Nehemia 2:1-20

  • Nehemia aruhusiwa kwenda Yerusalemu (1-10)

  • Nehemia akagua kuta za jiji (11-20)

2  Katika mwezi wa Nisani,* mwaka wa 20+ wa utawala wa Mfalme Artashasta,+ divai ililetwa mbele yake, nami kama kawaida, nikaichukua divai hiyo na kumpa mfalme.+ Lakini sikuwahi kuonekana nikiwa mwenye huzuni mbele yake.  Ndipo mfalme akaniambia: “Kwa nini unaonekana umehuzunika sana na wewe si mgonjwa? Lazima una huzuni moyoni.” Ndipo nikaogopa sana.  Kisha nikamwambia mfalme: “Mfalme na aishi muda mrefu! Kwa nini nisiwe na huzuni wakati lile jiji, mahali ambapo mababu zangu wamezikwa ni magofu, na malango yake yameteketezwa kwa moto?”+  Ndipo mfalme akaniuliza: “Basi unataka nini?” Mara moja nikasali kwa Mungu wa mbinguni.+  Kisha nikamjibu mfalme: “Ukipenda, Ee mfalme, na ikiwa mimi mtumishi wako nimepata kibali chako, niruhusu niende Yuda, kwenye jiji ambalo mababu zangu wamezikwa ili nilijenge upya.”+  Ndipo mfalme akaniuliza hivi huku malkia wake akiwa ameketi kando yake: “Safari yako itachukua muda gani, nawe utarudi lini?” Basi jambo hilo likampendeza mfalme, akaniruhusu niende,+ nami nikamwambia muda hususa.+  Kisha nikamwambia mfalme: “Ukipenda, Ee mfalme, naomba nipewe barua niwapelekee magavana wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto,*+ ili waniruhusu kupita hadi nifike Yuda salama salimini,  pia barua nimpelekee Asafu mtunzaji wa Bustani ya Mfalme,* ili anipe mbao za kujengea mihimili ya malango ya Ngome+ ya ile Nyumba* na kuta za jiji+ na nyumba nitakayoishi.” Basi mfalme akanipa barua hizo,+ kwa sababu mkono mwema wa Mungu wangu ulikuwa juu yangu.+  Mwishowe nikafika kwa magavana wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto na kuwapa barua za mfalme. Pia, mfalme alinipa wakuu wa jeshi na wapanda farasi. 10  Sanbalati+ Mhoroni na Tobia+ ofisa* Mwamoni+ waliposikia jambo hilo, walikasirika sana kwa sababu mtu fulani alikuwa amekuja kuwatendea watu wa Israeli jambo jema. 11  Hatimaye nikafika Yerusalemu, nami nikakaa huko kwa siku tatu. 12  Nikaondoka usiku, mimi pamoja na wanaume wachache, nami sikumwambia mtu yeyote mambo ambayo Mungu wangu alikuwa ameweka moyoni mwangu ili nilifanyie jiji la Yerusalemu, wala sikuwa na mnyama mwingine ila mnyama aliyenibeba. 13  Nikatoka nje usiku kupitia Lango la Bondeni,+ nikapita mbele ya Chemchemi ya Nyoka Mkubwa, nikaelekea kwenye Lango la Marundo ya Majivu,+ nami nikachunguza kuta za Yerusalemu zilizokuwa zimebomolewa na malango yake yaliyokuwa yameteketezwa kwa moto.+ 14  Kisha nikapita kuelekea kwenye Lango la Chemchemi+ na kuelekea kwenye Kidimbwi cha Mfalme, lakini mnyama aliyenibeba hangeweza kupita kwa sababu hapakuwa na nafasi ya kutosha. 15  Hata hivyo, nikaendelea kupanda juu bondeni*+ usiku, nami nikaendelea kuukagua ukuta, nami nikaingia kupitia Lango la Bondeni, kisha nikarudi. 16  Watawala wasaidizi+ hawakujua nilikokwenda au jambo nililokuwa nikifanya, kwa sababu sikuwa nimewaambia Wayahudi jambo lolote, wala makuhani, wala wakuu, wala watawala wasaidizi, wala wafanyakazi wengineo. 17  Hatimaye nikawaambia: “Mnaona hali mbaya sana tunayokabili, jinsi Yerusalemu lilivyobaki magofu na malango yake yameteketezwa kwa moto. Njooni, tujenge upya kuta za Yerusalemu, ili aibu hii isiendelee.” 18  Kisha nikawaambia jinsi mkono mwema wa Mungu wangu ulivyokuwa juu yangu+ na pia maneno ambayo mfalme alikuwa ameniambia.+ Ndipo wakasema: “Twendeni tukajenge.” Basi wakaimarishana* ili kufanya kazi hiyo njema.+ 19  Sasa Sanbalati Mhoroni, Tobia+ ofisa* Mwamoni,+ na Geshemu Mwarabu+ waliposikia jambo hilo, wakaanza kutudhihaki+ na kutudharau wakisema: “Mnafanya nini? Je, mnamwasi mfalme?”+ 20  Lakini nikawajibu: “Mungu wa mbinguni, Ndiye atakayetufanikisha,+ nasi watumishi wake tutasimama na kujenga; lakini ninyi hamna fungu wala haki ya kudai chochote wala kumbukumbu* katika Yerusalemu.”+

Maelezo ya Chini

Au “maeneo yaliyo magharibi ya Mto Efrati.”
Au “msitu wa mfalme.”
Au “Hekalu.”
Tnn., “mtumishi.”
Au “korongoni.”
Tnn. “wakaitia nguvu mikono yao.”
Tnn., “mtumishi.”
Au “haki ya kumiliki.”