Mwanzo 50:1-26

  • Yosefu amzika Yakobo Kanaani (1-14)

  • Yosefu awahakikishia ndugu zake kwamba amewasamehe (15-21)

  • Siku za mwisho za Yosefu na kifo chake (22-26)

    • Amri ya Yosefu kuhusu mifupa yake (25)

50  Ndipo Yosefu akamwangukia baba yake,+ akamlilia na kumbusu.  Kisha Yosefu akawaamuru watumishi wake, matabibu, wampake baba yake dawa ili asioze. + Basi matabibu hao wakampaka dawa Israeli,  wakafanya hivyo kwa siku 40, muda kamili uliotumiwa kupaka dawa, nao Wamisri wakaendelea kumlilia kwa siku 70.  Siku za kumwombolezea zilipopita, Yosefu akawaambia hivi watu wa makao* ya Farao: “Ikiwa nimepata kibali machoni penu, mpeni Farao ujumbe huu:  ‘Baba yangu aliniapisha+ akisema: “Tazama! ninakufa.+ Nizike katika kaburi langu+ nililochimba katika nchi ya Kanaani.”+ Tafadhali, niruhusu nipande kwenda kumzika baba yangu, kisha nitarudi.’”  Farao akajibu: “Nenda ukamzike baba yako kama alivyokuapisha.”+  Basi Yosefu akapanda kwenda kumzika baba yake, alienda pamoja na watumishi wote wa Farao, wazee+ wa makao ya Farao na wazee wote wa nchi ya Misri  na watu wote wa nyumba ya Yosefu na ndugu zake na watu wa nyumba ya baba yake.+ Watoto wao wadogo na kondoo wao na ng’ombe wao ndio tu waliobaki katika nchi ya Gosheni.  Alienda pia na magari+ na wapanda farasi; lilikuwa kundi kubwa sana. 10  Kisha wakafika kwenye uwanja wa kupuria wa Atadi, katika eneo la Yordani, na huko wakafanya maombolezo makubwa sana na kulia kwa uchungu, naye akaendelea kumwombolezea baba yake kwa siku saba. 11  Wakaaji wa nchi, Wakanaani, wakawaona wakiomboleza kwenye uwanja wa kupuria wa Atadi, wakasema kwa mshangao: “Haya ni maombolezo makubwa sana ya Wamisri!” Ndiyo sababu mahali hapo paliitwa Abel-misraimu,* katika eneo la Yordani. 12  Kwa hiyo wana wa Yakobo wakamfanyia kama tu alivyokuwa amewaagiza.+ 13  Wanawe walimbeba na kumpeleka katika nchi ya Kanaani na kumzika katika pango lililo katika shamba la Makpela, shamba lililo mbele ya Mamre ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kutoka kwa Efroni Mhiti ili awazike humo watu wake.+ 14  Baada ya kumzika baba yake, Yosefu akarudi Misri pamoja na ndugu zake na wote walioenda naye kumzika baba yake. 15  Ndugu za Yosefu walipoona kwamba baba yao amekufa, wakasema: “Huenda Yosefu ana chuki kutuelekea na atatulipiza uovu wote tuliomtendea.”+ 16  Kwa hiyo wakamtumia Yosefu ujumbe huu: “Baba yako alitoa amri hii kabla ya kifo chake: 17  ‘Hivi ndivyo mtakavyomwambia Yosefu: “Nakusihi, tafadhali, wasamehe ndugu zako uovu wao na dhambi waliyokutendea ili kukudhuru.”’ Sasa, tafadhali, wasamehe watumishi wa Mungu wa baba yako uovu wao.” Na Yosefu akalia walipomwambia hivyo. 18  Kisha ndugu zake wakaja pia na kuanguka mbele yake na kumwambia: “Tazama, sisi ni watumwa wako!”+ 19  Yosefu akawaambia: “Msiogope. Je, nimechukua nafasi ya Mungu? 20  Ingawa mlikusudia kunidhuru,+ Mungu alikusudia hali hiyo ibadilike na kuwa njema na kuokoa maisha ya watu wengi, kama anavyofanya leo.+ 21  Sasa basi msiogope. Nitaendelea kuwapa ninyi na watoto wenu chakula.”+ Kwa hiyo akawafariji na kuwatia moyo. 22  Na Yosefu akaendelea kuishi Misri, yeye na watu wa nyumba ya baba yake; Yosefu aliishi miaka 110. 23  Yosefu akaona kizazi cha tatu cha wana wa Efraimu,+ pia wana wa Makiri,+ mwana wa Manase. Walizaliwa kwenye magoti ya Yosefu.* 24  Mwishowe Yosefu akawaambia ndugu zake: “Ninakufa, lakini kwa hakika Mungu atawakazia uangalifu,+ naye hakika atawapandisha kutoka katika nchi hii na kuwapeleka katika nchi aliyoapa kwamba atawapa Abrahamu, Isaka, na Yakobo.”+ 25  Basi Yosefu akawaapisha wana wa Israeli, akisema: “Kwa hakika Mungu atawakazia ninyi uangalifu. Mnapaswa kuiondoa mifupa yangu huku.”+ 26  Yosefu akafa akiwa na umri wa miaka 110, nao wakampaka dawa ili asioze,+ akawekwa ndani ya jeneza nchini Misri.

Maelezo ya Chini

Au “nyumba.”
Maana yake “Maombolezo ya Wamisri.”
Yaani, aliwatendea kama wanawe na kwa njia ya pekee.