Mwanzo 45:1-28

  • Yosefu ajitambulisha (1-15)

  • Ndugu za Yosefu warudi kumchukua Yakobo (16-28)

45  Ndipo Yosefu akashindwa kujizuia mbele ya watumishi wake wote.+ Basi akasema kwa sauti kubwa: “Mwondoeni kila mtu mbele yangu!” Hakuna yeyote aliyebaki pamoja na Yosefu alipokuwa akijitambulisha kwa ndugu zake.+  Kisha akaanza kulia kwa sauti kubwa hivi kwamba Wamisri wakamsikia na watu wa nyumba ya Farao wakamsikia.  Mwishowe Yosefu akawaambia ndugu zake: “Mimi ni Yosefu. Je, baba yangu angali hai?” Lakini ndugu zake wakashindwa kabisa kumjibu, kwa sababu walishtuka sana kusikia hivyo.  Basi Yosefu akawaambia ndugu zake: “Tafadhali, nikaribieni.” Basi wakamkaribia. Kisha akawaambia: “Mimi ni Yosefu ndugu yenu, mliyemuuza Misri.+  Lakini sasa msikasirike wala kulaumiana kwa kuniuza huku; kwa sababu Mungu alinituma huku niwatangulie ili kuokoa uhai.+  Huu ni mwaka wa pili wa njaa kali nchini,+ na bado kuna miaka mitano ambayo watu hawataweza kulima wala kuvuna.  Lakini Mungu alinituma niwatangulie ili niwahifadhie ninyi wazao watakaobaki+ duniani* na ili mwendelee kuwa hai kupitia ukombozi mkubwa.  Hivyo basi, si ninyi mlionituma hapa, bali ni Mungu wa kweli, ili aniweke kuwa mshauri mkuu* wa Farao na msimamizi wa nyumba yake yote na mtawala wa nchi yote ya Misri.+  “Rudini upesi kwa baba yangu, mkamwambie, ‘Mwana wako Yosefu amesema hivi: “Mungu ameniweka kuwa msimamizi wa nchi yote ya Misri.+ Shuka uje kwangu. Usikawie.+ 10  Utaishi katika nchi ya Gosheni,+ utakuwa karibu nami—wewe, wana wako, wajukuu wako, makundi yako, mifugo yako, na kila kitu ulicho nacho. 11  Nitakupa chakula huko, kwa maana bado kuna miaka mitano ya njaa kali.+ La sivyo, utakuwa maskini, wewe na nyumba yako na kila kitu ulicho nacho.’” 12  Ninyi pamoja na ndugu yangu Benjamini mnajionea wenyewe kwamba kwa kweli ni mimi ninayezungumza nanyi.+ 13  Kwa hiyo mnapaswa kumwambia baba yangu kuhusu utukufu wangu wote nchini Misri na kila kitu mlichoona. Sasa fanyeni haraka mkamteremshe huku baba yangu.” 14  Kisha akamkumbatia* Benjamini ndugu yake na kuanza kulia, naye Benjamini akalia huku akiwa amemkumbatia shingoni.+ 15  Akawabusu ndugu zake wote na kuwalilia, kisha ndugu zake wakaongea naye. 16  Habari hizi zikafika katika nyumba ya Farao: “Ndugu za Yosefu wamekuja!” Habari hizo zikamfurahisha Farao na watumishi wake. 17  Basi Farao akamwambia Yosefu: “Waambie ndugu zako, ‘Fanyeni hivi: Watwikeni mizigo wanyama wenu wanaobeba mizigo, mwende katika nchi ya Kanaani, 18  mkamchukue baba yenu na familia zenu mje kwangu. Nitawapa vitu vizuri vya nchi ya Misri, nanyi mtakula* sehemu bora kabisa ya* nchi.+ 19  Nami nakuamuru uwaambie:+ ‘Fanyeni hivi: Chukueni magari ya kukokotwa+ kutoka katika nchi ya Misri ya kuwabeba watoto wenu na wake zenu, nanyi mnapaswa kutumia gari moja kumleta baba yenu.+ 20  Msijali kuhusu mali zenu,+ kwa sababu sehemu bora katika nchi yote ya Misri ni yenu.’” 21  Basi wana wa Israeli wakafanya hivyo, naye Yosefu akawapa magari ya kukokotwa kama Farao alivyoamuru, pia akawapa vyakula kwa ajili ya safari. 22  Akampa kila mmoja wao nguo ya kubadili, lakini akampa Benjamini vipande 300 vya fedha na nguo tano za kubadili.+ 23  Naye akamtumia baba yake vitu vifuatavyo: punda kumi waliobeba vitu vizuri vya Misri na punda majike kumi waliobeba nafaka na mikate na vyakula vingine kwa ajili ya safari yake. 24  Basi akawaaga ndugu zake, na walipokuwa wakiondoka akawaambia: “Msigombane njiani.”+ 25  Basi wakapanda kutoka Misri na kufika katika nchi ya Kanaani kwa Yakobo baba yao. 26  Wakamwambia: “Yosefu angali hai, na ndiye mtawala wa nchi yote ya Misri!”+ Lakini moyo wake ukafa ganzi kwa sababu hakuwaamini.+ 27  Walipoendelea kumwambia mambo yote ambayo Yosefu aliwaambia na alipoona magari ya kukokotwa ambayo Yosefu aliwapa ili yambebe, roho ya Yakobo baba yao ikaanza kuhuika. 28  Israeli akasema kwa mshangao: “Inatosha! Yosefu mwanangu angali hai! Ni lazima niende kumwona kabla sijafa!”+

Maelezo ya Chini

Au “nchini.”
Tnn., “kuwa kama baba.”
Tnn., “akamwangukia shingoni.”
Au “mtaishi kwa kutegemea.”
Au “sehemu nono ya.”