Mwanzo 6:1-22

  • Wana wa Mungu wajichukulia wake duniani (1-3)

  • Wanefili wazaliwa (4)

  • Uovu wa wanadamu wamhuzunisha Yehova (5-8)

  • Noa aagizwa ajenge safina (9-16)

  • Mungu atangaza kuja kwa Gharika (17-22)

6  Sasa idadi ya wanadamu ilipoanza kuongezeka duniani, nao wakazaa mabinti,  wana wa Mungu wa kweli*+ wakaanza kuona kwamba mabinti wa wanadamu ni warembo. Basi wakaanza kuwachukua wote waliowachagua ili wawe wake zao.  Ndipo Yehova akasema: “Roho yangu haitamvumilia mwanadamu daima,+ kwa sababu yeye ni mwili tu.* Kwa hiyo, jumla ya siku zake itakuwa miaka 120.”+  Wanefili* walikuwa duniani siku hizo na baadaye. Wakati huo wana wa Mungu wa kweli waliendelea kufanya ngono na mabinti wa wanadamu, nao wakawazalia wana. Wana hao walikuwa watu wenye nguvu wa nyakati za kale, wanaume maarufu.  Basi, Yehova akaona kwamba uovu wa mwanadamu ulikuwa mkubwa duniani na kwamba kila mwelekeo wa mawazo ya moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.+  Yehova akaghairi* kwamba aliwaumba wanadamu duniani, na moyo wake ukahuzunika.*+  Kwa hiyo Yehova akasema: “Nitawafagilia mbali kutoka duniani wanadamu ambao nimewaumba, wanadamu pamoja na wanyama wa kufugwa, wanyama wanaotambaa, na viumbe wanaoruka angani, kwa sababu ninaghairi kwamba niliwaumba.”  Lakini Noa akapata kibali machoni pa Yehova.  Hii ndiyo historia ya Noa. Noa alikuwa mtu mwadilifu.+ Alijithibitisha mwenyewe kuwa mtu asiye na kosa* miongoni mwa watu wa siku zake.* Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.+ 10  Baada ya muda, Noa alizaa wana watatu, Shemu, Hamu, na Yafethi.+ 11  Lakini dunia ilikuwa imeharibika machoni pa Mungu wa kweli, nayo dunia ilikuwa imejaa ukatili. 12  Naam, Mungu aliitazama dunia, nayo ilikuwa imeharibika;+ watu wote walikuwa wameharibu njia yao duniani.+ 13  Baada ya hayo Mungu akamwambia Noa: “Nimeamua kuwaangamiza wanadamu wote, kwa sababu wameijaza dunia ukatili, kwa hiyo nitawaangamiza pamoja na dunia.+ 14  Jitengenezee safina* kwa mbao za mti wenye utomvu.+ Utatengeneza vyumba ndani ya safina na uifunike kwa lami+ ndani na nje. 15  Hivi ndivyo utakavyoitengeneza: Safina inapaswa kuwa na urefu wa mikono 300,* upana wa mikono 50, na kimo cha mikono 30. 16  Utatengeneza dirisha la kuingiza mwangaza kwenye safina,* mkono mmoja kutoka juu. Unapaswa kutengeneza mlango ubavuni mwake,+ na utengeneze ghorofa ya chini, ghorofa ya pili, na ghorofa ya tatu. 17  “Nami kwa upande wangu, nitaleta gharika ya maji+ duniani ili kuangamiza viumbe wote wenye pumzi ya uhai* walio chini ya mbingu. Kila kitu kilicho duniani kitaangamia.+ 18  Nami ninafanya pamoja nawe agano langu, nawe lazima uingie ndani ya safina, wewe, wanao, mke wako, na wake wa wanao.+ 19  Nawe uingize ndani ya safina viumbe hai+ wawili wawili wa kila aina ili kuwahifadhi hai pamoja nawe, dume na jike;+ 20  viumbe wanaoruka angani kulingana na aina zao, wanyama wa kufugwa kulingana na aina zao, na wanyama wote wanaotambaa kulingana na aina zao, watakuja ndani kwako viumbe wawili wawili wa kila aina ili uwahifadhi hai.+ 21  Nawe unapaswa kukusanya na kuchukua kila aina ya chakula,+ kwa ajili yako na wanyama.” 22  Basi Noa akafanya kulingana na mambo yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Hivyo ndivyo alivyofanya.+

Maelezo ya Chini

Msemo wa Kiebrania unaorejelea malaika, wana wa Mungu.
Au labda, “kwa sababu anatenda kulingana na mwili.”
Huenda neno hili linamaanisha “Waangushaji,” yaani, wale wanaowaangusha wengine chini. Angalia Kamusi.
Au “akasikitika.”
Au “naye akaumia moyoni mwake.”
Au “lawama.”
Tnn., “vizazi vyake.”
Tnn., “sanduku”; chombo kikubwa.
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Katika Kiebrania ni tsoʹhar. Baadhi ya watu wanasema kwamba tsoʹhar ni nafasi ya mkono mmoja kati ya paa na dari, si dirisha au nafasi ya kuingizia mwangaza.
Au “roho ya uhai.”