Mwanzo 46:1-34

  • Yakobo na familia yake wahamia Misri (1-7)

  • Majina ya waliohamia Misri (8-27)

  • Yosefu na Yakobo wakutana Gosheni (28-34)

46  Basi Israeli akachukua kila kitu alichokuwa nacho* na kuondoka. Alipofika Beer-sheba,+ alimtolea dhabihu Mungu wa Isaka, baba yake.+  Kisha Mungu akaongea na Israeli katika maono usiku na kumwambia: “Yakobo, Yakobo!” naye akajibu: “Mimi hapa!”  Akamwambia: “Mimi ndiye Mungu wa kweli, Mungu wa baba yako.+ Usiogope kushuka kwenda Misri, kwa maana huko nitakufanya uwe taifa kubwa.+  Mimi mwenyewe nitashuka pamoja nawe Misri, na pia mimi mwenyewe nitakurudisha kutoka huko,+ na Yosefu atayafumba macho yako kwa mkono wake.”*+  Kisha Yakobo akaondoka Beer-sheba, na wanawe* wakamsafirisha Yakobo baba yao na watoto wao na wake zao katika magari ya kukokotwa ambayo Farao alikuwa amewapa ili yamsafirishe.  Wakachukua mifugo yao na mali zao, walizokuwa wamekusanya katika nchi ya Kanaani. Basi wakafika Misri, Yakobo na wazao wake wote.  Alienda Misri pamoja na wanawe na mabinti zake na wajukuu wake wa kiume na wa kike—wazao wake wote.  Sasa haya ndiyo majina ya wana wa Israeli waliokuja Misri,+ Yakobo na wanawe: mzaliwa wa kwanza wa Yakobo alikuwa Rubeni.+  Wana wa Rubeni walikuwa Hanoki, Palu, Hezroni, na Karmi.+ 10  Wana wa Simeoni+ walikuwa Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Zohari, na Shauli+ mwana wa mwanamke Mkanaani. 11  Wana wa Lawi+ walikuwa Gershoni, Kohathi, na Merari.+ 12  Wana wa Yuda+ walikuwa Eri, Onani, Shela,+ Perezi,+ na Zera.+ Lakini Eri na Onani walikufa katika nchi ya Kanaani.+ Wana wa Perezi walikuwa Hezroni na Hamuli.+ 13  Wana wa Isakari walikuwa Tola, Puva, Iobu, na Shimroni.+ 14  Wana wa Zabuloni+ walikuwa Seredi, Eloni, na Yahleeli.+ 15  Hao ndio wana wa Lea, aliomzalia Yakobo huko Padan-aramu, kutia ndani Dina binti yake.+ Wanawe na mabinti zake wote walikuwa 33. 16  Wana wa Gadi+ walikuwa Zifioni, Hagi, Shuni, Esboni, Eri, Arodi, na Areli.+ 17  Wana wa Asheri+ walikuwa Imna, Ishva, Ishvi, na Beria, na dada yao aliitwa Sera. Wana wa Beria walikuwa Heberi na Malkieli.+ 18  Hao ndio wana wa Zilpa,+ kijakazi ambaye Labani alimpa Lea binti yake. Alimzalia Yakobo wana hao: wote walikuwa 16. 19  Wana wa Raheli, mke wa Yakobo, walikuwa Yosefu+ na Benjamini.+ 20  Katika nchi ya Misri, Asenathi+ binti ya Potifera kuhani wa Oni,* alimzalia Yosefu wana hawa: Manase+ na Efraimu.+ 21  Wana wa Benjamini+ walikuwa Bela, Bekeri, Ashbeli, Gera,+ Naamani, Ehi, Roshi, Mupimu, Hupimu,+ na Ardi.+ 22  Hao ndio wana ambao Raheli alimzalia Yakobo: wote walikuwa 14. 23  Mwana* wa Dani+ alikuwa Hushimu.+ 24  Wana wa Naftali+ walikuwa Yahzeeli, Guni, Yezeri, na Shilemu.+ 25  Hao ndio wana wa Bilha, kijakazi ambaye Labani alimpa Raheli binti yake. Alimzalia Yakobo wana hao: wote walikuwa saba. 26  Wazao wote wa Yakobo walioenda Misri pamoja naye walikuwa 66, bila kuhesabu wake wa wanawe.+ 27  Wana wa Yosefu aliowazaa akiwa Misri walikuwa wawili. Watu wote wa nyumba ya Yakobo waliokuja Misri walikuwa 70.+ 28  Yakobo alimtuma Yuda+ atangulie na kumwambia Yosefu kwamba alikuwa njiani kwenda Gosheni. Walipofika katika nchi ya Gosheni,+ 29  Yosefu akaagiza gari lake litayarishwe, kisha akaenda kumpokea Israeli baba yake huko Gosheni. Alipokutana na baba yake, mara moja akamkumbatia* na kulia kwa muda.* 30  Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Sasa niko tayari kufa; nimeona uso wako na kujua kwamba ungali hai.” 31  Ndipo Yosefu akawaambia ndugu zake na watu wa nyumba ya baba yake: “Acheni nipande niende kumjulisha Farao,+ ‘Ndugu zangu na watu wa nyumba ya baba yangu waliokuwa katika nchi ya Kanaani wamekuja kwangu.+ 32  Watu hao ni wachungaji+ na wafugaji,+ nao wamekuja na kondoo wao na ng’ombe wao na kila kitu walicho nacho.’+ 33  Farao akiwaita na kuwauliza, ‘Mnafanya kazi gani?’ 34  Mnapaswa kumwambia, ‘Sisi watumishi wako tumekuwa wafugaji tangu tulipokuwa vijana mpaka sasa, sisi pamoja na mababu zetu,’+ ili mwishi katika nchi ya Gosheni,+ kwa sababu Wamisri wanamchukia kila mtu anayefuga kondoo.”+

Maelezo ya Chini

Au “watu wake wote.”
Yaani, atayafumba Yakobo atakapokufa.
Au “wana wa Israeli.”
Yaani, Heliopolisi.
Tnn., “Wana.” Huenda alikuwa na wana wengine ambao majina yao hayatajwi.
Tnn., “akamwangukia shingoni.”
Au “na kumlilia shingoni tena na tena.”