Mwanzo 31:1-55

  • Yakobo aenda kwa siri Kanaani (1-18)

  • Labani amfikia Yakobo (19-35)

  • Agano kati ya Yakobo na Labani (36-55)

31  Baada ya muda Yakobo akawasikia wana wa Labani wakisema: “Yakobo amechukua kila kitu cha baba yetu, amepata utajiri huu wote kutokana na mali+ ya baba yetu.”  Kila mara Yakobo alipomtazama Labani, alitambua kwamba mtazamo wake kumwelekea ulikuwa umebadilika.+  Hatimaye Yehova akamwambia Yakobo: “Rudi kwenye nchi ya baba zako na kwa watu wako wa ukoo,+ nami nitaendelea kuwa pamoja nawe.”  Kisha Yakobo akatuma ujumbe kwa Raheli na Lea na kuwaambia waje malishoni alikokuwa akichunga mifugo yake,  akawaambia: “Nimeona kwamba mtazamo wa baba yenu kunielekea umebadilika,+ lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami.+  Ninyi wenyewe mnajua kwa hakika kwamba nimemtumikia baba yenu kwa nguvu zangu zote.+  Na baba yenu amejaribu kunidanganya na kubadili mshahara wangu mara kumi; lakini Mungu hajamruhusu anidhuru.  Kila mara aliposema, ‘Wanyama wenye madoadoa watakuwa mshahara wako,’ kundi lote lilizaa wanyama wenye madoadoa; na aliposema, ‘Wanyama wenye mistarimistari watakuwa mshahara wako,’ kundi lote lilizaa wanyama wenye mistarimistari.+  Kwa hiyo Mungu akaendelea kuchukua mifugo ya baba yenu na kunipa. 10  Siku moja wanyama walipopata joto la kupandana, niliinua macho yangu na kuona katika ndoto kwamba mbuzi dume waliokuwa wakipanda majike walikuwa wenye mistarimistari, mabakamabaka, na madoadoa.+ 11  Kisha malaika wa Mungu wa kweli akaniita katika ndoto hiyo, ‘Yakobo!’ nikajibu, ‘Mimi hapa.’ 12  Akaniambia, ‘Tafadhali inua macho yako, uone kwamba mbuzi dume wote wanaowapanda majike wana mistarimistari, mabakamabaka, na madoadoa, kwa maana nimeona mambo yote ambayo Labani anakutendea.+ 13  Mimi ni Mungu wa kweli wa Betheli,+ mahali ambapo uliitia nguzo mafuta na kuniwekea nadhiri.+ Sasa inuka, ondoka katika nchi hii, urudi kwenye nchi uliyozaliwa.’”+ 14  Ndipo Raheli na Lea wakamuuliza: “Je, kuna urithi wowote uliobaki kwa ajili yetu katika nyumba ya baba yetu? 15  Je, haoni kwamba sisi ni wageni kwa sababu ametuuza na amekuwa akitumia pesa alizopewa kwa ajili yetu?+ 16  Utajiri wote ambao Mungu amechukua kutoka kwa baba yetu ni wetu na wa watoto wetu.+ Basi sasa, fanya kila kitu ambacho Mungu amekuambia ufanye.”+ 17  Kwa hiyo Yakobo akainuka na kuwapandisha watoto wake na wake zake juu ya ngamia,+ 18  naye akaanza kuchukua mifugo yake yote na mali zote alizokusanya+ huko Padan-aramu, akaanza safari ya kwenda kwa Isaka baba yake katika nchi ya Kanaani.+ 19  Sasa Labani alikuwa ameenda kuwakata manyoya kondoo wake, Raheli akaiba sanamu za terafimu*+ za baba yake.+ 20  Isitoshe, Yakobo akamshinda akili Labani, Mwaramu, kwa maana hakuwa amemwambia kwamba ataondoka. 21  Akatoroka na kuvuka ule Mto,*+ yeye pamoja na vyote alivyokuwa navyo. Kisha akaelekea kwenye eneo lenye milima la Gileadi.+ 22  Siku ya tatu, Labani akaambiwa kwamba Yakobo ametoroka. 23  Basi Labani akawachukua ndugu zake* na kumfuatia Yakobo kwa muda wa siku saba na kumfikia katika eneo lenye milima la Gileadi. 24  Ndipo Mungu akamtokea Labani Mwaramu+ katika ndoto wakati wa usiku+ na kumwambia: “Uwe mwangalifu kuhusu mambo utakayomwambia Yakobo, yawe mema au mabaya.”+ 25  Basi Labani akamkaribia Yakobo alipokuwa amepiga hema lake mlimani; Labani alikuwa amepiga kambi na ndugu zake kwenye eneo lenye milima la Gileadi. 26  Labani akamuuliza Yakobo: “Umefanya nini? Kwa nini umenichezea akili na kuwachukua mabinti wangu kama mateka waliochukuliwa kwa upanga? 27  Kwa nini ulitoroka kwa siri, ukanichezea akili badala ya kuniambia? Ikiwa ungeniambia, ningekuaga kwa shangwe na nyimbo, kwa tari na kinubi. 28  Lakini hukunipa nafasi ya kuwabusu wajukuu* wangu na mabinti wangu. Umetenda kipumbavu. 29  Nina uwezo wa kuwadhuru, lakini Mungu wa baba yenu aliongea nami usiku wa kuamkia leo, akaniambia, ‘Uwe mwangalifu kuhusu mambo utakayomwambia Yakobo, yawe mema au mabaya.’+ 30  Sasa umeondoka kwa sababu umekuwa ukitamani sana kurudi kwenye nyumba ya baba yako, lakini kwa nini umeiba miungu yangu?”+ 31  Yakobo akamjibu Labani: “Ni kwa sababu niliogopa, kwa maana nilisema moyoni mwangu, ‘Huenda ukaninyang’anya kwa nguvu mabinti wako.’ 32  Yeyote utakayempata na miungu yako, atauawa. Pekua vitu nilivyo navyo mbele ya hawa ndugu zetu, uchukue chochote kilicho chako.” Lakini Yakobo hakujua kwamba Raheli alikuwa ameiba miungu hiyo. 33  Kwa hiyo Labani akaingia katika hema la Yakobo na hema la Lea na hema la wale vijakazi wawili,+ lakini hakuipata. Kisha akatoka katika hema la Lea na kuingia katika hema la Raheli. 34  Raheli alikuwa amechukua sanamu hizo za terafimu na kuziweka ndani ya kikapu cha wanawake kilicho kwenye matandiko ya ngamia na kuzikalia. Basi Labani alizitafuta kabisa katika hema lote lakini hakuzipata. 35  Ndipo Raheli akamwambia baba yake: “Bwanangu, usikasirike, kwa sababu siwezi kusimama mbele yako, kwa maana niko katika siku zangu za hedhi.”*+ Kwa hiyo akaendelea kuzitafuta kwa makini lakini hakuzipata sanamu hizo za terafimu.+ 36  Ndipo Yakobo akakasirika na kuanza kumshutumu Labani. Akamuuliza Labani: “Nimefanya kosa gani, nimetenda dhambi gani hivi kwamba unanifuatia kwa bidii hivi? 37  Sasa kwa kuwa umepekua kabisa vitu vyangu vyote, umepata nini cha nyumba yako? Kiweke hapa mbele ya ndugu zangu na ndugu zako, waache waamue ni nani mwenye kosa kati yetu. 38  Kwa miaka hii 20 ambayo nimekaa nawe, mimba za kondoo wako na mbuzi wako hazikuharibika,+ wala sijawahi kula kondoo dume wa kundi lako. 39  Sijawahi kukuletea mnyama yeyote aliyeraruliwa na mnyama wa mwituni.+ Mimi mwenyewe nililipia hasara hiyo. Ulidai malipo kutoka kwangu kwa ajili ya mnyama yeyote aliyeibiwa mchana au usiku. 40  Jua lilinichoma wakati wa mchana na baridi ilinipiga usiku, na macho yangu yalipoteza usingizi.+ 41  Ilikuwa hivyo kwa miaka 20 niliyokaa nyumbani mwako. Nimekutumikia kwa miaka 14 ili niwapate mabinti wako wawili na kuchunga mifugo yako kwa miaka 6, nawe ulibadili tena na tena mshahara wangu mara kumi.+ 42  Ikiwa Mungu wa baba yangu,+ Mungu wa Abrahamu, Yule ambaye Isaka anamwogopa,*+ hangekuwa pamoja nami, sasa ungeniambia niende zangu mikono mitupu. Mungu ameyaona mateso yangu na kazi ngumu ya mikono yangu, na ndiyo sababu alikukaripia usiku wa kuamkia leo.”+ 43  Labani akamwambia Yakobo: “Mabinti hawa ni mabinti wangu na watoto hawa ni watoto wangu na wanyama hawa ni wanyama wangu, na kila kitu unachoona hapa ni changu na cha mabinti wangu. Ni jambo gani ninaloweza kufanya leo kuwadhuru mabinti hawa au kuwadhuru watoto wao ambao wamewazaa? 44  Sasa njoo, tufanye agano kati yetu, wewe na mimi, nalo litakuwa ushahidi kati yetu.” 45  Basi Yakobo akachukua jiwe na kulisimamisha kama nguzo.+ 46  Kisha Yakobo akawaambia ndugu zake: “Okoteni mawe!” Basi wakaokota mawe na kutengeneza rundo la mawe. Halafu wakala chakula juu ya rundo hilo la mawe. 47  Na Labani akaanza kuliita rundo hilo Yegar-sahadutha,* lakini Yakobo akaliita Galeedi.* 48  Ndipo Labani akasema: “Rundo hili la mawe ni ushahidi kati yangu mimi na wewe leo.” Ndiyo sababu aliliita Galeedi,+ 49  na Mnara wa Mlinzi, kwa sababu alisema: “Yehova na awe mlinzi kati yangu mimi na wewe tunapokuwa hatuonani. 50  Ukiwatesa mabinti wangu na kuanza kuoa wake wengine kuongezea mabinti wangu, hata mwanadamu asipoona jambo hilo, kumbuka kwamba Mungu atakuwa shahidi kati yangu mimi na wewe.” 51  Labani akaendelea kumwambia Yakobo: “Hili hapa ni rundo la mawe, na hii hapa ni nguzo ambayo nimesimamisha kati yangu mimi na wewe. 52  Rundo hili la mawe ni ushahidi, na nguzo hii pia ni ushahidi+ kwamba sitapita rundo hili la mawe ili kuja kukudhuru, nawe hutapita rundo hili la mawe na nguzo hii ili kuja kunidhuru. 53  Mungu wa Abrahamu+ na Mungu wa Nahori, Mungu wa baba yao, na awe mwamuzi kati yetu.” Basi Yakobo akaapa kwa jina la Yule ambaye Isaka baba yake alimwogopa.*+ 54  Kisha Yakobo akatoa dhabihu mlimani na kuwaalika ndugu zake wale chakula.* Wakala na kulala mlimani usiku huo. 55  Hata hivyo, Labani akaamka asubuhi na mapema, akawabusu wajukuu wake+ na mabinti zake na kuwabariki.+ Kisha Labani akaondoka, akarudi nyumbani.+

Maelezo ya Chini

Au “miungu ya familia; sanamu.”
Yaani, Mto Efrati.
Au “watu wake wa ukoo.”
Tnn., “wana.”
Tnn., “desturi ya wanawake imenijia.”
Tnn., “woga wa Isaka.”
Neno la Kiaramu linalomaanisha “Rundo la Ushahidi.”
Neno la Kiebrania linalomaanisha “Rundo la Ushahidi.”
Tnn., “kwa woga wa Isaka baba yake.”
Tnn., “mkate.”