Mwanzo 32:1-32

  • Malaika wakutana na Yakobo (1, 2)

  • Yakobo ajitayarisha kukutana na Esau (3-23)

  • Yakobo apigana mweleka na malaika (24-32)

    • Yakobo apewa jina jipya, Israeli (28)

32  Kisha Yakobo akaendelea na safari yake, na malaika wa Mungu wakakutana naye.  Mara tu alipowaona, Yakobo akasema: “Hii ni kambi ya Mungu!” Kwa hiyo akapaita mahali hapo Mahanaimu.*  Kisha Yakobo akawatuma wajumbe wamtangulie kwenda kwa Esau ndugu yake katika nchi ya Seiri,+ katika eneo* la Edomu,+  akawaamuru hivi: “Hivi ndivyo mtakavyomwambia bwana wangu, Esau, ‘Mtumishi wako Yakobo anasema hivi: “Nimeishi* na Labani kwa muda mrefu mpaka sasa.+  Nami nimepata ng’ombe dume, punda, kondoo, na watumishi wa kiume na wa kike,+ nami ninakutumia ujumbe huu bwana wangu, ili nipate kibali machoni pako.”’”  Baada ya muda wajumbe hao wakarudi kwa Yakobo na kumwambia: “Tulikutana na ndugu yako Esau, naye yuko njiani, anakuja kukutana nawe akiwa na wanaume 400.”+  Ndipo Yakobo akaogopa sana na kushikwa na wasiwasi.+ Basi akawagawa katika kambi mbili watu aliokuwa nao, na pia ng’ombe, ngamia, na mifugo mingine.  Akasema: “Esau akiishambulia kambi moja, kambi nyingine itaponyoka.”  Kisha Yakobo akasema: “Ee Mungu wa baba yangu Abrahamu na Mungu wa baba yangu Isaka, Ee Yehova, wewe unayeniambia, ‘Rudi kwenye nchi yako na kwa watu wako wa ukoo, nami nitakutendea mema,’+ 10  mimi sistahili upendo wote mshikamanifu na uaminifu wote ambao umenitendea mimi, mtumishi wako,+ kwa maana nilivuka mto huu wa Yordani nikiwa na fimbo yangu tu lakini sasa nina kambi mbili.+ 11  Nakuomba uniokoe+ kutoka mikononi mwa ndugu yangu Esau, kwa maana naogopa kwamba anaweza kuja kunishambulia mimi,+ na pia akina mama na watoto wao. 12  Lakini uliniambia: ‘Hakika nitakutendea mema, nami nitaufanya uzao* wako uwe mwingi kama chembe za mchanga wa bahari, zisizoweza kuhesabiwa kwa sababu ni nyingi sana.’”+ 13  Naye Yakobo akalala huko usiku huo. Kisha akachukua baadhi ya mali zake ili ampe zawadi Esau ndugu yake:+ 14  mbuzi jike 200, mbuzi dume 20, kondoo jike 200, kondoo dume 20, 15  ngamia 30 wanaonyonyesha, ng’ombe 40, ng’ombe dume 10, punda jike 20, na punda dume 10 waliokomaa.+ 16  Akawapa watumishi wake kundi moja baada ya lingine, akawaambia: “Nitangulieni mvuke kabla yangu, nanyi mwache nafasi kati ya kundi moja na kundi lingine.” 17  Pia akamwamuru hivi yule wa kwanza: “Ikiwa Esau ndugu yangu atakutana nawe na kukuuliza, ‘Wewe ni mtumishi wa nani, unaenda wapi, na wanyama hawa walio mbele yako ni wa nani?’ 18  utamwambia, ‘Ni mali ya mtumishi wako Yakobo. Ni zawadi aliyokutumia wewe, bwana wangu Esau,+ na tazama! yeye mwenyewe yuko nyuma anatufuata.’” 19  Akamwamuru hivi pia mtumishi wa pili, wa tatu, na wale wote waliokuwa wakiyafuata makundi hayo: “Mkikutana na Esau, mtamwambia maneno hayohayo. 20  Vilevile mtamwambia, ‘Mtumishi wako Yakobo yuko nyuma anatufuata.’” Kwa maana Yakobo alisema moyoni mwake: ‘Nikimtumia zawadi kwanza+ huenda nikamtuliza, na huenda atanipokea kwa fadhili nitakapokutana naye baadaye.’ 21  Kwa hiyo zawadi hizo zikavushwa na kupelekwa kwanza, lakini yeye mwenyewe akalala kambini usiku huo. 22  Baadaye usiku huo, akaamka na kuwachukua wake zake wawili+ na vijakazi wake wawili+ na wanawe wachanga 11 na kuvuka kivuko cha Yaboki.+ 23  Basi akawachukua na kuwavusha kwenye kijito,* akavusha pia vitu vingine vyote alivyokuwa navyo. 24  Mwishowe Yakobo akabaki peke yake. Kisha mwanamume fulani akaanza kupigana naye mweleka mpaka kulipopambazuka.+ 25  Mwanamume huyo alipoona kwamba hajamshinda Yakobo, akamgusa kiungio cha nyonga; na kiungio cha nyonga ya Yakobo kikateguka alipokuwa akipigana naye mweleka.+ 26  Kisha mwanamume huyo akasema: “Niache niende, kwa maana kunapambazuka.” Yakobo akamwambia: “Sitakuacha uende mpaka unibariki.”+ 27  Basi akamuuliza: “Jina lako ni nani?” akajibu: “Yakobo.” 28  Kisha akamwambia: “Jina lako halitakuwa tena Yakobo bali Israeli,*+ kwa maana umepambana na Mungu+ na wanadamu na hatimaye umeshinda.” 29  Naye Yakobo akamuuliza: “Tafadhali, niambie jina lako.” Hata hivyo, mwanamume huyo akamwambia: “Kwa nini unataka kujua jina langu?”+ Halafu akambariki huko. 30  Basi Yakobo akapaita mahali hapo Penieli,*+ kwa sababu alisema, “Nimemwona Mungu uso kwa uso, lakini uhai wangu umeokolewa.”*+ 31  Na jua likachomoza mara tu Yakobo alipopita karibu na Penueli,* lakini alikuwa akichechemea kwa sababu ya nyonga yake.+ 32  Ndiyo maana tangu siku hiyo Waisraeli hawajazoea kula kano ya paja,* iliyo kwenye kiungio cha nyonga, kwa sababu mwanamume huyo aligusa kiungio cha nyonga ya Yakobo karibu na kano ya paja.

Maelezo ya Chini

Maana yake “Kambi Mbili.”
Tnn., “shamba.”
Au “Nimeishi kama mgeni.”
Tnn., “mbegu.”
Au “bonde la mto; korongo.”
Maana yake “Anayepambana na (Anayestahimili Pamoja na) Mungu” au “Mungu Hupambana.”
Maana yake “Uso wa Mungu.”
Au “nafsi yangu imehifadhiwa.”
Au “Penieli.”
Tnn., “kano ya mshipa wa paja.”