Mwanzo 35:1-29

  • Yakobo aondoa miungu ya kigeni (1-4)

  • Yakobo arudi Betheli (5-15)

  • Benjamini azaliwa; Raheli afa (16-20)

  • Wana 12 wa Israeli (21-26)

  • Kifo cha Isaka (27-29)

35  Baada ya hayo Mungu akamwambia Yakobo: “Ondoka, nenda Betheli+ ukaishi huko, na unijengee madhabahu mimi Mungu wa kweli, niliyekutokea ulipokuwa ukimkimbia ndugu yako Esau.”+  Basi Yakobo akawaambia watu wa nyumba yake na wote waliokuwa pamoja naye: “Ondoeni kabisa miungu ya kigeni iliyo kati yenu,+ na mjisafishe wenyewe na kubadili mavazi yenu,  na acheni tuondoke twende Betheli. Huko nitamjengea madhabahu Mungu wa kweli, aliyenijibu katika siku yangu ya taabu na ambaye amekuwa pamoja nami kila mahali nilipoenda.”*+  Basi wakampa Yakobo miungu yote ya kigeni waliyokuwa nayo na vipuli walivyovaa masikioni, kisha Yakobo akavifukia* chini ya mti mkubwa uliokuwa karibu na Shekemu.  Walipokuwa wakisafiri, hofu ya Mungu iliyakumba majiji yaliyowazunguka, kwa hiyo wakaaji wake hawakuwafuatia wana wa Yakobo.  Hatimaye Yakobo akafika Luzi,+ yaani, Betheli, katika nchi ya Kanaani, pamoja na watu wote waliokuwa naye.  Akajenga madhabahu huko na kupaita mahali hapo El-betheli,* kwa sababu Mungu wa kweli alikuwa amemtokea mahali hapo alipomkimbia ndugu yake.+  Baadaye Debora,+ mlezi wa Rebeka, akafa na kuzikwa chini ya mwaloni karibu na Betheli. Basi akauita mwaloni huo Alon-bakuthi.*  Mungu akamtokea Yakobo tena alipokuwa akitoka Padan-aramu, akambariki. 10  Mungu akamwambia: “Jina lako ni Yakobo.+ Hutaitwa tena Yakobo, jina lako litakuwa Israeli.” Naye akaanza kumwita Israeli.+ 11  Mungu akaendelea kumwambia: “Mimi ni Mungu Mweza-Yote.+ Zaa uwe na watoto wengi. Mataifa na kusanyiko la mataifa litatoka kwako,+ na wafalme watatoka kwako.*+ 12  Na nchi niliyompa Abrahamu na Isaka, nitakupa wewe na uzao wako* baada yako.”+ 13  Kisha Mungu akapanda na kumwacha mahali alipoongea naye. 14  Basi Yakobo akasimamisha nguzo mahali hapo alipoongea naye, nguzo ya mawe, naye akamimina toleo la kinywaji juu yake na pia akamimina mafuta juu yake.+ 15  Na Yakobo akaendelea kupaita mahali hapo ambapo Mungu alikuwa ameongea naye, Betheli.+ 16  Kisha wakaondoka Betheli. Na walipokuwa umbali fulani kabla ya kufika Efrathi, Raheli akaanza kuzaa, na uchungu wa kuzaa ulikuwa mkali sana. 17  Lakini alipokuwa aking’ang’ana kuzaa, mkunga akamwambia: “Usiogope, kwa maana utamzaa mwana huyu pia.”+ 18  Uhai wake ulipokuwa ukitoka (kwa kuwa alikuwa akifa), akamwita mwana huyo Ben-oni,* lakini baba yake akamwita Benjamini.*+ 19  Kwa hiyo Raheli akafa na kuzikwa njiani kuelekea Efrathi, yaani, Bethlehemu.+ 20  Yakobo akasimamisha nguzo juu ya kaburi lake; hiyo ndiyo nguzo ya kaburi la Raheli mpaka leo hii. 21  Kisha Israeli akaendelea na safari na kupiga hema lake umbali fulani mbele ya mnara wa Ederi. 22  Siku moja, Israeli alipokuwa akiishi katika nchi hiyo, Rubeni alienda na kulala na Bilha suria wa baba yake, naye Israeli akasikia habari hizo.+ Basi Yakobo alikuwa na wana 12. 23  Wana wa Lea walikuwa Rubeni,+ mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, kisha Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, na Zabuloni. 24  Wana wa Raheli walikuwa Yosefu na Benjamini. 25  Na wana wa Bilha kijakazi wa Raheli walikuwa Dani na Naftali. 26  Na wana wa Zilpa kijakazi wa Lea walikuwa Gadi na Asheri. Hao ndio wana wa Yakobo waliozaliwa Padan-aramu. 27  Hatimaye Yakobo akafika mahali ambapo Isaka baba yake alikuwa kule Mamre,+ Kiriath-arba, yaani, Hebroni, ambako Abrahamu na pia Isaka waliishi wakiwa wageni.+ 28  Isaka aliishi miaka 180.+ 29  Kisha Isaka akakata pumzi na kufa, akazikwa pamoja na watu wake,* baada ya kuishi maisha marefu na yenye kuridhisha;* na Esau na Yakobo wanawe wakamzika.+

Maelezo ya Chini

Au “katika njia niliyotembea.”
Au “akavificha.”
Maana yake “Mungu wa Betheli.”
Maana yake “Mwaloni wa Kilio.”
Tnn., “watatoka katika kiuno chako.”
Tnn., “mbegu yako.”
Maana yake “Mwana wa Mkono wa Kulia.”
Maana yake “Mwana wa Maombolezo Yangu.”
Tnn., “Akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Tnn., “akiwa amezeeka na akiwa amejaa siku.”