Nehemia 5:1-19

  • Nehemia akomesha ukandamizaji (1-13)

  • Nehemia hakutenda kwa ubinafsi (14-19)

5  Hata hivyo, watu na wake zao wakaanza kulalamika sana kuhusu ndugu zao Wayahudi.+  Baadhi yao walikuwa wakisema: “Sisi na wana wetu na mabinti zetu ni wengi. Tunahitaji nafaka ili tule tuendelee kuishi.”  Na wengine walikuwa wakisema: “Tunatoa mashamba yetu na mashamba yetu ya mizabibu yetu na nyumba zetu kuwa rehani ili tupate nafaka wakati wa njaa.”  Na wengine walikuwa wakisema: “Tumekopa pesa kwa kuweka rehani mashamba yetu na mashamba yetu ya mizabibu ili kulipa ushuru wa mfalme.+  Sasa sisi na ndugu zetu ni watu wa mwili mmoja na damu moja,* na watoto wetu ni sawa na watoto wao; lakini tumelazimika kuwafanya wana na mabinti zetu kuwa watumwa, na baadhi ya mabinti zetu tayari wako utumwani.+ Na hatuna uwezo wa kuzuia jambo hili, kwa sababu mashamba yetu na mashamba yetu ya mizabibu yamechukuliwa na wengine.”  Nilikasirika sana niliposikia kilio chao na maneno hayo.  Kwa hiyo nikatafakari mambo hayo moyoni mwangu, kisha nikawashutumu wakuu na watawala wasaidizi na kuwaambia: “Kila mmoja wenu anamtoza riba* ndugu yake mwenyewe.”+ Pia, nikapanga kusanyiko kubwa kwa sababu yao.  Nikawaambia: “Kwa kadiri tulivyoweza, tumewanunua ndugu zetu wenyewe, Wayahudi, waliouzwa kwa mataifa; lakini je, sasa mtawauza ndugu zenu wenyewe,+ nasi tulazimike kuwanunua tena?” Ndipo wakanyamaza kimya, hawakuwa na lolote la kusema.  Kisha nikawaambia: “Jambo mnalofanya si jema. Je, hampaswi kutembea kwa kumwogopa Mungu+ wetu ili mataifa, maadui wetu, wasitushutumu? 10  Zaidi ya hayo, mimi, ndugu zangu, na watumishi wangu tunawakopesha pesa na nafaka. Tafadhali, tuache kukopesha kwa riba.+ 11  Tafadhali, warudishieni leo hii mashamba yao,+ mashamba yao ya mizabibu, na mizeituni yao, na nyumba zao, na pia sehemu moja ya mia* ya pesa zao, nafaka, divai mpya, na mafuta mnayowadai kama riba.” 12  Ndipo wakasema: “Tutawarudishia vitu hivyo bila kuwadai chochote. Tutafanya sawasawa na ulivyotuagiza.” Basi nikawaita makuhani na kuwaapisha wanaume hao ili watimize ahadi hiyo. 13  Pia, nikakung’uta vazi langu* na kusema: “Mungu wa kweli na amkung’ute hivi kutoka nyumbani mwake na kutoka katika mali zake kila mwanamume ambaye hatatimiza ahadi hii, na akung’utwe hivi na kubaki bila chochote.” Ndipo kutaniko lote likajibu: “Amina!”* Wakamsifu Yehova, na watu wakafanya kama walivyoahidi. 14  Isitoshe, tangu siku mfalme aliponiteua kuwa gavana+ katika nchi ya Yuda, kuanzia mwaka wa 20+ mpaka mwaka wa 32+ wa utawala wa Mfalme Artashasta,+ miaka 12, mimi na ndugu zangu hatukula chakula kilichokuwa haki ya gavana.+ 15  Lakini magavana walionitangulia waliwalemea watu, kila siku walichukua kutoka kwao shekeli 40 za fedha* kwa ajili ya mkate na divai. Pia, watumishi wao waliwakandamiza watu. Lakini mimi sikufanya hivyo+ kwa sababu nilimwogopa Mungu.+ 16  Isitoshe, mimi pia nilishiriki kujenga ukuta huu, nasi hatukuchukua hata shamba moja;+ watumishi wangu wote walikusanyika hapo ili kufanya kazi. 17  Kulikuwa na Wayahudi na watawala wasaidizi 150 waliokula kwenye meza yangu, na pia watu waliokuja kwetu kutoka mataifa jirani. 18  Kila siku nilitayarishiwa* ng’ombe dume mmoja, kondoo sita walio bora, na ndege wengi, na kila baada ya siku kumi tuliandaliwa kwa wingi divai ya kila aina. Licha ya hayo sikudai chakula kilichokuwa haki ya gavana, kwa kuwa tayari watu walikuwa wamelemewa na kazi. 19  Ee Mungu wangu, nikumbuke na kunitendea wema,* kwa ajili ya yote niliyowatendea watu hawa.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “nyama ya mwili wa ndugu zetu ni sawa na nyama ya mwili wetu.”
Au “faida.”
Au “asilimia moja,” yaani, kila mwezi.
Au “Na iwe hivyo!”
Tnn., “nikatikisa kifua changu.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “Kila siku nilitayarishiwa kwa gharama yangu.”
Au “na kunipa kibali.”