Nehemia 4:1-23

  • Kazi yaendelea licha ya upinzani (1-14)

  • Ujenzi waendelea wajenzi wakiwa na silaha (15-23)

4  Mara tu Sanbalati+ aliposikia kwamba tunajenga upya ukuta, alishikwa na ghadhabu na kukasirika sana,* naye akazidi kuwadhihaki Wayahudi.  Akasema hivi mbele ya ndugu zake na jeshi la Samaria: “Wayahudi hawa wanyonge wanafanya nini? Je, watafanya kazi hii peke yao? Je, watatoa dhabihu? Je, watamaliza kwa siku moja? Je, watayatoa mawe yaliyoungua kutoka katika marundo ya vifusi ili yafae kwa ujenzi?”+  Basi Tobia+ Mwamoni,+ aliyekuwa amesimama kando yake, akasema: “Hata mbweha akipanda juu ya kile wanachojenga, atauangusha ukuta wao wa mawe.”  Sikiliza, Ee Mungu wetu, kwa maana tunadharauliwa;+ na urudishe dharau yao juu ya vichwa vyao wenyewe,+ nawe uwafanye wawe nyara na mateka katika nchi nyingine.  Usiifunike hatia yao wala usiifute dhambi yao kutoka mbele zako,+ kwa maana wamewatukana wajenzi.  Basi tukaendelea kujenga, na ukuta wote ukaungana kufikia nusu ya kimo chake, nao watu wakaendelea kufanya kazi kwa moyo wote.  Sasa mara tu Sanbalati, Tobia,+ Waarabu,+ Waamoni, na Waashdodi+ waliposikia kwamba kazi ya kurekebisha kuta za Yerusalemu inasonga mbele na kwamba mianya ilikuwa ikizibwa, wakakasirika sana.  Wakapanga njama pamoja ili kupigana na Yerusalemu na kuleta vurugu humo.  Lakini tulisali kwa Mungu wetu na kuweka walinzi dhidi yao mchana na usiku. 10  Hata hivyo, watu wa Yuda walikuwa wakisema: “Wafanyakazi* wameishiwa na nguvu, na kuna vifusi vingi sana; hatutafaulu kamwe kuujenga ukuta.” 11  Maadui wetu wakaendelea kusema: “Kabla hawajajua au kutuona, tutaingia kati yao, tuwaue, na kuikomesha kazi.” 12  Kila mara Wayahudi walioishi karibu nao walipokuja, walikuwa wakituambia tena na tena:* “Watatushambulia kutoka kila upande.” 13  Basi nikaweka wanaume kwenye sehemu za chini zaidi zilizo wazi nyuma ya ukuta, nikawapanga kulingana na familia zao, wakiwa na mapanga yao, mikuki yao, na pinde zao. 14  Nilipoona jinsi walivyoogopa, mara moja nikasimama na kuwaambia wakuu+ na watawala wasaidizi na watu wengine wote: “Msiwaogope.+ Mkumbukeni Yehova, ambaye ni mkuu na mwenye kuogopesha;+ nanyi mpigane kwa ajili ya ndugu zenu, wana wenu na mabinti zenu, wake zenu na nyumba zenu.” 15  Sasa baada ya maadui wetu kusikia kwamba tunajua walichokuwa wakifanya na kwamba Mungu wa kweli alikuwa amevuruga mpango wao, sote tukarudi kuujenga ukuta. 16  Tangu siku hiyo na kuendelea, nusu ya wanaume wangu walikuwa wakifanya kazi+ na nusu nyingine walikuwa wakishika mikuki, ngao, pinde, na kuvaa makoti ya vita. Na wakuu+ walisimama nyuma ya watu wote wa nyumba ya Yuda 17  waliokuwa wakijenga ukuta. Watu waliokuwa wakibeba mizigo walifanya kazi kwa mkono mmoja, huku wakiwa wameshika silaha kwa mkono mwingine. 18  Na kila mjenzi alikuwa amejifunga upanga kiunoni huku akijenga, na mtu wa kupiga pembe+ alikuwa amesimama kando yangu. 19  Ndipo nikawaambia wakuu na watawala wasaidizi na watu wengine wote: “Kazi hii ni kubwa na nzito, nasi tumetawanyika kwenye ukuta kila mmoja mbali na mwenzake. 20  Mtakaposikia mlio wa pembe, kusanyikeni mahali tulipo. Mungu wetu atatupigania.”+ 21  Basi tukaendelea kufanya kazi huku nusu ya wanaume wakiwa wameshika mikuki, kuanzia mapambazuko mpaka nyota zilipoonekana. 22  Wakati huo nikawaambia watu: “Kila mwanaume na mtumishi wake na wakae ndani ya Yerusalemu usiku, nao watakuwa walinzi usiku na watafanya kazi mchana.” 23  Basi mimi, ndugu zangu, watumishi wangu,+ na walinzi waliofuatana nami hatukuvua mavazi yetu kamwe, na kila mmoja wetu aliendelea kushika silaha yake kwa mkono wa kulia.

Maelezo ya Chini

Au “aliudhika.”
Au “Wabeba mizigo.”
Tnn., “mara kumi.”