiona kwamba mwana ambaye Hagari+ Mmisri alimzalia Abrahamu, alikuwa akimdhihaki Isaka.+ 10  Kwa hiyo akamwambia Abrahamu: “Mfukuze kijakazi huyu na mwanawe, kwa maana mwana wa kijakazi huyu hatakuwa mrithi pamoja na mwanangu, pamoja na Isaka!”+ 11  Lakini jambo hilo alilomwambia Abrahamu kumhusu mwanawe, halikumpendeza kamwe Abrahamu.+ 12  Kisha Mungu akamwambia Abrahamu: “Usikasirishwe na jambo ambalo Sara anakuambia kuhusu mvulana huyo na kuhusu kijakazi wako. Msikilize,* kwa maana ule utakaoitwa uzao wako utapitia* kwa Isaka.+ 13  Na kuhusu mwana wa kijakazi wako,+ nitatokeza pia taifa kutoka kwake,+ kwa sababu yeye ni uzao wako.”* 14  Basi Abrahamu akaamka asubuhi na mapema, akachukua mkate na kiriba cha ngozi chenye maji na kumpa Hagari. Akamtwika vitu hivyo begani na kumwambia aende zake pamoja na mwanawe.+ Kwa hiyo Hagari akaondoka na kutangatanga katika nyika ya Beer-sheba.+ 15  Mwishowe maji yaliyokuwa ndani ya kiriba hicho cha ngozi yakaisha, naye akamsukuma mvulana huyo chini ya kichaka fulani. 16  Kisha akaenda na kuketi chini peke yake, karibu umbali ambao mshale hufika unaporushwa kwa upinde, kwa maana alisema: “Sitaki kumwona mvulana huyu akifa.” Kwa hiyo akaketi chini umbali fulani na kuanza kulia kwa sauti na kutokwa na machozi. 17  Ndipo Mungu akasikia sauti ya mvulana huyo,+ na malaika wa Mungu akamwita Hagari kutoka mbinguni na kumwambia:+ “Hagari, kwa nini unalia? Usiogope, kwa sababu Mungu amesikia sauti ya mwanao pale alipo. 18  Simama, mwinue mwanao na umshike kwa mkono wako, kwa maana nitamfanya kuwa taifa kubwa.”+ 19  Kisha Mungu akamfungua macho, naye akaona kisima cha maji, akaenda na kukijaza maji kile kiriba cha ngozi na kumnywesha mwanawe. 20  Na Mungu alikuwa pamoja na mvulana huyo+ alipoendelea kukua. Aliishi nyikani, akawa mpiga mishale. 21  Alienda kuishi katika nyika ya Parani,+ na mama yake akamtafutia mke kutoka katika nchi ya Misri. 22  Wakati huo Abimeleki akiwa pamoja na Fikoli mkuu wa jeshi lake akamwambia Abrahamu: “Mungu yuko pamoja nawe katika kila jambo unalofanya.+ 23  Basi sasa niapie hapa mbele za Mungu kwamba hutanitendea kwa udanganyifu mimi na watoto wangu na wazao wangu, na kwamba utanitendea kwa upendo mshikamanifu mimi na wakaaji wa nchi ambayo umekuwa ukiishi, kama nilivyokutendea kwa upendo mshikamanifu.”+ 24  Kwa hiyo Abrahamu akasema: “Ninaapa hivyo.” 25  Hata hivyo, Abrahamu akamlalamikia Abimeleki kuhusu kisima cha maji ambacho watumishi wa Abimeleki walikuwa wamechukua kwa nguvu.+ 26  Abimeleki akamwambia: “Sijui ni nani aliyefanya jambo hilo; hukuniambia jambo hilo, leo ndio ninasikia habari hizo.” 27  Ndipo Abrahamu akachukua kondoo na ng’ombe na kumpa Abimeleki, na wote wawili wakafanya agano. 28  Abrahamu alipowatenga wanakondoo jike saba kutoka katika kundi, 29  Abimeleki akamuuliza Abrahamu: “Kwa nini umewatenga hawa wanakondoo jike saba?” 30  Akamjibu: “Pokea hawa wanakondoo jike saba kutoka mkononi mwangu kama ushahidi kwamba mimi ndiye niliyechimba kisima hiki.” 31  Ndiyo maana alipaita mahali hapo Beer-sheba,*+ kwa sababu wote wawili walikuwa wamekula kiapo mahali hapo. 32  Kwa hiyo wakafanya agano+ huko Beer-sheba, kisha Abimeleki akaondoka pamoja na Fikoli mkuu wa jeshi lake, wakarudi katika nchi ya Wafilisti.+ 33  Baada ya hayo Abrahamu akapanda mti wa mwesheli huko Beer-sheba, na huko akaliitia jina la Yehova,+ Mungu wa milele.+ 34  Naye Abrahamu akaishi* katika nchi ya Wafilisti kwa muda mrefu.*+

Maelezo ya Chini

Au labda, “atanicheka.”
Tnn., “Isikilize sauti yake.”
Tnn., “ile itakayoitwa mbegu yako itapitia.”
Tnn., “mbegu yako.”
Maana yake “Kisima cha Kile Kiapo; Kisima cha Wale Saba.”
Au “akaishi akiwa mgeni.”
Tnn., “kwa siku nyingi.”